November 18, 2013


Kocha Mkuu wa Kenya, Adel Amrouche, amechukizwa na kufutwa kwa mchezo wa timu yake dhidi ya Taifa Stars, lakini akawaomba radhi wananchi wote wa Tanzania.


Stars ilipaswa kucheza na Kenya, kesho Jumanne kwenye mchezo wa kirafiki Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, lakini mtanange huo umeahirishwa kutokana na matatizo ya mawasiliano, hivyo Stars itakipiga na Zimbabwe kesho kwenye uwanja huo.

Amrouche raia wa Ubelgiji, amesema taarifa za kufutwa kwa mchezo huo zimemkosesha raha, kwani alitarajia Stars ingekuwa kipimo kizuri kwa kikosi chake.

Amrouche aliyewahi kuifundisha Burundi kabla ya Kenya, amesema kikubwa kilichosababisha mechi hiyo kufutwa ni tatizo la mawasiliano kati ya Chama cha Soka cha Kenya (KFF) na nyota aliowataka kujiunga na timu hiyo.
“Nawaomba radhi Watanzania wote, sikutarajia kama hilo lingeibuka, nilitarajia kupata upinzani mzuri kutoka kwa Tanzania, kitu ambacho sasa kimekosekana,” alisema Amrouche na kuongeza:

“Kuna moja ambalo limesababisha kuahirishwa kwa mechi hiyo, chama cha soka huku hakikuwa na mawasiliano mazuri na klabu ambazo wachezaji wake niliwachagua, kitu ambacho kilisababisha hata kambi yetu kuchelewa.”

Kwa mujibu wa taarifa iliyotumwa jana na Kaimu Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kiingilio cha chini cha mchezo huo wa kesho ni Sh 5,000.

“Mbali ya kiingilio hicho cha Sh 5,000 ambacho ni kwa viti vya bluu na kijani, viingilio vingine ni Sh 30,000 kwa VIP A, Sh 20,000 kwa VIP B, Sh 15,000 kwa VIP C, wakati viti vya rangi ya chungwa ni Sh 10,000,” alisema Wambura.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic