November 11, 2013


Hadi mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Bara unamalizika, tumeona namna kikosi cha Mbeya City chini ya Kocha Juma Mwambusi ambavyo kimekuwa gumzo kutokana na uwezo wake mkubwa wa kucheza soka.


Achana na kwamba Mbeya City imemaliza mzunguko wa kwanza ikiwa katika nafasi ya tatu juu ya timu kama Simba, lakini bado ilionyesha soka safi na la kuvutia kwa kila timu iliyokutana nayo.

Angalia kwa timu kongwe kama Yanga, Simba na Azam FC ambayo imekuwa ni moja ya timu ngumu, kati ya hizo hakuna ambayo imeifunga Mbeya City, kila moja imeambulia sare na ukiangalia sare mbili timu hiyo imepata ikiwa ugenini dhidi ya Simba na Azam FC.

Ligi imefikia tamati katika mzunguko wa kwanza na imeacha mambo mengi sana ambayo yanatakiwa kufanyiwa kazi kama somo na si kuachwa yapite.

Mbeya City hadi ilipofikia haikuwa ni kitu cha kukaa na kuota tu, badala yake walifanya kazi. Kwao ni watu wanaotakiwa kutobweteka na kufikiri mambo yalienda kwa kuhatisha tu au walipofikia ndiyo mwisho, ligi haijaisha.

Kwa timu nyingine, zikiwemo zilizo katika nafasi za chini lazima ziamini kuwa mzunguko wa kwanza umekuwa na changamoto, hivyo somo ni kuangalia wapi waliteleza na nini cha kufanya kwa kipindi hiki cha mapumziko ya ligi.

Simba na Yanga pia, ni timu kongwe lakini imeonekana wazi kwamba mzunguko wa kwanza umekuwa mgumu kwao na ukongwe wao haukuonekana kama inavyotakiwa.

Angala Yanga ilianza ligi kwa kusua, ikaenda inabadilisha gia hadi kufikia ilipokuwa na imemaliza inaongoza. Lakini Simba ilianza vizuri na mwisho ikaenda inaporomoka kila kukicha na imeishia katika nafasi ya nne.

Huu ni wakati wa mapumziko, lakini hakuna mtu makini awe mchezaji, kocha au kiongozi anaweza kupumzika na kulala eti kwa kuwa ndiyo kipindi cha kupumzika kimefika. Inawezekana kupumzika lakini kazi nzuri hufanywa katika kipindi cha utulivu.

Ninamaanisha hivi, kila mmoja kwenye upande wake anapaswa kujitathmini, kwamba alichezaje, alifundishaje, aliongozaje na baada ya hapo ni nini cha kufanya.

Wachezaji wanapaswa kufanya mazoezi ya ziada ili kukabiliana na mzunguko wa pili wa lala salama ambao huwa mgumu zaidi kwa kuwa ni sawa na mtihani shule, kwamba itajulikana umepata daraja lipi.

Kwa makocha, huu si wakati wa soka tu, wasome, waangalie walichofanya na nini cha kuongeza. Maneno mengi halafu uwezo wa kazi hakuna pia si kitu kizuri. Kwa upande wa viongozi pia nao wanapaswa kuangalia waliposhindwa kuziongoza vizuri timu zao.

Vizuri itakuwa kiwango kilichoonyeshwa mzunguko wa kwanza, kipande zaidi katika mzunguko wa pili na hakiwezi kupanda kama sikukuu itakuwa ndefu na wachezaji, makocha na viongozi  watalala hadi kusubiri siku chache kabla ya ligi kuanza, eti ndiyo waanze kujiandaa.
Ndoto ya mafanikio katika kitu chochote ndiyo jambo la kwanza la msingi, kwamba nataka kufanya hivi, kufikia hapa. Lakini siku zote hicho hakiwezi kufanikiwa kama ufanisi ni ziro.

Ndani ya ufanisi kuna juhudi na maarifa, kama hauna maarifa umekwama lakini haujitumi, mwisho utaishia kusema umepigwa misumari na huo utakuwa mwisho wako. 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic