November 29, 2013


 

Na Saleh Ally
Nusu msimu baada ya kumuacha Juma Kaseja ikidai ameshuka kiwango, Simba imekuwa na matatizo makubwa katika nafasi ya kipa.


Lawama kwamba Kaseja alikuwa anaachwa kutokana na masuala ya siasa za soka na wala si uwezo zilipingwa vikali na viongozi hasa wale wa kamati ya usajili ya Simba.

Sasa hakuna ubishi tena kwamba siasa zimewaumbua Simba, kwamba Kaseja hakuwa ameshuka kiwango na badala yake kipa Mganda Abel Dhaira aliyekuwa anawekewa nafasi ya kucheza ndiyo hakuwa na kiwango kizuri.

Tayari Simba iko katika hatua za mwisho za kuachana na Dhaira na haina ujanja wa kumpata Kaseja na badala yake imelazimika kumsajili kipa Yaw Berko aliyewahi kudakia Yanga.

Berko raia wa Ghana aliletwa nchini na Kocha Mserbia, Kosta Papic ambaye aliwahi kufanya naye kazi nchini humo kabla ya kutua nchini na kuifundisha Yanga.

Berko anakuja nchini kuifanyia Simba kazi kwa nusu msimu na baada ya hapo hatakuwa na ujanja maana atalazimika kuondoka nchini baada ya kuanza kwa kanuni mpya ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), timu kutosajili makipa wa kigeni.

Berko si mgeni katika soka nchini, anajulikana kwa mambo kadhaa lakini matatu yanaweza kuwa maarufu zaidi kuhusiana naye.

Kwanza ni mpole na anayetumia muda wake mwingi kusajili, muoga wa ushirikina, mwenye tabia ya kususa lakini anajulikana kuwa ni kipa mwenye uwezo wa juu na Simba inaweza kufaidika na yale ambayo ni mazuri.

Kusali:
Ni nadra kumuona Berko akiwa hana rozali shingoni mwake, mara nyingi amekuwa akitumia muda mwingi akiwa na Biblia.
Muumini huyo Mkristo ni mtaratibu na mara nyingi hupenda kuwa peke yake, katika mahojiano yake huko nyuma na gazeti hili amewahi kusema hawezi kuanza mazoezi au kucheza mechi bila ya kumuomba Mungu na kila anapomaliza lazima afanye hivyo.
Ushirikina:
Pamoja na kuwa mcha Mungu kwa sana, Berko amekuwa na sifa ya kuhofia ushirikina kupita kiasi, huenda ni kutokana na nchi ya Afrika Magharibi anayotokea.

Aliwahi kulalamika hadharani kuwa kipa mwenzake wakati huo, Shabani Kado alikuwa anamfanyia vitendo vya kishirikina ndiyo maana akawa anashindwa kudaka vizuri.

Kutokana na hali hiyo ukazuka mtafaruku kati ya Berko na Kado lakini uongozi wa Yanga ukaingilia na kulifukia suala hilo lakini siku chache baadaye Kado aliachwa na Mghana huyo akaendelea kubaki Yanga.

Kususa:
Suala la kususa limekuwa ugonjwa wake mkuu, lakini hadi anaondoka Yanga alishika nafasi ya kuwa kipa ‘anayedeka’ kuliko wote katika timu 14 zinazoshiriki ligi kuu.

Mfano amekuwa mgonjwa wa bega, lakini anapoona mashambulizi makali yanaelekezwa langoni mwake,ni rahisi sana kusema anasikia maumivu na kutoka.

Hali hiyo ilikuwa inamuudhi sana Papic na aliwahi kuizungumzia lakini mara ilipoonyesha kumuudhi Ernie Brandts baada ya Berko kusema bega linamuuma anataka kutoka, basi hakumrudisha tena na moja kwa moja akaamua kumpa nafasi ya kipa wa kwanza Ally Mustapha ‘Barthez’.

Baada ya hapo ndiyo safari ya Berko kurejea Ghana ikamkuta kwa kuwa ilionekana Brandts ameamua kumtumia Mtanzania huyo aliyetokea Simba kama kipa namba mbili.

Uwezo:
Hakuna ubishi kila mtu ana uwezo wa kuchagua lakini namba ya Berko kwa makipa katika ligi kuu ni moja au mbili na mshindani wake mkubwa anaweza kuwa Kaseja.

Berko ana uwezo wa juu kabisa na alionyesha hilo akiwa Yanga hata pale safu ya ulinzi ilipoonekana kupoteza uelekeo.

Berko ni mzuri kudaka mipira ya krosi inayoelekezwa langoni mwake lakini ana kasi zaidi katika kupangua mipira ya pembeni.
Burudani zaidi kutoka kwa Berko ni ‘timing’ ya kuziba lango hasa anapokuwa amebaki na mshambuliaji mmoja ambaye anajaribu kufunga.

Pamoja na hapo, kipa huyo hauwezi kumuondoa katika tatu bora ya makipa wenye uwezo mkubwa wa kudaka mikwaju ya penalti na alilionyesha hilo Yanga ilipocheza na Simba katika fainali ya Ngao ya Jamii, mwaka juzi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic