November 15, 2013

LUIZIO KAZINI


Na Saleh Ally
Tayari taarifa za timu fulani kumtaka huyo na nyingine kumtaka yule, zimeanza kwa kasi katika vyombo mbalimbali vya habari.


Inajulikana wazi timu mbili za Simba na Azam FC zimekuwa zikihaha kupata makocha, hata kama viongozi watakataa kama ilivyo kawaida ya wengi, lakini ukweli ni kwamba zinaendelea kufanya mazungumzo na makocha kadhaa.

Pamoja na kuendelea kufanya mazungumzo na makocha kadhaa, suala la kutaka kusajili wachezaji halijasimama na wale wanaofanya vizuri kwenye Ligi Kuu Bara watakuwa ni kati ya wanaowindwa sana.
 
YEYA
Washambuliaji wameendelea kuwa tatizo kwa Tanzania, hasa kwa wazawa. Lakini safari hii imeonekana hivi, wazawa wa Yanga, Azam FC na Simba wamekuwa hawana kasi kubwa sana ya upachikaji mabao kama ilivyo kwa wageni.

Wageni kutoka timu hizo tatu ndiyo wanaonekana kuwa na uwezo wa juu zaidi huku wakishindana na wazawa walio katika timu nyingine kama Mbeya City, Ruvu Shooting na Kagera Sugar.
 
THEMI FELIX
Mrundi wa Simba, Amissi Tambwe ndiye anaongoza kwa upachikaji mabao, sasa ana mabao 10 akiwa kileleni na anafuatiwa na Elius Maguri wa Ruvu Shooting akiwa mzawa wa kwanza msimu huu kufikisha mabao tisa.

Halafu Mganda wa Yanga, Hamis Kiiza mwenye nane, sawa na mzawa mwingine, Juma Luizio wa Mtibwa Sugar na chini ya hapo unamkuta Kipre Herman Tchetche, raia wa Ivory Coast mwenye mabao saba.

Mabao sita kushuka chini, utawakuta wazawa wakiwa kwa wingi wakipambana na wageni wachache kama Didier Kavumbagu wa Yanga kutoka Burundi mwenye mabao matano na Mkenya, Jerry Santo wa Coastal Union mwenye manne.

Wazawa wengine ambao wanaonyesha kasi kidogo ni Mrisho Ngassa (Yanga) na Themi Felix (Kagera Sugar), kila mmoja akiwa ana mabao sita.

Hii ni dalili kwamba timu zenye nguvu ya fedha lazima zitaelekeza nguvu zao kwa wachezaji wazawa wenye uwezo mkubwa wa kufunga mabao ambao katika mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Bara wameonyesha wanaweza.

Hakuna ubishi Maguri wa Ruvu Shooting atakuwa anayeonekana zaidi na hakuna ubishi huenda kuna timu zimeanza naye mazungumzo tayari. Mwingine ni Luizio wa Mtibwa Sugar, mwenye mabao nane na ukiangalia wazawa hawa ndiyo waliowapiku washambuliaji wa kigeni waliosajiliwa kwa mamilioni ya fedha pamoja na wazawa wenye majina makubwa.

Lakini kasi ya wengine wawili ambao ni Felix wa Kagera Sugar na Mwagane Yeya wa Mbeya City siyo ya kitoto. Hao ni kati ya washambuliaji wanaozungumzwa hivi sasa. Mvuto wao ni kupachika mabao, kitu ambacho kitatakiwa na timu yoyote ile.

Kila mchezaji anafanya juhudi ili kufanikiwa zaidi na maana yake sahihi ni kupata maslahi zaidi. Ni kwamba, kama itatokea mmoja au wawili kusikia wanatakiwa na Yanga, Simba au Azam FC, basi hawatasita kukimbilia mara moja hilo dau, ndiyo maisha, wafanye nini!

Pamoja na hivyo, labda Felix ambaye ni mkongwe sasa hivi, lakini wale ambao ndiyo msimu wa kwanza wanaonyesha cheche zao, vizuri pia wakajifanyia tathmini na kuangalia kama wanapaswa kujiunga na timu hizo. Kwamba sasa ni wakati mwafaka?

Kwa kuwa wanaweza kukimbilia fedha halafu ukawa ndiyo mwisho wao, maana kuna mifano kadhaa mmekuwa mkiiona.

Angalia wakati ule Shija Mkina na Simba, alikuwa tegemeo Kagera Sugar lakini Simba ikaonekana kama alikuwa hana msaada. Mfano mwingine mzuri wa hivi karibuni ni Hussein Javu ambaye alitokea Mtibwa Sugar na kujiunga na Yanga.

Alikuwa tishio na hata Yanga walikuwa wanamhofia, wakafanya juhudi kubwa na siku chache baadaye wakafanikiwa kumpata. Lakini sasa hata benchi tu imekuwa ni bahati kwake kupata nafasi ya kukaa pale.

Sasa jiulize kutokea tegemeo katika timu kama Mtibwa Sugar hadi kukosa hata nafasi angalau ya kukaa benchi tu Yanga. Hii si sawa kwa mchezaji anayetaka kuendelea.

Hapa kuna mawili, huenda uongozi ulikurupuka na kumsajili kupitia kamati yake ya usajili bila ya mapendekezo ya benchi la ufundi lakini pili, mchezaji mwenyewe hakupima kwamba wapi pa kwenda na kama ni Yanga, ilikuwa ni wakati mwafaka?

Usajili wa mikataba unaanza kabla ya dirisha dogo halijafunguliwa, sasa ni wakati mwafaka kwa wachezaji kupima mambo kwamba walipo au wanapotaka kwenda kwa kipindi husika ni wapi sahihi? “Akili mkichwa”.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic