November 1, 2013


Pamba ya Mwanza, RTC Shinyanga, Ushirika Moshi, RTC Kigoma, Lipuli Iringa, Majimaji Songea na timu nyingine kibao ambazo zimebaki majina, leo zinaenziwa na Mbeya City.

Vuta subira, twende taratibu nikueleze. Wakati huo nakumbuka nikiwa shule ya msingi, timu zilizokuwa zinafanya vizuri ukiacha Simba na Yanga, zilikuwa ni zile zilizokuwa chini ya mashirika mbalimbali kama RTC na mengine.


Wachezaji wake walikuwa bora, walikuwa tayari kupambana kwa kila namna kuhakikisha timu zao zinatamba kwa kuwa walikuwa na uhakika wa ajira zao, maana yake uendeshaji wa maisha haukuwa wa kusuasua tena.

Hili unaweza kuliona si muhimu sana, lakini wakati ule timu kama Mwadui Shinyanga ilikuwa inamiliki ndege yake, hakuna anayesema.

Pamba ya Mwanza ndiyo ilikuwa inaongoza kwa kukodi ndege, mfano ilikwenda Songea, ikatua mchana, moja kwa moja ikaenda uwanjani na kuiadhibu Majimaji na baada ya hapo ikarudi kwenye ndege na kupaa kurejea Mwanza.

Leo ukisikia timu imepanda ndege, basi ni kati ya hizi, Yanga, Simba au matajiri Azam FC. Timu nyingine hata safari za kawaida kwenda kwenye vituo vya ligi, imekuwa tatizo kubwa.

Simba na Yanga zina uhakika kwa kuwa nazo zimepewa mabasi na wadhamini, lakini kabla ya hapo, usafiri wao ulikuwa ni wa kuungaunga tu, oh! Hapa nilikuwa nakumbushia tu.

Maana hata baada ya mashirika kuachana na timu hizo, zilitua mikononi mwa wananchi na zikaendelea kufanya vizuri, nakumbuka RTC Shinyanga ilibadilishwa na kuwa Biashara Shinyanga.

Tatizo lililotokea ni ubinafsi na watu wote wa Tanzania kuamini unapokuwa shabiki wa soka, eti lazima upende Yanga au Simba, kitu ambacho ni sawa na kutumia hoja chakavu ili kutetea jambo la msingi.

Wananchi wa mikoani walikosa uzalendo na nguvu zao wakazielekeza kwenye ushabiki wa Simba na Yanga ambazo hazitokei mikoani walipo wenyewe.

Leo watu wa Mbeya wamebadilika, wamezinduka na wanaonyesha upendo unatakiwa kuanzia nyumbani, wanaipenda kwa dhati na kuiunga mkono timu yao ya Mbeya City.

Mbeya City ndiyo imepanda daraja hadi Ligi Kuu Bara lakini sasa inatoa ushindani mkubwa kwa kuwa inapata sapoti kubwa sana. Angalia mechi ya juzi ya Mbeya ‘derby’ dhidi ya Prisons, Uwanja wa Sokoine ulijaa utafikiri ni Simba na Yanga.

Wengine katika mikoa kama Mwanza, Arusha, Shinyanga, Rukwa na kwingine, wala msione aibu kufuata wanachofanya watu wa Mbeya kipindi hiki. Siwaungi mkono kwa zile vurugu zilizotokea baada ya mechi dhidi ya watani wao Prisons, lakini wanastahili sifa kwa kuiunga mkono timu nayo.

Mkoa mzima kutokuwa na timu hata moja katika ligi kuu au daraja la kwanza ni aibu kubwa, hasa kwa mikoa ambayo ina historia ya juu kuhusiana na soka. Mfano Mwanza, Kigoma, Dodoma, Iringa na Morogoro ambayo pamoja na kuwa na Mtibwa Sugar inastahili kuwa na Moro City au Moro Municipal.

Najua ninawaudhi lakini lengo ni kuwakumbusha kwamba, kuna kila sababu ya kuukuza mpira nchini kwa kuwa na timu nyingi bora kutoka katika maeneo mengi.
Hakuwezi kuwa na maendeleo kwa kila Mtanzania mpenda soka kushangilia Simba au Yanga pekee na kama ni uzalendo, basi uanzie sehemu mnazotokea.

Zisaidieni timu zenu kwanza na Yanga na Simba mnaweza kuzishangilia pia, lakini wahusika wakuu wa klabu hizo kongwe ni watu wa Ilala na Dar es Salaam kwa jumla.

Inawezekana mwanzo mlipuuzia kuhusiana na hilo, Mbeya City na wananchi wa Mbeya wamewazindua na kuwaonyesha kwamba inawezekana. Kitu kizuri ni hiki, kuiga maendeleo si dhambi, hivyo mnaweza kuwafuata kwa kukimbiza mgongo wao ili kuleta mabadiliko katika soka.

 SOURCE: CHAMPIONI


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic