November 1, 2013


Hapa nyumbani suala la waamuzi kulaumiwa sana linakua kila kukicha, ajabu kila mwamuzi anayeingia kwenye mgogoro wa namna hiyo siku chache baadaye hupotea.


Mwamuzi anayebainika kuwa ameharibu, baada ya siku chache hupotea kabisa, labda aibuke baadaye sana. Huenda kuna kitu cha kujifunza kwa waamuzi wa Ligi Kuu Bara kwani mambo ni tofauti kwa Howard Webb ambaye anaonekana ni wa aina yake, kwani pamoja na lawama nyingi kila kukicha, kama utazungumzia mwamuzi mahiri zaidi katika Ligi Kuu England, hakika hautamkwepa Webb.

Webb ndiye mwamuzi mwenye mafanikio zaidi nchini humo kwa kipindi hiki, lakini ndiye anaongoza kwa kulaumiwa zaidi kuliko mwingine yeyote.

Hata kimataifa, yeye ndiye mwenye mafanikio makubwa na mfano mzuri ni mwaka 2010 alipopewa nafasi ya kuwa mwamuzi bora duniani, kwani ndiye alishika kipenga wakati wa fainali ya Kombe la Dunia kati ya Hispania waliochukua ubingwa na Uholanzi.

Kama hiyo haitoshi, inaonekana yeye ndiye anaaminiwa zaidi katika fainali mbalimbali kubwa na maarufu kama ile ya Ligi ya Mabingwa Ulaya mwaka 2010, Kombe la FA 2010 na 2006 na  Kombe la Ligi 2007 na ndiye anaongoza kwa kupewa mechi zinazoonekana zina ushindani zaidi Premiership.

Hata hivyo, Webb amekuwa akiambiwa apunguze kumwaga kadi kama njugu, hasa za njano, tena amekuwa akifanya hivyo huku akicheka.

Baadhi ya makosa amekuwa akifanya na kukubali kuwa aliboronga, lakini kwingine anashikilia msimamo wake. Mambo ni mengi, baadhi wamekuwa wakisema ni shabiki mkubwa wa Manchester United.

Askari:
Alikuwa askari polisi wa cheo cha sajenti kabla ya kuamua kuachana na kazi hiyo na kuwa mwamuzi. Hali yake ya kujiamini sana inaelezwa inatokana na mafunzo yake ya uaskari.

Baba:
Baba yake mzazi, Billy Webb, alikuwa ni mwamuzi mahiri kwa kipindi cha miaka 35 na alikumbana na kashkash kibao kama zile anazopata mwanaye katika kipindi hiki.

Man United:
Amekuwa akisisitiza yeye si shabiki wa Man United na wengi kuamini anaishabikia timu hiyo, ilitokana na Kocha Alex Ferguson kumtetea kuhusiana na uamuzi wake wa kuipa timu yake penalti ambayo wengi walikuwa wanaipinga.

Yeye ni shabiki wa timu inayojulikana kwa jina la Rotherham United ambayo imekuwa ikishiriki ligi za chini kama daraja la kwanza, la pili, tatu na mengine.

Webb amekuwa hajifichi kuhusiana na ushabiki wake katika timu hiyo ambako ndiko alizaliwa na siku zote amekuwa akisisitiza yeye na Man United ni vitu viwili tofauti.

Nje:
Nje ya soka, Webb ana maisha yake, ameoa, baba wa watoto watatu na amekuwa akionekana mara kadhaa na familia yake katika sehemu mbalimbali, hali inayoonyesha ni baba bora.

Juni 2011, Webb alipewa urais wa Ligi ya Baris Northern Counties East ambayo aliwahi kufanya kazi kama mwamuzi pia.
Ana digrii ya udaktari aliyopokea katika Chuo Kikuu cha Bedfordshire na digrii nyingine ya heshima ya masuala ya sayansi ya afya aliyoipokea katika Chuo Kikuu cha York St John.

Makosa:

Moja:
Webb ana makosa yake kama binadamu wengine, lakini yako kadhaa ambayo hayatasahaulika kama lile la mwaka 2009 alipochezesha fainali ya Kombe la FA kati ya Man United na Tottenham.

Wakati Spurs wakiongoza kwa mabao 2-0, alitoa penalti ya utata kwa Man United ambayo ilisaidia kuamsha nguvu ya vijana wa Ferguson na kuwashusha Spurs ambao mwisho walipigwa 5-2 na United wakawa mabingwa.

Kweli baadaye alikiri kuwa alichofanya hakikuwa ni sahihi na aliipa United penalti kwa mizengwe akiamini kuwa ilikuwa ni sahihi kumbe siyo.

Mbili:
Mapema mwaka 2009, Webb aliugonga mpira uliopigwa na Radhi bila ya kutegemea ukamfikia Michael Kightly wa Wolverhampton aliyetoa pasi nzuri iliyozaa bao la pili na kuimaliza Birmingham.

Katika mechi hiyo, tayari kipindi cha kwanza alitoa penalti isiyo sahihi baada ya Marcus Bent kuanguka katika eneo la hatari lakini haikuwa hivyo. Akakubali lilikuwa ni kosa.

Birmingham walipoteza mchezo huo na ikaonekana tatizo ni hilo bao la pili ndilo lililowaua na kosa la Webb lililaumiwa hata na waamuzi wengine kwamba mwamuzi anapaswa kuwa makini kuepuka kuingilia mchezo.

Tatu:
Februari 2012 alitoa penalti kwa Manchester United ikasawazisha katika mechi yake dhidi ya Chelsea na matokeo yakawa 3-3. Kocha wa Chelsea wakati huo, Andre Villa Boas, akalalama na kusema Webb aliwauma.

Ikaonekana kama kocha huyo alikuwa na jazba kama ilivyozoeleka, lakini mwisho uchunguzi ukaonyesha United hawakustahili kupata mkwaju huo.

TAKWIMU ZA WEBB MSIMU HUU:

MECHI 30
NJANO 110
NJANO YA PILI 0

NYEKUNDU 4

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic