December 20, 2013





Na Waandishi Wetu
UNAIKUMBUKA sare ya maajabu ya mabao 3-3 ya Oktoba 20, mwaka huu? Sasa hiyo cha mtoto, kesho ndiyo kesho kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, wababe hao wa Tanzania wanakutana kwa mara nyingine kwenye dimba hilohilo katika mechi ya Nani Mtani Jembe.


Mengi yanazungumzwa lakini machache ambayo ni gumzo ni Emmanuel Okwi kuruhusiwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuichezea Yanga katika mtanange huo, huku Kocha wa Simba, Zdravko Logarusic akisema Okwi ambaye ametua jana jijini, kwake siyo tatizo na kudai dawa yake ipo na amewataka mashabiki wa Simba wasiwe na hofu hata kidogo.

Okwi atua aruhusiwa kucheza
Okwi alitua jana majira ya saa kumi katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar, ambapo alipokewa na umati mkubwa wa mashabiki wa Yanga wengi wao wakiwa wamevaa jezi za njano zenye jina la Okwi, huku wakiimba “Rage bado Kapombe, Rage bado Kapombe.”

Alipowasili ilibidi apitishiwe mlango wa watu maarufu ‘VIP’, akiwa amevalishwa jezi yenye namba 25, Okwi alizungumza machache kwa kusema: “Nawashukuru Simba kwa kipindi chote tulichokuwa pamoja, nimerejea Tanzania kuja kufanya kazi na ninaamini mechi ya Jumamosi timu yangu ya Yanga itaibuka na ushindi.”

Wakati akitoka uwanjani hapo ilibidi askari polisi waongezeke kumlinda kutokana na mashabiki wengi kugombania kumsalimia kwa kumgusa na kumkumbatia.

Upande mwingine, Mkurugenzi wa Mashindano wa TFF, Saad Kawemba, ameliambia gazeti hili kuwa, wamepokea pingamizi la kumzuia Okwi kutoichezea Yanga kutoka kwa Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage, juzi lakini akasisitiza Yanga ikiamua kumtumia ni ruksa.

“Hakuna kitu kinachoitwa ITC feki, ITC ikitoka imetoka, hilo watu wanatakiwa kujua, tumepokea pingamizi la Rage kuhusu Okwi. Rage ametumia haki yake ya kidemokrasia kuwasilisha pingamizi kwa kuwa tupo katika kipindi cha mapingamizi kinachomalizika Desemba 23.

“Kuhusu Okwi kucheza Jumamosi hakuna tatizo kwa kuwa mechi hiyo siyo ya kimashindano, unakumbuka (Mrisho) Ngassa aliichezea Seattle Sounders ya Marekani dhidi ya Manchester United licha ya kuwa alikuwa ni mali ya Azam FC, kumtumia au la huo ni uamuzi wa Yanga,” alisema Kawemba.  

ITC ni Hati ya Uhamisho wa Kimataifa ambayo inamruhusu mchezaji kuhama kutoka timu moja kwenda nyingine katika nchi tofauti.

Simba kutumia mifumo mitatu
Loga amesema ana mifumo mitatu atakayoitumia kuwamaliza Yanga lakini akagoma kuitaja ili Kocha wa Yanga, Ernie Brandts asijue janja yake na kuitegua. “Nimepanga kutumia mifumo mitatu tofauti katika mechi moja, sitakutajia kwa kuwa nitakuwa najimaliza mwenyewe,” alisema.

Vita ya Berko, Ivo ni ngumu
Inaelezwa kuwa, Loga bado hajafanya uamuzi wa kipa wa kumtumia na kuwa chaguo la kwanza kati ya Yaw Berko na Ivo Mapunda ambao wote wametua klabuni hapo hivi karibuni.

Loga amesema: “Ninahitaji muda zaidi wa kuangalia uwezo wa kila kipa akiwa golini kabla ya kuamua yupi anafaa kuwepo kwenye kikosi changu cha kwanza nitakachokitumia kwenye mzunguko wa pili.”

Yanga bado waota sare ya maajabu
Beki wa Yanga, Mbuyu Twite amesema Simba wasitarajie kupata mchekea wa kusawazisha mabao kama ilivyokuwa katika mechi ya 3-3, licha ya Yanga kuongoza kwa mabao 3-0 mpaka mapumziko.

“Simba wasitarajie kuwa tutarudia makosa ya mechi iliyopita ya kuwafunga mabao matatu na baadaye wanarudisha yote, kiukweli wasahau hilo,” alisema.

Chollo, Telela waondolewa
Kiungo Salum Telela wa Yanga na beki wa Simba, Said Masoud ‘Chollo’ kwa nyakati tofauti wameondolewa katika timu zao na hawatakuwepo kwenye mechi hiyo kutokana na kuwa majeruhi.

Eti Okwi alikuwa tishio kwa Cannavaro!
Nahodha wa Yanga, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ amefunguka kuwa Okwi ndiye mchezaji pekee aliyekuwa akimsumbua wakati alipokuwa Simba.

“Niseme ukweli nimepokea kwa furaha sana taarifa za ujio wa Okwi, katika maisha yangu ya soka Okwi alikuwa akinisumbua kila nilipokuwa nikikutana naye lakini sasa presha hiyo sina tena, nawapongeza sana viongozi wa klabu waliofanikisha hili,” alisema Cannavaro.

Wachezaji ‘full’ tambo
Jerry Tegete wa Yanga: “Tumejipanga vizuri kuhakikisha tunapata ushindi, kutokana na maandalizi ya nguvu tunayofanya na kocha wetu.”

Juma Kaseja wa Yanga: “Sina hofu ya mechi hiyo kutokana na uzoefu mkubwa nilionao wa kuzichezea timu hizi mbili.”

Amissi Tambwe wa Simba: “Kesho mpaka kieleweke, ushindi ndiyo lengo letu, tuna maandalizi mazuri.”

Ivo Mapunda wa Simba: “Nitazingatia kile kilichonileta Simba ili niweze kufanya vizuri na kitu cha msingi cha kuzingatiwa ni ushirikiano kutoka kwa wachezaji, viongozi na wanachama kwa jumla.”

Didier Kavumbagu wa Yanga: “Unapohitaji kufunga hauna sababu ya kuangalia nani anakukaba au anayedaka, kwa hiyo uwepo wa Berko haunitishi.”

Yanga wajifua kwa penalti, mashuti
Kikosi cha Yanga, jana kilikuwa katika mazoezi makali lakini cha kuvutia katika mazoezi hayo ni upigwaji wa penalti na mashuti makali katika Uwanja wa Bora, Kijitonyama jijini.

Kaseja alifungwa mashuti 18, akaokoa 11, akiteswa zaidi na Nizar Khalfan wakati Barthez akifungwa mashuti 21, akiokoa 10, akiteswa na Didier Kavumbagu na Hussein Javu.

Tegete alikuwa kinara katika penalti kwa kumtesa Kaseja, ambapo jumla Kaseja alifungwa mikwaju nane huku akipangua penalti za Athuman Idd ‘Chuji’, Mrisho Ngassa huku Barthez akicheza nne.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic