December 20, 2013





Na Saleh Ally
JUZI Jumatano, Mzee Small alieleza namna alivyoshindwa kuvumilia na kumtimua mganga aliyekuwa akimtibu tena kwa kumshikia panga, hali hiyo ilitokana na wao kutoelewana. Nini kilifuata baada ya hapo?

Endelea na Mzee Small…
HATA hivyo haikuwa kazi rahisi Mzee Small kumfukuza mganga huyo kwa kuwa mkewe Mama Said alijaribu kumshawishi angalau avumilie kidogo.


“Mganga alimueleza mke wangu kwamba nilikuwa nimechanganyikiwa ndiyo maana ilikuwa ni vigumu kwangu kumuelewa.

“Lakini mimi sikuwa nimechanganyikiwa, nilikuwa naelewa kila kitu na kwa kifupi nilikuwa nimechoka kutokana na mambo yalivyokuwa yanakwenda.


“Mwisho nikashikilia msimamo wangu, kwamba ilikuwa lazima aondoke, kweli ikawa hivyo na nikaamua kuendelea na matibabu mengine.

“Unaona kipindi hiki ninafanya mazoezi mara mbili kwa siku pale kwenye hospitali ya hukuhuku Tabata. Kweli napata nafuu na unaona mambo yanakwenda yanabadilika.

“Natamani sana kupona ili nirudi kufanya kazi yangu ya sanaa, naipenda sana. Utaona hata yule kijana pale (anaelekeza kidole kwa mtoto wa ndugu yake). Nilimuambia nikipona tu, basi nitaanza kumfundisha, naye amekuwa akisubiri.

“Unajua sanaa hii ndiyo imefanya nijulikane kwa watu wengi kila sehemu. Sanaa hii ndiyo imenipandisha ndege na kunipeleka hadi Ulaya na kwingineko.

“Nimesomesha wanangu kupitia kazi hii, wengine wamefika hadi vyuoni ambako sijawahi kufika, lakini ni hiihii sanaa ya uigizaji ndiyo maana naiheshimu sana,” anasema Mzee Small akionyesha kujiamini.

“Achana na kuwasomesha wanangu na kuilea familia kwa jumla, lakini ninaipenda sana. Wakati mwingine ukifanya kitu, lazima ukipende.

“Pia sanaa hii imenikutanisha na watu wengi wakubwa, mfano Rais Kikwete amekuwa rafiki yangu miaka mingi sana tokea akiwa kiongozi wa Umoja wa Vijana wa CCM.

“Baadaye pia alivyokuwa waziri, tulikuwa tukizungumza mambo mengi kuhusiana na sanaa na tulibadilishana sana mawazo. Natamani sana siku moja aje anione.

“Najua kutokana na nafasi yake atakuwa amebanwa na majukumu mengi sana, lakini akiweza kufika hapa siku moja na kuniona, basi nitafurahi sana.

“Sisemi hivyo nalazimisha, hapana ila kama ikitokea hivyo litakuwa ni jambo zuri kwangu kwa kuwa yeye (Kikwete) ni rafiki yangu,” anasema Mzee Small akionyesha kujiamini.

Mzee Small amekuwa akitembea kwa kujivuta kutokana na mwili wake kuishiwa nguvu upande mmoja kutokana na kupooza.

Mara kwa mara amekuwa akieleza namna gharama za matibabu zinavyombana kwa kuwa anashindwa kujiingizia kipato kutokana kulazimika kubaki nyumbani tokea Mei, mwaka jana.

Lakini anasema hajakata tamaa na iko siku atarejea tena huku akisisitiza, kwamba wako watu wamekuwa wakikunwa na kuumwa kwake.

“Wako wanakuja kuniona na wanaumia na kuumwa kwangu, yote hii ni sanaa. Mimi sitaki kuingia kwenye kuwalaumu watu kutokana na kuumwa kwangu.

“Sanaa ni pana, bado naendelea kushukuru hapa nilipo na ninasema nina mke bora ambaye ananiangalia vizuri maana wakati fulani hali yangu ilikuwa mbaya sana.

“Ila bado nashukuru kwamba sanaa ya uigizaji imenilinda, imenipa watu. Tena sijakuambia, wakati fulani nilikuwa na urafiki na marehemu Julius Nyerere kutokana na sanaa hii na wakati ule kumkaribia hakikuwa kitu rahisi,” anasema Mzee Small.

KUMBE Mzee Small aliwahi kuwa rafiki wa marehemu baba wa Taifa? Je, wakati akiwa hai waliwahi kukutana mara ngapi, wapi na walizungumza nini? Fuatilia JUMATATU.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic