Kocha Mkuu wa Simba, Zdravko Logarusic
amewashusha presha mashabiki wa timu hiyo kuhusu makali ya mshambuliaji
Emmanuel Okwi ambaye ametua Yanga kwa kusema kuwa dawa yake ipo.
Logarusic ‘Loga’, amesema anatambua kuwa Okwi raia wa Uganda ni mmoja wa
washambuliaji bora katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, lakini kamwe hawezi
kupata wasiwasi dhidi yake kwa kuwa mabeki wake wanajua kazi wanayotakiwa
kuifanya.
Tambo za Loga zinatokana na Simba
kumsajili beki wa kati, Donald Musoti kutoka Gor Mahia ya Kenya, huku Joseph
Owino na Gilbert Kaze nao wakiwa fiti.
“Nimesikia kuwa kuna kelele nyingi
kuhusu Okwi, namjua huyo mchezaji ni mmoja wa wachezaji wazuri ambao nimewahi
kuwaona ukanda huu, lakini sidhani kama naweza kupata wasiwasi kwa kujiunga
kwake Yanga,” alisema Loga na kuongeza:
“Nimekuwa nikiwafanyia tathmini mabeki
wangu, nadhani wanaweza kutusaidia, tumeanza kazi ya kutengeneza safu makini ya
ulinzi, tukikamilisha hili haraka, nafikiri inaweza kuwa safu nzuri itakayoweza
kupambana na washambuliaji wakali, akiwemo huyo Okwi.”
0 COMMENTS:
Post a Comment