December 2, 2013


Sergio Kun Aguero ndiye anayeongoza kwa kupachika mabao katika Ligi Kuu England inayoendelea kwa kasi kubwa.
Takwimu zote zinazomhusu na zitakazozungumziwa hapa ni zile kabla ya mechi za ligi hiyo dhidi ya Swansea ambayo imepigwa jana Jumapili.


Raia huyo wa Argentina, pamoja na kuwa na mabao 10 ya kufunga, lakini takwimu za kitaalamu zinaonyesha ndiye mchezaji aliyepiga mashuti mengi zaidi, amepiga mashuti 42. Anayemfuatia ni Luis Suarez (41) na Danny Sturridge (40), wote wa Liverpool.

Ukirudi katika kucheza dakika nyingi, Aguero ana dakika 838 kabla ya mechi hiyo ya jana na anaingia moja kwa moja kwa washambuliaji watano waliocheza muda mwingi na kufanya vizuri zaidi.

Huu si msimu wa kwanza, tangu atue England akitokea Atletico Madrid msimu wa 2011-12, ameisaidia timu hiyo kutwaa ubingwa na amekuwa mmoja wa wachezaji nyota kwenye kikosi hicho na kwenye ligi hiyo kwa jumla.

Aguero aliweka rekodi ya kuwa mchezaji ghali zaidi tangu Sheikh Mansour alipoinunua Manchester City. Uhamisho wake ni ghali zaidi kuliko mchezaji yeyote katika kipindi chote cha Mwarabu huyo.
Alihamishwa kutoka Atletico Madrid kwa kitita cha pauni milioni 38, wengine waliomfuatia ni Robinho (pauni 32.5m), Edin Dzeko (pauni 27m), James Milner (pauni 26m) na Carlos Tevez (pauni 25.5m).
Bado rekodi zake akiwa Atletico Madrid zimekuwa bora na za kuvutia, hakuna ubishi tena hadi sasa ni mmoja wa washambuliaji bora na wanaokwenda tofauti na mfumo wa Ulaya kwamba mshambuliaji lazima awe mrefu na mwenye mwili mkubwa. Aguero si mrefu sana kwa kuwa urefu wake ni futi 5 na inchi 8 tu, sawa na washambuliaji wengi wa Ligi Kuu Bara.

Mafanikio yote hayo ya Aguero hayakupatikana kirahisi hata kidogo, inawezekana kabisa akawa changamoto kwa wachezaji wengi wa Bara la Afrika na hasa Tanzania ambako maisha kwa asilimia kubwa ni shida.
Aguero ameishi maisha ya shida, mabaya na makali kuliko Watanzania wengi ambao huenda wanaona wana shida sana au Mwenyezi Mungu amewasahau, lakini aliweza kutoka na kufikia alipo sasa.
Katika kujaribu maisha, amepita kila sehemu hadi kuamua kuwa mwanamuziki, aliimba bila ya mafanikio na mwisho akaamua kuushika mpira akiamini utamtoa, kweli ikawa hivyo.
Miaka 25 iliyopita, mshambuliaji huyo ambaye jina lake halisi ni Sergio Leonel Agüero del Castillo, alizaliwa katika mji mdogo wa Quilmes nchini Argentina na kukulia katika viunga vya mji mkubwa Argentina wa Buinos Aires vinavyojulikana kama Villa Itali.
Maisha yalikuwa ni ya shida sana kwa kuwa baba yake mzazi alikuwa ni dereva taxi ambaye alikuwa na uwezo wa kuingiza pauni 20 (Sh 50,000), fedha ambayo ilikuwa haitoshi hata kidogo.
Baba yake alikuwa akiondoka nyumbani alfajiri na kurejea saa 6 usiku, maisha yalikuwa ya kubahatisha sana na magumu. Malezi ya wazazi ya kawaida hayakuwepo kwa kuwa wazazi walilazimika kupambana kupata maisha.
Ugumu wa maisha ulimlazimisha Aguero kuishi maisha asiyokuwa akiyataka kwa maana ya mafanikio, alikuwa akikimbia kucheza soka na kwenda kwenye muziki kwa kuwa aliamini watu walio upande huo wangekuwa wastaarabu kuliko wale wanaocheza soka.
Eneo la Villa Itali lilikuwa na wakazi wanaofikia 60,000 tu, lakini inaelezwa nusu ya wakazi wake walikuwa wanajihusisha na uuzwaji wa madawa ya kulevya na hasa wale waliokuwa wakishiriki mchezo wa soka.
Wakati fulani, Aguero alipoulizwa kuhusiana na maisha ya Villa Italli, alijibu kwa kuonyesha anasikitika na neno la kwanza lilikuwa hivi: “Soka limeniokoa.”
“Hata rafiki niliokua nao, nimeambiwa asilimia zaidi ya 90, hasa kwa wale waliobahatika kuendelea kuishi, wapo gerezani. Yalikuwa maisha ambayo kila mmoja asingependa kuyakumbuka. Kama nisingeondoka pale kwa sababu ya mpira, kweli hata sielewi sasa ningekuwa ninaishi maisha gani.”
Kauli hiyo ya Aguero ilifuta lawama ya Gazeti la The Sun la Uingereza lililotumia kichwa cha habari cha Slumgold Millionaire, kuonyesha makazi duni aliyokulia, naye akasisitiza wala haoni tatizo lolote kwa kuwa Villa Itali ndiko alikotokea.
Inawezekana ni rahisi kwa wanasoka makinda waliokata tamaa kwa kuwa wanatokea katika familia duni, wazazi wao ni watunza bustani, madereva taxi, bajaj au bodaboda ambao walikuwa wakiamini hawawezi wakafanikiwa.
Aguero aliamua kuepuka biashara ya madawa ya kulevya angalau kwa kiasi fulani na kuingia katika muziki. Mara nyingi jioni alikwenda kujifunza kuimba na kipaji chake kilikubalika.
Lakini kila sehemu kuna wakatisha tamaa na mizengwe haina mipaka, alianza kuona baadhi ya walimu na viongozi wa bendi aliyokuwa akiitumikia wakipendelea watu fulani.
Mwisho, tena kwa hasira, akaamua kurejea kwenye soka, safari hii akiwa amepania kupata mafanikio kwa kuwa alichoka maisha ya mlo mmoja kwa siku huku waliokuwa wakifanya biashara ya madawa ya kulevya wakiishi kwa raha.
Kwa kuwa wengi walikuwa rafiki zake, walijaribu kumshawishi lakini yeye akaapa kwa kuwa muziki ulishindikana, siku moja atatoka kupitia soka.
Muziki aliupenda kiukweli, ni shida tu ndizo zilimlazimu kuimba. Ndiyo maana hata baada ya kupata mafanikio akiwa na timu ya Independiete iliyomkuza kisoka na baadaye Atletico Madrid, aliamua kurejea katika muziki.
Aliimba wimbo maarufu wa El Kun Aguero ulio katika miondoko ya Cumbia, maarufu zaidi katika Bara la Amerika Kusini na hasa nchini Colombia. Wimbo huo alioshirikiana na bendi moja maarufu, umekuwa ukiendelea kupigwa hadi leo.
Tayari amefanya mambo mengi makubwa ikiwa ni pamoja na kuwajengea nyumba, kuwanunulia usafiri na kuwafungulia biashara wazazi wake.

Zaidi amekuwa akitumia jina la Kun alilopewa na babu na bibi yake kutokana na kuvutiwa zaidi ya katuni ya kwenye runinga iliyokuwa maarufu kwa jina la Kunkun.

Aguero ni mkwe wa gwiji la soka Argentina na duniani, Diego Armando Maradona, kwani alimuoa binti yake Giannina ambaye alizaa naye mtoto Benjamin aliyezaliwa Februari 19, 2009. Hata hivyo Januari 2013, Aguero na binti huyo mdogo kuliko wote wa Maradona, walitengana.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic