Kocha Mkuu wa Simba, Zdravok Logarusic,
amekutana na mchezaji wa kwanza wa Simba, kipa Yaw Berko, lakini akafanya
kituko kwa kukagua tumbo lake hadharani.
Logarusic, raia wa Croatia, alifanya jambo
hilo jana na kushuhudiwa na SALEHJEMBE, wakati akiwa na viongozi wa
timu hiyo, kaimu makamu mwenyekiti, Swed Nkwabi na mjumbe wa kamati ya utendaji
Said Pamba, wakati wakimuonyesha kocha huyo Uwanja wa Kinesi unaotumiwa na
kikosi hicho kwa mazoezi.
Wakati Logarusic, maarufu kwa jina la
Loga, akiwa ndani ya Uwanja wa Kinesi, alikutana na Berko ambaye naye ni kipa
mpya wa Simba. Mara baada ya kumaliza kumsalimia, alifunua tumbo lake bila ruhusa
ya kipa huyo akikagua jinsi alivyo fiti.
Loga awali alikuwa akizungumza na Nkwabi
juu ya mipango ya kuanza mazoezi ya kikosi hicho ambapo wakati wakijadiliana
juu ya kuwapelekea nyota hao gym, kocha huyo alisema hataki hilo lifanyike kwa sasa,
ndipo alipoamua kufunua fulana ya Berko na kuangalia jinsi tumbo lake lilivyo.
Mara baada ya kumaliza kuliangalia tumbo
hilo, akitumia sekunde mbili, Loga alimfunika na kusema siku zote anajua kuwa
wachezaji wa Kiafrika wako sawa kimazoezi na kumwambia Nkwabi hakuna ulazima wa
kuandaa mazoezi hayo.
“Unaona, nilikwambia najua kuwa
wachezaji wa Kiafrika wako sawa, angalia jinsi tumbo la mazoezi lilivyo,
nafikiri hiyo ratiba ya gym tuifute kwa sasa, tutaifanya huko mbele, kwa sasa
nataka hayo tuliyoongea tukayafanye kwanza,” alisema Loga huku akiwaacha katika
mshangao watu wote walioshuhudia tukio hilo.
0 COMMENTS:
Post a Comment