December 9, 2013





Na Saleh Ally
AFRIKA Mashariki na Kati ilishajitoa kabisa katika mbio za kucheza Kombe la Dunia kwa vile kila inapofanyika michuano hiyo, nchi zinazoshiriki zinatokea Afrika Magharibi na Kaskazini.
Kanda hizo mbili za Bara la Afrika ndizo zimekuwa zikitoa washiriki kuiwakilisha Afrika, angalia hata zilipoongezwa na kufikia timu tano, hakuna timu ya Afrika Mashariki angalau imepata nafasi ya kutia mguu.
 
Mwaka 2010 wakati Kombe la Dunia lilipofanyika kwa mara ya kwanza barani Afrika, harufu kwamba angalau nchi za Afrika Mashariki zingeshiriki kwa kuwa ulikuwa wakati mwafaka, mambo yakawa yaleyale.

Timu kutoka Afrika Magharibi na Kaskazini ndizo ziliiwakilisha Afrika katika michuano hiyo iliyomalizika kwa Hispania kubeba kombe kwa kuifunga Uholanzi bao 1-0 kutokana na shuti la Iniesta.
Nchi zilizoiwakilisha Afrika zilikuwa ni Ghana, Afrika Kusini, Nigeria, Cameroon, Ivory Coast na Algeria ambapo Afrika Kusini iliingia kwa kuwa ilikuwa mwenyeji wa fainali hizo.

 Timu tano ndiyo hizohizo zipo tena mwakani nchini Brazil.

Kuwakilishwa na timu zilezile katika kipindi cha miaka minane, kunaonyesha hakuna mabadiliko yoyote ya kisoka kwa Afrika Mashariki.

Achana na Afrika Mashariki, kikubwa cha kuangalia ni kwamba katika timu hizo za Afrika ni Ghana pekee ndiyo ilifikia robo fainali mwaka 2010 na nusura ivuke hadi nusu fainali na kuweka rekodi, lakini mkwaju wa penalti wa Gyan Asamoah ukagonga mtambaa-panya na kutoka.
Maana yake hakuna timu ya Afrika imewahi kuvuka robo fainali na kama ni timu zilezile za 2010, ipi ina nafasi ya kupita na kuweka rekodi mpya kwa kuwa inaonekana zimebanwa?

Cameroon iko kundi A na Croatia, Mexico na Brazil na inaonekana hapa kazi ya ziada inabidi ifanyike ili kuvuka hatua hiyo maana Brazil na Mexico ndizo zinapewa nafasi zaidi wakati Cameroon haina kiwango cha juu sana.

Kundi C kuna Ivory Coast ambayo itapambana na timu za mabara matatu, Ulaya, Amerika Kusini na Asia ili ivuke. Bado hakuna timu ya mzaha lakini angalau inapewa nafasi ya kuzipita Japan, Ugiriki na Colombia na kusonga mbele.
Nigeria kama itajitutumua, inaweza kusonga kutoka kundi F ambako kuna Argentina, Bosnia & Herzegovina na Iran. Hata hivyo bado Argentina inapewa nafasi ya kwanza katika kundi hilo.

Ghana iliyokuwa inapewa nafasi ya kufanya vyema, iko kwenye kundi G ambalo ni gumu zaidi kwa timu za Afrika, maana ina Ujerumani, Ureno ya Cristano Ronaldo na Marekani, maarufu kama wabishi.

Lakini bado huenda kukawa na matumaini kwa kuwa inaonekana kuwa na kikosi bora ukilinganisha na timu zote, ingawa ugumu wa kundi ni tatizo.
Timu ya mwisho ya Afrika ni Algeria ambayo mwaka 2010 pia ilitoka mapema, safari hii iko kundi H, ambalo lina timu za Ubelgiji, Urusi, Korea Kusini na linaonekana si gumu sana, hivyo inatakiwa kubadili gia na kuhakikisha inafuzu.

Ukiangalia mpangilio wa makundi na nafasi ya timu za Afrika, inaonekana kila mmoja anasubiri miujiza kwa kuwa hakuna hata timu moja ya bara hilo inayopewa angalau kumaliza nafasi ya kwanza katika kundi.
Timu ya Afrika inayopewa nafasi ya kusonga mbele kutoka katika hatua ya makundi ni ile inayopewa nafasi ya pili katika kundi.
Hii inaonyesha ni kiasi gani ugumu wa timu za bara hili kufika mbali katika michuano hiyo mikubwa zaidi ya soka duniani ingawa katika mchezo wa soka, mambo yanawezekana kwenda tofauti na yalivyokuwa yanatarajiwa.

Inawezekana Afrika ikaweka rekodi mpya ya kucheza nusu fainali angalau timu tatu zitavuka kutoka katika hatua ya makundi na kupambana vilivyo kuifukuzia rekodi hiyo. 

Kundi A
Brazil, Croatia, Mexico na Cameroon
Kundi C
Colombia, Ugiriki, Japan na Ivory Coast
Kundi F
Argentina, Bosnia & Herzegovina, Iran na Nigeria
Kundi G
Ujerumani, Ureno, Marekani na Ghana
Kundi H
Ubelgiji, Urusi, Korea Kusini na Algeria
 



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic