December 25, 2013





 Na Saleh Ally
JUZI Jumatatu Mzee Small alizungumzia kuhusiana na mapenzi yake na mchezo wa soka na namna alivyo na mapenzi makubwa na Dar Young African maarufu kama Yanga.


Lakini akaeleza namna anavyovutiwa na uwezo wa mshambuliaji wa zamani wa Simba, Abdallah Kibadeni ambaye ni rafiki yake.

Pamoja na hivyo, Mzee Small ambaye sasa ni mgonjwa, anasumbuliwa na ugonjwa wa kupooza upande mmoja aliahidi kuelezea alivyowahi kukutana na hayati Mwalimu Julius Nyerere na pia rais wa awamu ya pili, Ali Hassan Mwinyi. Endelea kumfuatilia.

UKIACHANA na soka, Mzee Small ambaye ni kati ya wasanii wacheshi nchini, anasema alikuwa akikutana na viongozi wengi wakubwa wa kitaifa kutokana na sanaa hiyo.

Mmoja wa aliokuwa akikutana nao mara kwa mara na wakati mwingine akawa rafiki yake alikuwa ni Mwalimu Nyerere.

Baba wa Taifa alikuwa akifuatilia michezo ya Mzee Small na mara kadhaa aliwahi kumueleza anavyovutiwa na umahiri wake lakini hakuacha kumshauri.

“Nilikutana na Nyerere mara kadhaa, si kwamba ilikuwa kwa mwaliko maalum lakini alipokwenda kutembelea mabanda kwenye maonyesha ya Sabasaba alikuwa akiniita.

“Tunakaa hapa na hapa, halafu tunaanza kuzungumza mambo mengi sana kuhusiana na sanaa ya uigizaji na alikuwa anajua sana.

“Nilikuwa nasikia faraja sana, unajua unakutana na kiongozi mkubwa kama yule anakuita jina lako, raha sana. Lakini anakwenda zaidi ya hapo na kukueleza kwamba alikuwa anafuatilia kazi yako.

“Nyerere alikuwa akinieleza kwamba anafuatilia sana michezo yangu, tena alionyesha ni mtu anayeijua sanaa kwa kuwa alikuwa akinikosoa na kunieleza namna mambo yanavyokwenda au anapoamini nimekosea,” anasema Mzee Small.

Pamoja na Nyerere, Mzee Small anasema pia amekuwa rafiki wa Rais Mwinyi kutokana na sanaa yake.

“Mwinyi pia ni mtu ambaye alikuwa akifuatilia kazi zangu, yeye tumekutana mara nyingi zaidi kikazi. Hata sasa sema ndiyo hivyo kazi na mimi kuumwa zinatutenganisha.

“Lakini kipindi cha uongozi wake nakumbuka nilipata mafanikio makubwa sana. Kweli ni kati ya watu walionivutia sana alipokuwa rais,” anasema Mzee Small.

Kuhusiana na heshima ya michezo ya uigizaji, Mzee Small anasema mambo yamekuwa tofauti kila sanaa hiyo inavyozidi kupata wigo mkubwa.

“Kila inavyozidi kuendelea na kuwa kubwa, wasanii wengi wanakuwa hawapendani na ushirikiano si kama ule wakati wa enzi zetu.

“Kipindi hiki kila msanii anajijali mwenyewe zaidi, hali hiyo si nzuri kwa sanaa yenyewe. Kila kitu kinatakiwa kufanyika kwa ushirikiano sana hata kama kila mmoja atakuwa anafanya juhudi zake binafsi,” anasema Mzee Small.

Kuhusiana na kuendelea na kazi yake, Mzee Small anasema mara tu atakapopata nafuu, basi atarejea tena na kuendelea na kutengeneza michezo.

“Sasa kama unavyoona siwezi kitu, lakini natamani sana lakini uwezo wa kufanya hivyo ndiyo sina. Kama nikipata nafuu na kupona basi nitarejea tena na kuendelea na kazi yangu,” anasema Mzee Small.

Kawaida analazimika kufanya mazoezi mara mbili kwa siku ili kuimarisha viungo vyake hasa ule upande uliopooza na kwa kiasi kikubwa mazoezi hayo yanamsaidia kupata nafuu.

 MWISHO YA SIMULIZI ZA MAISHA YA MZEE SMALL KWA UFUPI. KWA WALE WENYE UWEZO WA KUMSAIDIA MATIBABU KWA KUWA SASA HANA KIPATO, WANAWEZA KUFANYA HIVYO.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic