December 27, 2013





Na Saleh Ally
MCHEZAJI nyota wa zamani wa Manchester United, Bryan Robson amewafungua macho wapenda soka kwamba wanaweza wakafanya mambo mengi makubwa wakiwa hapa nyumbani na hakuna haja ya kutegemea msaada.


Robson ambaye pia aliwahi kuwa nahodha wa timu ya taifa ya England amepanda Mlima Kilimanjaro pamoja na mchezaji mwingine wa zamani, Kevin Moran ambaye pia alikipiga Man United, enzi zake.



Robson mwenye miaka 56, amepanda mlima huo na kufanikisha kuchangisha pauni 115,000 (Sh milioni 287.5) kwa ajili ya kuwachangia wanaosumbuliwa na kansa ya koo. Staa huyo alifanya tukio hilo miezi michache baada ya kupona kansa ya koo.

Safari yake ya siku tano kupanda mlima huo inavutia na katika mahojiano na Gazeti la Dailymail, Robson aliyewahi kufanya mahojiano ya ana kwa ana na Championi anaeleza namna walivyoanza baada ya kuwasili nchini hadi walivyofika kileleni.


Kilimanjaro ndiyo mlima mrefu kuliko yote barani Afrika, wakati fulani Wakenya walikuwa wakiutumia kujifaidisha huku wakiwadanganya watu kwamba uko nchini mwao.

Inaonekana sasa Watanzania wameamka na kulizuia hilo ndiyo maana utaona nyota wengi duniani wamekuwa wakija nchini na kuupanda.

Lakini wakati Robson na wenzake wakipanda na kufanikiwa kuchangisha mamilioni ya fedha kwa ajili ya kusaidia wenye matatizo ya kansa ya koo, wanamichezo wa Tanzania bado wamelala usingizi.



Ingawa imekuwa kipindi kidogo tokea afanye hivyo lakini nyota huyo wa Manchester United hata kama atakuwa ametumiwa na kampuni fulani pamoja na mwenzake Moran wameona kupitia Mlima Kilimanjaro wanaweza kufanya kitu fulani kusaidia.

Kweli wameingiza mamilioni ya fedha kusaidia huku kampuni kibao na idara nyingi zikiwemo taasisi na mashirikisho ya michezo yakiwa hayajui umuhimu wa mlima huo.

Michezo ina nguvu ya kusaidia na kuongoza mambo mengi kwenye jamii lakini wanaoiongoza hawalijui hilo ndiyo maana wamelala.

Inawezekana pia kwa kuwa kumekuwa na mashindano ya riadha, basi huenda wengi wanaona mchezo unaoweza kuhusishwa na mlima huo ni riadha pekee, kitu ambacho si sahihi.

Kwa wale wanaofuatilia Ligi Kuu England, wakiwa makini wataona lile tangazo la Adidas linalomhusisha mshambuliaji nyota wa Barcelona, Lionel Messi akiwa kwenye kilele cha mlima huo ulio Kaskazini mwa nchi yetu.

Mlima Kilimanjaro ingawa ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, Watanzania hata hawajui cha kuufanyia na badala yake wajanja kutoka nje kama ilivyokuwa kwa Wakenya, wamekuwa wakiutumia kujifaidisha wao binafsi na watu wa nchi zao.

Wakati wa kutoa tongotongo umefika, Watanzania ambao wanaweza kufanya jambo na sasa kupitia michezo basi wanaweza kufanya hivyo ili kuisaidia jamii ya nchi yetu.

Robson amechangisha kwa ajili ya wanaosumbuliwa na kansa ya koo, lakini kuna wengi wanaweza kusaidia, hivyo tujifunze ingawa limekuja kufanyika kwetu basi si vibaya kujua njia za kupita na mlima huo utumike kupitia michezo.

Kwa kuitumia michezo, kupitia Mlima Kilimanjaro kunaweza kuwa na misaada mingi na wanamichezo wawe tayari kujitolea kwa ajili ya jamii yao, si kila kitu lazima faida iwe kwao.

Siku tano za Robson kufika kileleni anaeleza mambo mengi ikiwa ni pamoja na kuteseka na baridi kali, kulala kwenye mahema lakini mwisho amefanikiwa kufikia malengo yake. Wanamichezo wa Tanzania wenye nia na upendo na nchi yetu, wanaliweza hili.

Lakini lazima wakubali kuanza na nia, waende kwenye ubunifu lakini muhimu ni kutaka kutekeleza jambo na mwisho, kuumia kwa ajili ya watu wako, yaani jamii iliyokuzunguka, jamani Mlima Kilimanjaro ni neema.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic