January 29, 2014





Kitendo cha Kocha Mkuu wa Simba, Zdravko Logarusic kumwingiza na kumtoa mshambuliaji wake Betram Mwombeki ndani ya dakika chache, kimewakera watu wengi na Mwenyekiti wa Chama cha Wachezaji wa Soka Tanzania (Sputanza), Mussa Kisoki amefunguka na kusema haikuwa sahihi.


 Kisoki ambaye ni bosi wa wachezaji wote wa Ligi Kuu Bara, amesema yeye binafsi ameshangazwa na kitu hicho na kushauri uongozi wa Simba ulifanyie kazi suala hilo na ikiwezekana umpe onyo Logarusic.
“Sitaki kuingilia uamuzi wa kocha, wala sitaki kusema hajui kazi yake. Lakini alichokifanya kwa Mwombeki si sahihi na kinaweza kummaliza mchezaji. Kocha lazima aangalie kwamba kama kweli mchezaji anataka kumtumia siku nyingine, basi asimfanyie vitendo vinavyoweza kumuathiri.
“Nilihesabu baada ya Mwombeki kuingia alicheza mipira mitano, alikosea miwili, mitatu akatoa pasi ukiwemo mmoja ambao alimpa pasi (Ramadhani Singano) Messi na angeweza kufunga lakini akashindwa. Sasa hilo ni tatizo la kumtoa mchezaji! Hata kama mimi si kocha lakini si sahihi.
“Inawezekana watu wakalizungumza hili suala kishabiki, lakini haya ni mawazo yangu na kwa kuwa ni mmoja kati ya wanaosimamia haki za wachezaji, naomba niseme wazi kuwa halikunifurahisha hata kidogo.
“Mpira ni mchezo wa makosa, kama mtu akikosea mara mbili anatolewa, basi Kiemba, Chanongo wote wangetolewa. Ingawa bado nasisitiza hiyo si sahihi,” alisema Kisoki ambaye pia ni mdau mkubwa wa soka.
“Ingekuwa Ulaya, vyama vyao vina sauti tofauti na hapa. Maana hata kuna mashabiki wanaona mchezaji ana makosa, lakini si sahihi, hata kupasha mwili inahitaji muda na lazima ujue Mwombeki ana umbo kubwa.
“Makosa kila mtu anayo, angalia hata kocha alikosea. Mchezaji anapiga penalti yeye anaangalia majukwaa, hilo ni kosa, lakini ndiyo kuvumiliana maana hata kama ni mchezo kuna ubinadamu.”

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic