January 31, 2014


Kiungo mshambuliaji wa Yanga, Emmanuel Okwi amesema hataki kuzisikia wala kuzungumzia habari za Simba na Etoile du Sahel kwa kuwa hana mpango wa kurejea alikotoka.


Okwi ametoa tamko hilo ikiwa ni siku chache mara baada ya kupewa ‘kifungo’ cha muda, huku uongozi wa Yanga ukisisitiza kuwa utamtumia mchezaji huyo katika mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Komorozine ya Comoro inayotarajiwa kuchezwa wiki ijayo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Okwi ambaye ni raia wa Uganda, alisema yeye ni mchezaji wa Yanga na mapenzi yake yapo klabuni hapo, ndiyo maana hataki kuzungumzia suala la mgogoro wa usajili wake, kwa kuwa hana mpango wa kurudi alipotoka.

“Najua baada ya muda TFF itaniruhusu kucheza, sitaki kurudi nilipotoka kwa kulizungumzia suala la Etoile (du Sahel), pia sitaki kuizungumzia Simba kwa kuwa siyo klabu yangu.

“Naipenda Yanga na mapenzi yangu yote yapo hapa, ndiyo maana leo hii nipo klabuni nikiwa mchezaji wao. Nilikuwa tayari kuanza kuichezea Yanga katika ligi hii (mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Bara) na Ligi ya Mabingwa Afrika,” alisema Okwi.

Akizungumzia juu ya sakata la kuzuiwa kwa Okwi, Katibu Mkuu wa Yanga, Beno Njovu ameliambia gazeti hili kuwa, watamtumia Okwi katika mechi dhidi ya Komorozine kwa kuwa wamepata ruhusa ya kumtumia kutoka Shirikisho la Soka la Afrika (Caf).

“Caf wametupa ruhusa ya kumtumia, sisi tunawaamini wao, kwani inavyoonekana TFF ndiyo hawamtaki (Okwi) kwenye ligi yao, sisi tunajua Caf ni wakubwa kuliko TFF, hivyo tutamtumia siku hiyo.

“TFF hawakutupa muda wa kujitetea walipomsimamisha Okwi, tulianza kuona taarifa hizo kwenye vyombo vya habari, baadaye ndiyo wakatupa barua, kwa hiyo Okwi tutaanza kumtumia rasmi kwenye mechi dhidi ya Komorozine,” alisisitiza Beno.

Wakati huohuo, Katibu Mkuu wa Simba, Ezekiel Kamwaga amesema anaamini tayari Fifa watakuwa wameshateua jaji wa kusikiliza kesi ya mchezaji huyo.


“Hatuna shida ya kuwaandikia barua ya kuwauliza Fifa kile kinachoendelea, tarehe ya awali iliyowekwa ni Januari 27, mwaka huu waliyotakiwa kuwa wametulipa fedha za usajili lakini hawajafanya hivyo,” alisema Kamwaga.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic