January 31, 2014



Na Saleh Ally
KILA kocha ana mfumo wake na anapopata timu ya kuifundisha, daima imekuwa hivi, atafanya kitu ambacho lazima kitaonyesha kuna tofauti na kocha aliyepita.


Mfano mzuri ni makocha wawili wapya, Zdravko Logarusic wa Simba na Hans van Der Pluijm wa Yanga, ambao baada ya kuchukua timu, waliingiza falsafa zao na kubadilisha mambo.

Logarusic aliyekabidhiwa timu kutoka kwa Abdallah Kibadeni, aliona kuna ‘watoto’ wengi, kuna tatizo kwenye safu ya ulinzi na hadi leo anasisitiza safu yake ya ushambuliaji haijakaa vizuri. Ndiyo maana akamsajili kipa Ivo Mapunda na beki Donald Musoti.

Van Der Pluijm naye tayari amecheza mechi mbili za kirafiki, mbili za mashindano akiwa na rekodi ya sare tatu na ushindi mmoja. Lakini pia amefanya mabadiliko na hasa katika mechi za Ligi Kuu Bara.

Juzi mara baada ya mechi kati ya Yanga dhidi ya Coastal Union kwisha, van Der Pluijm aliwaambia waandishi wa habari mambo mawili, kwamba pamoja na mchezo kuwa mgumu lakini kikosi chake kilishindwa kufanya vizuri kutokana na uwanja mbovu na upepo mkali uwanjani hapo.

Huenda sababu hizo zimeonyesha kuwashangaza wengi ingawa kweli kocha huyo ana haki ya kueleza kulingana na mwenyewe alivyoyaona mambo katika mechi hiyo.

Mazungumzo yake yanalenga kujitetea kitu ambacho makocha wengi hufanya, lakini kidogo inachanganya kwa kuwa siku chache tu zilizopita baada ya mechi dhidi ya Ashanti, van Der Pluijm alisema hawakucheza vizuri.

Mholanzi huyo alikiri kikosi chake hakikucheza vizuri katika mechi dhidi ya Ashanti na akatoa sababu ya hali ya hewa, kwamba walichelewa kuwasili nchini, hilo likachangia wao kutokuwa na pumzi ya kutosha.

Kukubali timu haikucheza vizuri na kuelezea kuhusiana na suala la hali ya hewa ni kitu kilichokuwa ‘kinaingia akilini’, lakini hili la upepo na uwanja, inawezekana van Der Pluijm inabidi afanye tathmini mara mbili.

Kwa kuwa kama ni upepo, hiyo ni kawaida kwenye uwanja huo na Yanga imecheza mara nyingi hapo. Lakini kuhusu uwanja, hapa ni tatizo kwa kuwa si sahihi kusema Uwanja wa Mkwakwani ni mbaya, sehemu yake ya kuchezea ni dhoofu kuliko Uwanja wa Bora au Loyola ambako wamekuwa wakifanyia mazoezi.

Labda ugeni pia wa Mholanzi huyo, bado hajui hali halisi ya sehemu wanazofanyia mazoezi, lakini ukweli ulio wazi ni kwamba hajapata kikosi sahihi na mabadiliko makubwa katika mechi mbili za ligi alizocheza yanaonyesha.

Suala la kwamba hajapata kikosi anachotaka, linaweza kukubalika hasa kwa kuwa ndiyo amejiunga na timu hiyo hivi karibuni.

Utaona katika mechi ya kwanza dhidi ya Ashanti, van Der Pluijm alifanya mabadiliko ambayo hayakutarajiwa sana. Langoni alianza na Deogratius Munishi ‘Dida’ badala ya Ally Mustapha ‘Barthez’ au Juma Kaseja, kama ilivyotegemewa na wengi.

Beki wa kulia akamuanzisha Juma Abdul na kumchezesha Mbuyu Twite namba nne, lakini akampa nafasi Said Bahanuzi kucheza namba kumi huku akimtoa David Luhende kucheza beki hadi kiungo wa pembeni, kushoto.

Siku chache baadaye kwenye mechi ya Coastal, kikosi cha kwanza akakifanyia mabadiliko makubwa matano, kumtoa Juma Abdul na nafasi yake ikachukuliwa na Twite, halafu akamuingiza Nadir Haroub ‘Cannavaro’ ambaye hakuwemo katika mechi ya Ashanti.

Kulia ambako alicheza Ngassa dhidi ya Ashanti, akampanga Simon Msuva ambaye hakuanza mechi ya Ashanti, Ngassa amkabadilisha na kumchezesha namba 10 ambayo alianza Bahanuzi katika mechi ya kwanza.

Mabadiliko hayo makubwa anayofanya van Der Pluijm, yanaonyesha bado anasaka kikosi na huenda inaweza kuwa sababu ya msingi zaidi kuliko upepo au hali ya uwanja.

Hata iwe vipi, lazima van Der Pluijm ajue kucheza kulingana na mazingira ya sehemu halisi kwa kuwa kazi yake ni kuongoza kikosi chake kupata ushindi na si vinginevyo.

Kweli, kuna tatizo la viwanja vya kuchezea, bado ni duni, hii ni Afrika ingawa lazima wahusika wapambane nalo. Hivyo, van Der Pluijm anatakiwa kulitambua mapema lakini si kuhusisha upepo kama kigezo cha kucheza vibaya.

Inawezekana mara moja likakubalika, lakini haliwezi kuwa utatuzi wa michezo mingine zaidi ya yeye kuhakikisha anakuwa na mbinu mbadala kulingana na mazingira.


Kikosi Vs Ashanti:
Dida, Juma Abdul, Oscar Joshua, Mbuyu Twite, Kelvin Yondani, Frank Domayo, Mrisho Ngassa, Haruna Niyonzima, Didier Kavumbagu, Said Bahanuzi na David Luhende

Kikosi Vs Coastal:
Dida, Mbuyu Twite, Oscar Joshua, Nadir Haroub, Kelvin Yondani, Frank Domayo, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Didier Kavumbagu, Mrisho Ngassa na David Luhende.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic