January 20, 2014


MASHABIKI wengi wa mpira hasa wale watu wenye tabia za kinazi au kikoma-ndoo, wamekuwa hawataki kuambiwa ukweli hata kidogo.


Ikitokea wameelezwa ukweli, wengi wao wamekuwa wakisingizia kitu kimoja tu, “umetumiwa”. Yaani kama kuna kiongozi, mwanachama au shabiki wa klabu fulani na hasa Yanga na Simba anaona umemueleza ukweli, utasikia anatumia lugha hiyo.

Neno ametumika limekuwa la kawaida kabisa kwa wale wanaoshindwa kujibu hoja za msingi kwa kuwa wanashindwa pa kusimamia, hivyo wanalazimisha kumaliza mambo mapema ili wasijibu wanachotakiwa kufanya hivyo.

Katika mkutano wa wanachama wa Yanga uliofanyika jana kwenye Ukumbi wa PTA jijini Dar es Salaam, kumejitokeza mambo kadhaa ambayo hakika yanaweza kuwa somo kwa wapenda soka nchini.
Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Mehbub Manji, alizungumza masuala kadhaa yanayohusiana na klabu hiyo lakini kubwa lililowagusa na kuwakosha wengi ni kuhusiana na suala la Katibu wa Wazee wa Yanga, Ibrahim Akilimali.

Akilimali anayejulikana na wapenda soka kama Abramovic, amekuwa mtu anayezungumza sana kuhusiana na klabu hiyo, wakati mwingine kuitetea au hata kuvuruga mambo.

Wiki chache zilizopita katika Hoja Yangu ya kila Ijumaa, nilizungumzia namna Mzee Akilimali alivyozungumza kuhusiana na kipa Juma Kaseja akimsakama kwamba alichangia kuifungisha Yanga katika mechi waliyofungwa 3-1 na Simba, na wao kama wazee waliutaka uongozi kumsajili Ivo Mapunda na si yeye.
Nilieleza kuhusiana na kila mmoja kumuachia nafasi mwenzake, kwanza haiingii akilini Mzee Akilimali kuzungumzia masuala ya kiufundi au kuwashambulia wachezaji wake hadharani, kitu ambacho si sahihi.
Lakini jana, Manji amefunguka kwa staili yake ambayo naweza kusema ile tabia ya kuamini ukiwa mtu mzima basi hata kama ukikosea haupaswi kuelezwa, si sahihi.

Manji amemueleza Mzee Akilimali namna ambavyo amekuwa akiwakwaza, kama kiongozi wa klabu akamueleza wanavyomheshimu, akasimulia namna mzee huyo alivyompokea wakati anaingia Yanga, lakini mwisho akasisitiza suala la kuheshimu katiba.

Kauli ya Manji hauwezi tena kuiita majungu, haikuwa na kunong’onezana wala kuitana pembeni, badala yake kila kitu kimetokea mbele ya wanachama wote wa Yanga na ninaweza kusema ilikuwa ni kwa njia njema ambayo huwezi kusema imemdhalilisha Mzee Akilimali.

Kama ni nidhamu haikuvunjwa na msisitizo wa Manji amesema anamheshimu sana, lakini akasisitiza lazima katiba ifuatwe ambacho ni kitu cha msingi zaidi. Baada ya hapo, Manji na Mzee Akilimali walipeana mikono na kukumbatiana.

Kilichonifurahisha zaidi si wao kupeana mikono na kukumbatiana, badala yake ni namna Mzee Akilimali alivyoamua kukaa kimya, kweli ameonyesha ni mzee hasa ambaye anajua nini cha kufanya.
Hakukurupuka, badala yake alikaa kimya. Naweza kusema ukimya wake umeonyesha ameelewa alichoelezwa na yuko tayari kubadilika, pia ninaamini alichoelezwa ameamini ni kwa manufaa ya klabu yao.
Kama Mzee Akilimali amekubali kujifunza, suala la msingi ni kwamba kila mmoja ana nafasi ya kujifunza na kukubali kwamba akikosea, akaelezwa basi ajirekebishe na suala la “anatumiwa” au vinginevyo lisipewe nafasi.
Kama Mzee Akilimali angekurupuka na kuamini Manji anamdhalilisha, au “anatumiwa” kama ambavyo wamekuwa wakisema wengi wasiopima mambo, huenda asingeelewa somo alilopewa. Lakini sasa atakuwa amepiga hatua moja mbele.
Ujasiri wa Manji pia kumkosoa Mzee Akilimali ni jambo la kujifunza, tabia za woga wa viongozi wengi kuonyesha hawajiamini na kuhofia kuonekana wabaya imechangia klabu kongwe kuendelea kuyumba kwa kuwa uamuzi wa mambo, haufanyiki wakati mwafaka.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic