February 11, 2014



Na Saleh Ally
MAKOCHA wageni waliojiunga na Simba na Yanga kwa ajili ya mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Bara kuanza sasa wanaweza wakawa wameanza kupata picha kamili ya kazi yao.


Yanga na Simba, kila moja inataka kuchukua ubingwa wa Ligi Kuu Bara, hakuna ubishi kama itashindikana kila moja inaona afadhali kubaki katika nafasi ya pili.

Nafasi ya pili inatoa nafasi kwa timu hizo kushiriki Kombe la Shirikisho ambayo pia ipo chini ya Shirikisho la Soka Afrika (Caf) kama ilivyo kwa Ligi ya Mabingwa Afrika.
Lakini nafasi hizo mbili zimegeuka na kuwa lulu, tayari timu nne zimeonyesha kuwa na nguvu sana katika kuziwania, Yanga, Azam FC, Simba na Mbeya City. Si rahisi kwa sasa kusema moja kati ya hizo tayari imefanikiwa.

Lakini bado kuna washindani ambao hawapaswi kudharauliwa sana, kwamba hata kama wasipopata  kati ya nafasi hizo, wanaweza kuwa tatizo kwa wanaowania. Mfano Coastal Union na Mtibwa Sugar, viko vizuri.

Kocha Zradvko Logarusic wa Simba na Hans van Der Pluijm wa Yanga ambao wote wameanza kazi kamili kwenye mzunguko wa pili, kila mmoja sasa anaweza kuwa ameona njia sahihi anayotakiwa kupita na huenda ni wakati mwafaka wa kuamini ligi hiyo haitabiriki.
Inawezekana makocha wote waliichukulia ligi hiyo kama ‘poa’ fulani hivi. Lakini mechi zao tatu za mwanzo, tayari wameona tofauti kubwa ambayo ndiyo picha halisi ya ligi hiyo kwamba si ya mzaha.
Wote wawili wamewahi kufanya kazi nchini Ghana, lakini Logarusic akajikita Kenya akiwa na Gor Mahia, bado wana kila sababu ya kujifunza kwenye Ligi Kuu Bara, kwamba si lelemama.

Wote wawili katika mechi zao tatu za mwanzo walipoteza pointi mbili na kuchanga saba. Maana yake Yanga na Simba, zilishinda mechi mbili na kutoa sare moja.
Yanga ilianza na ushindi wa bao 2-1 dhidi ya Ashanti United, ikatoka sare ya bila kufungana na Coastal Union na mechi ya tatu ikaifunga Mbeya City bao 1-0 ikiwa ni mara ya kwanza kwa timu hiyo ya Mbeya kupoteza mchezo.

Simba ilianza na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Rhino, ikaendeleza ushindi kwa kuifunga Oljoro mabao 4-0 halafu ikapunguzwa kasi ya bao 1-1 dhidi ya Mtibwa Sugar.  

Kila timu imeacha pointi mbili ndani ya mechi tatu, kwani zingeshinda zote kila moja ingepata pointi tisa, lakini kila sare imedondosha pointi mbili.

Kingine kinachovutia, makocha hao wawili wameonyesha kuteswa na mechi za ugenini, kwani Yanga ilipotoka kwa mara ya kwanza ikakutana na sare ‘tasa’ dhidi ya Coastal Union mjini Tanga na Simba ikaenda mwendo huo kwa sare ya 1-1 dhidi ya Mtibwa Sugar mjini Morogoro.

Simba imecheza mechi ya nne kabla ya Yanga, tayari Logarusic ameonja ladha ya kipigo katika Ligi Kuu Bara baada ya kuchapwa na Mgambo JKT kwa bao 1-0 kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga. Yanga bado hawajacheza mechi ya nne, inafuatia Februari 19 dhidi ya Azam FC, itakuwa big match.

Si Logarusic wala van Der Pluijm ambaye amewahi kushinda mechi ya nje ya Dar es Salaam ingawa mmoja amecheza mbili na mwingine moja.
Pamoja na uzoefu wa makocha hao kwa kuwa wamewahi kufanya kazi ya ukocha katika nchi zaidi ya mbili, lakini kazi ya soka ya Tanzania wamegundua si rahisi na kuna timu ambazo hazijatumia gharama kubwa kwenye usajili, lakini zina uwezo mkubwa.

Mfano mzuri mabadiliko ya Mgambo JKT ambayo mzunguko wa kwanza ilipigwa na Simba mabao 6-0, lakini mzunguko wa pili imejibu na kubeba pointi zote tatu kwa kuishinda Simba bao 1-0.

Wakati makocha hao wawili wanalazimika kuzungumza kwa rekodi, ugumu unazidi kuongezeka kuwania ubingwa au hata nafasi ya pili kwa kuwa Mbeya City ambayo ilipoteza kwa mara ya kwanza dhidi ya Yanga, imeamka tena na kuichapa Mtibwa Sugar kwa mabao 2-1.

Mbio zinaendelea, Azam FC pia ni washindani wakubwa, Mbeya City bado ina pumzi ya kutosha. Maana yake, hakuna kulala kwa van Der Pluijm na Logarusic na kwao ligi ni sawa na kama ndiyo imeanza vile kwa kuwa kwa kipindi hiki, rekodi ndiyo zinazozungumza.
REKODI:
Logarusic
NYUMBANI
Cheza 2 Shinda 2
UGENINI
Cheza 2, sare 1, poteza 1

Van Der Pluijm
NYUMBANI
Cheza 2 Shinda 2
UGENINI
Cheza 1, sare 1


 SOURCE: CHAMPIONI 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic