February 17, 2014



Na Saleh Ally

WIKI iliyopita kulikuwa na mechi zaidi ya tano za Ligi Kuu England na mashabiki wa soka duniani kote walivutiwa zaidi na mechi kati ya Arsenal na Manchester United inayoongozwa na David ‘Daudi’ Moyes.

Mechi hiyo iliwavuta wengi wakiwemo mashabiki wa soka nchini kwa kuwa Arsenal inafanya vizuri, inagombea ubingwa wa ligi wakati Man United imekuwa ikisuasua, si kama ile iliyokuwa chini ya Alex Chapman Ferguson.

Mashabiki walitaka kujua kama kweli Manchester ya Moyes ingeweza kupambana na Arsenal ya Arsene Wenger ambayo inapambana vilivyo kuhakikisha inatwaa ubingwa huku United ikionekana imeishatoka kwenye mbio hizo licha ya kuwa mabingwa watetezi.

Kingine kilichowavutia wengi ni Arsenal kuwa na safu ngumu ya ulinzi lakini soka la kuvutia zaidi ya Man United ambayo wakati wa Ferguson ilikuwa ina sifa za kucheza kwa kasi na mara nyingi ilipokutana na Arsenal ndiyo iliyoonyesha soka la kuvutia zaidi.

Mashabiki wengi walikaa kwenye runinga na kutaka kuona kitakachotokea, kweli ilikuwa mechi nzuri iliyoonyesha ufundi wa juu, lakini ikawaudhi wengi baada ya dakika 90, matokeo yalikuwa sare ya bila kufungana.

Wanasema raha ya mechi mabao, hivyo mashabiki kila upande walitaka kuona mabao yanafungwa, nani angefunga, yupi alitoa pasi ya bao halafu mwisho simulizi la mechi yenyewe lizidi kuwa juu.

Wakati mashabiki wakionekana kutofurahishwa na mechi hiyo kwisha kwa sare ya bila kufungana, wataalamu ambao hufanya tathmini za kitaalamu kutengeneza takwimu za kila mechi katika Ligi Kuu England, Kampuni ya EA Sports, wao wakaipa cheo mechi hiyo.

Mechi kati ya Arsenal dhidi ya Man United ndiyo mechi bora ya wiki hiyo kutokana na namna ilivyochezwa pamoja na kwamba hakukuwa na bao hata moja lililofungwa katika dakika zote 90. Unaamini hilo?

Watalaamu hao wana vigezo vyao vya kitaalamu walivyovitoa kuhusiana na mechi ilivyokuwa hadi kuwa bora, sehemu ya vigezo hivyo ni kasi ya mchezo kwa mchezaji mmojammoja na mwendo wa kila timu, halafu wakachambua wachezaji.

Wataalamu hao wanaeleza kwamba, mechi hiyo wachezaji walikimbia zaidi kuliko mechi nyingine zote zilizochezwa wiki hiyo na jumla ya wingi wa kilomita kwa kila timu kama ukijumlishwa, maana yake ndiyo mechi bora na inaonyesha wachezaji walikuwa fiti zaidi.

Jumla ya kilomita walizokimbia wachezaji wote wa Manchester United walioanza na kuingia ni 74.1 wakati wenyeji Arsenal wenyewe walipata jumla ya kilomita 69.7 na kama zikijumlishwa ni kilomita 143.8.

Kilomita 143.8 kwa mechi moja ilikuwa juu zaidi ya nyingine zilizochezwa, pia ni kigezo cha kuonyesha timu zote zilikuwa fiti na mechi ilikuwa bora kwa kuwa kukimbia kwa umbali mrefu kunaonyesha hakukuwa na ujanja wa kupoteza muda na kila timu ilicheza kiushindani zaidi.

Kwa wachezaji mmojammoja, pia Michael Carrick ambaye huenda mashabiki wa Man United hawakuliona hilo, ndiye alikimbia kilomita 7.5 ambazo ni nyingi zaidi ya wengi uwanjani na kufuatiwa na Mikel Arteta aliyekimbia 7.3.

Ukiachana na wingi wa kilomita, walikuwepo wachezaji waliokwenda kasi zaidi ya wengine, hasa katika mipira ambayo walitanguliziwa au wale waliokuwa wakikimbizana na mafowadi kwenda kuondosha hatari langoni mwao.

Alex Oxlade-Chamberlain aliyecheza dakika 16 tu akitokea benchi, alikimbia kwa kasi ya kilomita 33.2 kwa saa na kuweka rekodi ya aliyekimbia kasi ya juu zaidi katika mechi hiyo na wachezaji wengine wote katika Premiership wiki hiyo iliyopita.

Alifuatiwa na beki Nemanja Vidic wa Man United ambaye alikimbia hadi kufikia kilomita 33.1 na wengine walioonyesha wana kasi kubwa ni Mesut Ozil (Arsenal) kilomita 32.9 na Chris Smalling, kilomita 32.4.


MAPAFU YA MBWA…

ARSENAL                               DAKIKA                      KM
Mikel Arteta                       90                             7.3
Santiago Cazorla               90                             7.0
Mesut Ozil                         90                             7.0
Jack Wilshere                    90                             6.9
Olivier Giroud                     90                             6.7

JUMLA YA MWENDO KWA WACHEZAJI WOTE 69.7



MAN U                              DAKIKA                      KM
Michael Carrick                 90                             7.5
Wayne Rooney                 90                             7.4
Robin van Persie               90                             7.0
Tom Cleverley                   90                             7.0
Chris Smalling                   90                             6.8

JUMLA YA MWENDO KWA WACHEZAJI WOTE 74.1


WENYE KASI KUBWA…WEN
ARSENAL                                 DAKIKA                        KM/H
Oxlade-Chamberlain               16                               33.2
Mesut Ozil                              90                               32.9
Olivier Giroud                          90                               32.6
Laurent Koscielny                    90                               31.3
Bacary Sagna                          90                               31.3    LaL

MAN U                                  DAKIKA                      KM/H
Nemanja Vidic                      90                               33.1
Chris Smalling                      90                               32.4
Juan Mata                            75                               32.4
Rafael                                  45                               32.4
Wayne Rooney                     90                               31.5






0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic