February 13, 2014

 
MASHABIKI WA MBEYA CITY KWENYE UWANJA WA SOKOINE, TAYARI KUIUNGA MKONO TIMU YAO. MWANZA HAWANA TIMU YA KUIUNGA MKONO NA WENGI WAMEKALIA MAJUNGU NA KUTOPENDANA?
ENZI zile za Pamba ya Mwanza ambayo ilipewa majina lukuki yakiwemo kama TP Lindanda, Wana Kawekamo na mengine mengi ambayo yalitokana na ubora wa kikosi cha timu hiyo.


Pamba ya Mwanza iliundwa na wachezaji wengi mahiri ambao walipokutana na timu nyingine iwe Yanga, Simba, Majimaji, Coastal Union, African Sports, Sigara, Pilsner, Nyota Nyekundu au nyinginezo, basi habari walikuwa wanaipata.

Soka wakati huo, kila timu ilikuwa na wachezaji wake nyota, nakukumbusha Majimaji yenye watu kama Celestine Sikinde ‘Mbunga’, Coastal Union yenye akina Razak Yusuf ‘Careca’, Kasa Mussa, Juma Mgunda na Wenzao, Reli Morogoro na watu kama Mbuyi Yondani na David Mihambo walivyokuwa na uwezo mkubwa, lakini bado Pamba ya Mwanza iliendelea kung’ara na kufanya vizuri.

Mara nyingi siku hizi, wanamichezo wengi katika mikoa wanasema wanasema wanashindwa kuwa na timu imara kwa kuwa enzi hizo walikuwa wakisaidiwa sana na mashirika kuziendesha timu, wachezaji walikuwa wakilipwa mishahara na baada ya hapo, mambo yamekuwa magumu.
Leo si lahisi tena kwa Mwanza kuwasikia wachezaji wenye sifa kama Fumo Felician, Kitwana Selemani, Mao Mkami ‘Ball Dancer’, George Masatu, Hussein Amani Masha, Khalfan Ngassa, Rajab Rashid na wengine wengi kwa kuwa tu, hakuna mipango tena.

Kweli hakuna mashirika ambayo yanakubali kuziongoza timu, kwa kuwa ni hivyo, pamoja na mkoa Mwanza kuwa na vipaji lukuki ambavyo vinaendesha karibu asilimia 50 ya timu za soka zinazofanya vizuri, wadau wake wamelala na huenda wanasubiri tena mashirika yaanze ili kujengwa kwa Pamba upya.

Mwanza ni mmoja wa mkoa unaoongoza kwa kuwa na wachezaji wakongwe waliowahi kung’ara katika soka, lakini leo hawana ushawishi wowote, wengi wamekalia majungu, wamejitenga na kuwa mamluki wa timu za Dar es Salaam huku wakiuacha mkoa wao maarufu kwa soka ukibaki hauna hata timu ligi kuu, aibu na kichekesho lakini ajabu hakuna anayeona aibu.

Wakati Toto African ikiwa Ligi Kuu Tanzania Bara, asilimia kubwa ya wakongwe wa Mwanza wenye mapenzi na Simba kwa kushirikiana na wadau wengine waliona bora iteremke daraja kwa kuwa ina asili ya Yanga. Lakini wako ambao wanashabikia Yanga, hawakutaka wenzao wenye mapenzi na Simba waingie na kuisaidia kwa madai si damu yao.

Sasa wote wamekaa hawana lolote wanalolifanya zaidi ya kucheza Ma-bonanza na ndiyo umekuwa umaarufu wa Mwanza wakati mkoa kama Mbeya sasa umefikisha timu mbili huku watu wake wakiendelea kuungana bila ya kutegemea kampuni yoyote.

Kama Mbeya City inasaidiwa na Manispaa ya Mbeya na sasa ndiyo timu kutoka mkoani, yaani nje ya Dar es Salaam inayofanya vizuri kuliko nyingine yoyote, vipi Mwanza ambalo ni jiji kubwa kuliko Mbeya na lenye vipaji lukuki vya soka lishindwe? Hiki ni kichekesho na ajabu wanasoka na wadau wa mchezo huo wamejazana Mwanza, wakiwa katika usingizi wa pono, hakuna anayejua na wanaabudu majungu.
Kweli kama ulifanikiwa wakati unacheza soka, ukaogelea sifa lukuki ambazo umezeeka nazo, halafu wakati huu unaogelea katika dimbwi la waliofeli kuhamasisha mafanikio ya mchezo uliofanikiwa, una haja gani ya kuitwa gwiji? Wakongwe wa Mwanza wenye majina makubwa wako wapi, nini kinawakwamisha na kama wao wana nia na wanakwamishwa, nani amefungua mdomo?
Au wanaridhika na umamluki wa kuona timu za Dar es Salaam zikifanya vibaya na wao kushangilia kwa njia ya redio na vyombo vya habari wakiamini inawatosha. Au hawaoni ni sahihi vijana kutamba hapo Mwanza kwa kuwa wanaweza kufuta walichokifanya wao kwa kupata sifa zaidi? Mimi nawaona ni watu wasio na mapenzi na mkoa wao, wasiojua umuhimu wa wanapoishi na badala yake wanakubali kuwa vibaraka wa Dar es Salaam kwa kuwa tu hawajui mapenzi ya dhati ya wanapoishi, yaani Mwanza.
Kama kukosea mmekosea sana, Mwanza haistahili inachopata katika soka la Tanzania na wanaosababisha ni wadau wakiwemo viongozi wa vyama vya soka na wakongwe lukuki waliojazana Mwanza wanaoshabikia timu za Dar es Salaam. Sasa badilikeni, mnaweza kujifunza kwa Mbeya wala msione haya hata kidogo.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic