April 2, 2014


Na Saleh Ally
PAMOJA na mambo mengi lakini hakuna ubishi kuwa Azam FC ndiyo timu yenye uhakika wa kumtwaa beki wa zamani wa Simba, Shomari Kapombe.

Kapombe ambaye alikuwa akikipiga nchini Ufaransa katika kikosi cha AS Cannes kinachoshiriki ligi Daraja la Nne nchini humo, tayari amerejea nchini na amekuwa akifanya mazungumzo na Azam FC.

Kawaida, Kapombe amekuwa mgumu kuzungumza lakini taarifa za kiuchunguzi za gazeti hili zimekuwa zikieleza namna mazungumzo kati ya Kapombe na Azam yanavyoendelea na hivi karibuni imebainika ameishavunja mkataba na AS Cannes.

Kinachomkwamisha ni kuwepo mgogoro wa malipo ya fedha zake za mshahara kutoka kwa AS Cannes, lakini bado kwa mujibu wa sheria za Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), Kapombe ana nafasi ya kusajili katika timu mpya.

Beki huyo kiraka alianza kung’ara na Simba ndipo AS Cannes kupitia wakala wa kuuza wachezaji anayetambuliwa na Fifa, Denis Kadito ambaye ni Mtanzania anayeishi nchini Uholanzi, ikamnasa na kuanza naye kazi.

Hata hivyo, Kapombe hakuwa katika wakati mzuri baada ya kujikutana safari yake ina misukosuko kibao pale alipoumia na kufanyiwa upasuaji wa kidole akiwa Ufaransa, hali iliyomlazimu kukaa nje kwa zaidi ya mwezi mmoja.

Aliporejea, alionyesha kiwango kizuri na kufanikiwa kupata namba huku benchi la ufundi la AS Cannes likimuamini na kumpa namba mbili au beki wa kulia.
Lakini taratibu migogoro ilianza  baada ya kurejea nyumbani kuichezea timu ya taifa, Taifa Stars dhidi ya Zimbabwe. Akachelewa kurudi na baadaye akatangaza kwamba anadai mshahara wake, mgogoro haukupoa mapema hadi ilipoelezwa Wafaransa hao wako tayari kumlipa.
Lakini baadaye Kapombe akashikilia msimamo wa kutaka kubaki nchini, kazi ya kuvunja mkataba na AS Cannes ikaanza na baadaye taarifa za Yanga na Azam FC kuanza kumuwania zikajulikana.
Baadaye ikaonekana Azam FC ndiyo wamekuwa ‘siriaz’ na suala la kumnasa Kapombe. Baadaye Simba wakaingilia na kudai bado Kapombe ni mchezaji wao, lakini bado hawakuonyesha kweli wako ‘siriaz’ kama ilivyo kwa Azam.
Kapombe amekuwa akijificha na kutotaka kulizungumzia suala lake, lakini Championi Jumatano lilifanikiwa kumpata na kufanya naye mazungumzo kwa ufupi.
Kapombe anasisitiza kweli ameamua kurejea nchini na anajua baada ya muda itajulikana anachezea timu gani lakini akitaka watu wawe na subira kwa kuwa mazungumzo yanaendelea ingawa dalili zote zinaonyesha kuwa itakuwa ni Azam FC. Msome anavyofafanua maswali.
Simba:
Ningependa sana kufanya mazoezi na Simba kwa kuwa ndiyo timu niliyotoka na sina matatizo nao, lakini kuna vifaa ambavyo ninavihitaji nisingeweza kuvipata lakini kwa Azam inakuwa rahisi kwa kuwa wana vifaa vya kutosha.
Pamoja na hivyo, kuna jambo la kocha, angalia mwendo wa Simba na aina ya kocha wao (Zdravko Logarusic), ni mkali sana wakati mwingine anawaweka nje wachezaji ambao ni wake.
Kwa hali ya kawaida tu kama binadamu nikaingia hofu, nikajiuliza kama kweli wachezaji wakikosea kidogo anawaadhibu au kuwaondoa mazoezini. Kwa mimi ambaye sijasajiliwa, lengo langu ni mazoezi, nitaweza kufanya mazoezi kwa uhakika na utulivu?
Azam:
Suala la Azam wananitaka au la, nisingependa liwe ndiyo gumzo. Lakini kweli nimeomba kufanya mazoezi kwao kwa kuwa ninajua nitapata kila kitu.
Lengo langu ni kuwa fiti na ikifikia nimekubaliana na timu fulani kuichezea na kuingia nayo mkataba, basi niwe katika kiwango kizuri kuliko kukaa tu ninasubiri.
Kingine ni suala la gharama, mfano pale kwenye Uwanja wao Azam, wana gym. Lakini kama ningefanya mazoezi na Simba, ningelazimika kuwa na fungu la kulipia gym tena sehemu nyingine.
Kwa sasa mimi sina sehemu inayoniingizia, hivyo siwezi nikawa ninatoa tu fedha bila ya kuingiza. Kwa kutumia vifaa vya Azam kwa kuwa vimekamilika, nitapunguza gharama na kufanya mazoezi ya uhakika.
Kurudi Ulaya:
Nimeamua kubaki hapa nyumbani na kweli kuna timu ambazo ninafanya nazo mazungumzo, hakuna upande ambao kila kitu kimekamilika, lakini baada ya muda nitaeleza kila kitu.
Nataka nikuhakikishie, sijawahi kuzungumza na mwandishi na kumueleza mambo mengi, angalau leo. Lakini mara baada ya kukamilisha suala usajili na nikiwa nimejua ninakwenda wapi, basi nitakuwa tayari kuzungumza.
Safari yangu ya Ufaransa ina mambo mengi sana, nitazungumza kuanzia nilivyoondoka hapa, nilivyofika na kufanya majaribio na mambo yote yatakavyokwenda. Hivyo vuteni subira kidogo.
Gharama:
Kweli kuna gharama za matibabu kama Cannes ambavyo wamekuwa wakisema, lakini mimi nilikataa kufanyiwa oparesheni. Unajua lilikuwa ni lengelenge tu, haikuwa ni mara ya kwanza kunitokea, hivyo nikawaambia sitapasuliwa.
Unajua hapa nyumbani hicho ni kitu cha kawaida tu, halafu unachofanya unatoa kile kingozi cha juu unaendelea na mambo yako. Lakini wao wakaona ni tatizo na lazima iwe vile, nikawakubalia.
Lakini subiri kwanza nimalize mambo yangu kama nilivyosema, halafu nitatoa ufafanuzi wa kutosha kuhusiana na suala hilo na mengine mengi.





0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic