April 4, 2014



 
Na Mwandishi Wetu
MAFANIKIO ndiyo majibu ya kufanya mambo kwa juhudi na maarifa na mwanasoka yeyote anayetaka kufikia mafanikio, hawezi kuridhika hadi wacheze kwenye vikosi vya timu zao za taifa.
Timu ya taifa ni sehemu ya kipimo cha mafanikio kwa mwanasoka au mwanamichezo yoyote, kwamba umefikia kiwango cha juu hadi kuwa mwakilishi wa taifa lako.


Bukaba Paul ni Mtanzania anayecheza soka la kulipwa nchini DR Congo na amepita njia tofauti kufikia hapo alipo zaidi akiongozwa na nia ya kutaka kupata mafanikio.


Mwanasoka huyo anayependwa kutumia jina lake la kwanza la Bukaba sasa anakipiga katika timu ya OC Muungano inayoshiriki Ligi Kuu nchini Dr Congo.
Bukaba ni kati ya wachezaji wachache nchini ambao wamefanikiwa kutoka nje na kucheza soka la kimataifa bila ya kuzichezea timu maarufu kama Yanga, Simba au Azam FC. Safari yake ilikuwaje hadi kufikia alipo sasa?

“Haikuwa safari lahisi kwa kuwa ilikuwa ni lazima kupita katika sehemu ambazo sikuwa na msaada zaidi ya mimi mwenyewe kupambana,” anasema Bukaba kutoka DR Congo.

Hadi DRC:
Nilipambana sana, nilifanikiwa kufuzu majaribio ya kuichezea Athletico Olympic ya Burundi, nilipambana na kufanikiwa kupata namba na msimu huo tukamaliza ligi tukiwa wa pili nyuma ya Vital’O.
Baada ya msimu mmoja tayari nilianza kuonekana na timu ya OC Muungano ilifanya mazungumzo na timu yangu ya Burundi na baada ya muda mambo yakaenda vizuri nikaja hapa Congo. Hadi sasa naendelea vizuri kabisa.

Kiwango:
Kama ni kiwango cha fedha hapa Congo kipo juu zaidi ya Burundi na hata nyumbani Tanzania, hivyo ninapambana zaidi ili nijiunge na timu kubwa zaidi za hapa au nchini nyingine.

Nyumbani:
Nilianzia nyumbani lakini kimyakimya sana, nilianza kucheza soka nikiwa na miaka nane. Nilisoma kule kwetu Ukerewe, nikiwa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Nakoza, nilichaguliwa katika timu ya Taifa Cup ya Mwanza. Baada ya mashindano, Toto African waliniona wakanisajili, wakati huo tayari nilikuwa ninacheza Nansio United ya kwetu Ukerewe hiyo ilikuwa mwaka 2011.
Mwaka uliofuata nilipata nafasi ya kucheza Kombe la Uhai chini ya miaka 20 nikiwa na mkoa wa Mwanza. Baada ya hapo nilirejea na kuitumikia Toto kabla ya kwenda Burundi kufanya majaribio ambako nilifuzu.

Anachotaka:
Kwa sasa natamani kuichezea timu yangu ya taifa, Taifa Stars. Nina uwezo huo sema inakuwa vigumu kuniona, lakini ningependa wasogee na kuniona ninapokuwa kazini.

Simba&Yanga:
Najua ni timu kubwa, niko tayari kama watanihitaji. Kikubwa ni kufanya utaratibu na mimi nitaangalia kama maslahi wanayotangaza yananifaa basi itakuwa vizuri.
Zaidi:
Pamoja na mambo yote, kweli natamani sana kucheza soka Ulaya, hii ni ndoto yangu. Najua si kitu lahisi lakini nitapambana hadi kuhakikisha nafika.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic