April 4, 2014



 
MGAMBO...
LIGI Kuu Bara inaelekea ukingoni na asilimia kubwa inaonyesha Azam FC huenda kwa mara ya kwanza itakuwa ndiyo bingwa mpya wa Tanzania Bara.

Azam FC ambayo imeanzishwa katika kipindi kifupi kisichofikia miaka kumi, sasa imekuwa tishio na kero kubwa kwa timu kongwe za Yanga na Simba ambazo zimeanzishwa zaidi ya miaka 75 na zimeshindwa kukua kwa maana ya maendeleo.
Simba na Yanga ndiyo kongwe, zina mchango wao mkubwa katika soka nchini, lakini zina sehemu ambazo zimechangia kwa kiasi kikubwa kudumaa kwa mchezo huo kama zile migogoro, kujenga makundi ya watu wenye nguvu lakini wasiokuwa na changamoto za mafanikio kwenye soka.
Yanga na Simba, hadi sasa ni mfano mbaya kwa kuwa zimeshindwa kumiliki hata uwanja wa kuingiza watu 20 ambao utakuwa na sehemu nzuri ya kuchezea ambayo ni afya kwa wachezaji wao na mfumo wa kitaalamu ili kwenda na wakati.
Leo utawaona Yanga wanalazimisha timu yao kwenda kufanya mazoezi kwenye uwanja mbovu kabisa huku watani wao Simba wakifanya porojo ya kupeleka watu kwenda kufyeka uwanja wao wanaoumiliki nje ya jiji la Dar es Salaam ambako hakuna lolote la maana!
Sasa ligi inakwenda ukingoni huku mabadiliko yakionyesha wakati wa mabadiliko ni sasa na kama kuna watu wabunifu au wenye malengo ya kufanya mambo bora katika soka, si lazima wawe Yanga au Simba pekee.
Wanaweza kwenda Mgambo FC, angalia inakaribia kuteremka daraja lakini imeweza kushinda na kuzifunga Yanga na Simba katika mechi zake mbili kwenye Uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga.
Ukilinganisha Mgambo dhidi ya Yanga na Simba, karibu kila kitu timu hizo kongwe zitakuwa juu. Mfano, mishahara mikubwa, kuwa na wachezaji wa kigeni, huduma kwa makocha na wachezaji lakini Mgambo FC imeshinda.
Kikubwa ambacho kiliwabeba Mgambo itakuwa ni nidhamu ya mazoezi, mfumo wa uongozi na nidhamu ya uwanjani kufuata maelekezo kutoka kwa walimu wao, kitu ambacho kina matatizo katika timu nyingi kubwa na hasa Yanga na Simba.
Inawezekana Yanga na Simba wakawa na lawama nyingi kipindi hiki kwamba walihujumiwa katika mechi hizo au kulikuwa na tatizo. Lakini mfumo na mwendo wa maisha ya klabu hizo na timu zake kuna tatizo kubwa sana na lazima wakubali ili kujifunza na baadaye kubadilika.
Azam FC nao wanataka kuuchukua ubingwa, pia kutakuwa na walakini kama Yanga au Simba watatanguliza lawama katika kitu fulani kuhusiana na hilo. Badala yake waangalie na kukubali walipokosea na kujifunza.
Dunia inabadilika kwa kasi sana, kuna mengi ya kujifunza kila kukicha kwa kuwa watu wanajifunza na wanaelimika. Wako tayari kufanya mambo mapya, hivyo lazima Yanga na Simba wajiangalie upya, la sivyo wataishia kwenye lawama na mwisho utakuwa ni mwanzo wa kuanguka kwao.
Simba iko mbioni kugombea nafasi ya tano, dalili zinaonyesha wakizubaa hata nafasi ya nne itakuwa kazi kubwa kwao. Kuna la kujiuliza hapa na utaona chanzo kikubwa ni kutokuwa na uongozi imara, uongozi uliokuwa ukilumbana kila kukicha na haufanyi mambo kwa manufaa ya timu.
Kwa wale wanaofanya mambo yao kishabiki wanaweza kuwa wagumu sana kuamini au kukubali, lakini mwendo wa klabu zao si mzuri kwa kuwa zinakwenda kwa mfumo wa kizamani, hazitaki kujifunza na zinaamini sana historia kuliko hali halisi.
Kubadilika ni muhimu na moja ya mambo yanayoweza kuonyesha kuwa watu wamekubali kuwa na mafanikio ni viwanja na vifaa bora vya mazoezi, mfumo mzuri wa kudhibiti fedha ili kila inayopatikana itumike kwa manufaa ya klabu.
Lakini pia kuwaachia makocha kama wataalamu au wataalamu wengine kwenye klabu wafanye kazi zao si kwa matakwa ya viongozi, badala yake kwa kufuata utalaamu. Azam FC inabadilisha mambo kidogo tu na imeweza kufanikiwa na ukiangalia utaona ilipopitia ni kwenye mashimo ambayo Yanga na Simba walishindwa kuyafukia.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic