August 18, 2014



USIANZE kwa kuniuliza umuhimu au walichokifanya wachezaji kama Edibily Lunyamila au Shadrack Nsajigwa ni kipi katika soka hapa nchini, hakika utakuwa unajua mengi.


Ukitaka nikukumbushe, nitasema walikuwa tegemeo katika kikosi cha timu ya taifa, Taifa Stars, lakini kwenye kikosi cha Yanga, pia Simba. Walijituma, walionyesha kweli wanaifanya kazi yao kwa juhudi kubwa.

Sasa nawatambua kama wachambuzi wa masuala ya soka katika gazeti hili maarufu la michezo la Championi. Maana yake maisha yao kwa asilimia 95 ni soka, pia utaona sasa Nsajigwa ni kocha wa vijana wa Yanga, maana yake ataendelea kujifunza mengi na kutokoma kutoa mchango wake katika mchezo huo nchini.

Si wao tu, wapo wengine kama Madaraka Selemani, Selemani Matola, Bakari Malima na wengine wengi ambao mchango wao kwa taifa letu katika mchezo wa soka ulikuwa ni mkubwa sana.

Inawezekana hatuwapi thamani kubwa, lakini tunapaswa kufanya hivyo ingawa leo nina ushauri kwao kwamba kuna jambo la kujifunza ambalo nimeliona, ningependa waige.

Ukweli sijui wachezaji hao niliowataja au wenzao wa kariba yao wamejaaliwa watoto wa wanawake au wanaume, yote ni mambo ya Mwenyezi Mungu lakini hili la kujifunza litakuwa linawahusu.

Wakati Kocha Patrick Phiri, maarufu kama Big Phiri alipotua nchini kuja kumalizia mazungumzo na Simba kabla ya mkataba mpya, aliongozana na mwanasheria wake. Pamoja na kwamba aliwahi kuifundisha Simba kwa vipindi viwili tofauti, lakini hii ilikuwa ni mara ya kwanza kufanya hivyo.

Yule mwanasheria aliyeongozana naye, aliwaambia viongozi wa Simba kuwa ni meneja wake, lakini baadaye akawatambulisha ni mwanasheria wake pia. Halafu mwisho ikagundulika ni binti yake wa kumzaa.

Anaitwa Melesiana Patrick Phiri, namkadiria kuwa na miaka kati ya 24-26. Alionekana ni mtulivu muda wote na taarifa zinaeleza hata wakati wa kujadili mkataba huo na viongozi wa Simba, yeye ndiye alikuwa mzungumzaji mkuu.

Taarifa zinaeleza Melesiana aliwachachafya viongozi wa Simba kutokana na kuuliza maswali kibao kutaka kupata uhakika wa mkataba wa mzee wake au ukipenda sema ‘mteja’ wake.

Hata alipoambiwa atapewa nyumba, Melesiana alihakikisha kwanza anaiona ni ya kiwango kipi na mwisho alipata fedha yake kama mwanasheria kutoka kwa Mr Phiri, halafu ndiyo akarejea Zambia.

Tusizungushe mambo, suala la elimu na soka barani Afrika limekuwa na walakini. Waliosoma hadi elimu ya juu ni aghalabu, hili linajulikana kutokana na mfumo wa maisha yenyewe, si Tanzania au Zambia pekee, sehemu nyingi za bara letu au hata Asia na Amerika Kusini.

Phiri ameliona hilo, amesisitiza elimu kwa wanaye na Melesiana sasa amekuwa msaada kwake na anamsaidia baba sasa kupeleka mambo kitaalamu na katika mpangilio ulio sahihi.

Kwa kifupi Phiri sasa ana msaada katika kazi zake, ndiyo maana leo nikakumbuka kuwakumbusha wachezaji wakongwe wa hapa nyumbani kwamba hawajui mbele baadaye itakuwaje.

Hivyo wana jukumu la kusimamia elimu za watoto wao ambao baadaye wanaweza kuwasaidia kama ambavyo Melesiana anavyosimamia maslahi ya Phiri ambayo ndiyo maslahi ya familia yake.

Unaposimamiwa kimaslahi na baba, mama au mtoto, uchungu kwa mwenye akili nzuri unakuwa juu na unaongeza chachu ya utendaji. Hivyo Melesiana amemsaidia Phiri kuzungumza au kuongoza yale ambayo angeshindwa kuyaongoza kwa kuwa kazi yake kubwa ni kufundisha mpira.

Wachezaji wakongwe, wasimamieni watoto wenu wapate elimu zaidi, wajue umuhimu wake na wasiamini au kuishia mlipoishia nyie kwa kuwa huko mbele, safari ni ndefu na ushindani utakuwa juu zaidi.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic