August 18, 2014



Na Saleh Ally
BILA ya kujali ni kwa saa ngapi lakini ukweli ni kwamba, mechi ya kwanza ya Ligi Kuu England msimu wa 2014-15, imeionjesha Manchester United utamu wa mkiani.


Baada ya kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Swansea, Manchester United ikawa katika nafasi ya 20.

Haitafutika kwamba Manchester United ilipoteza mechi yake ya kwanza ya ligi na kuvunja rekodi huku ikiweka mpya kwa kuwa tangu mwaka 1972, haikuwahi kufungwa katika mechi ya ufunguzi, tena nyumbani.

Swansea wameivuruga Man United katika mechi ambayo imeonekana kuwavuruga sana mashabiki wa Man United ambao wengi wameonyesha kuwa, tabia za mashabiki hazipishani sana bila ya kujali wako Afrika au Ulaya.


Mashabiki wa Man United hapa Bongo, walikuwa wakilalama na kuona kuwa kipigo hicho ni tatizo kubwa, wengine wakitaka van Gaal aondoke. Lakini hata wale wa Ulaya na Asia, pia waliungana na wenzao wa Bongo kwa kumshambulia van Gaal kupitia Mtandao wa Twitter.

Kinachowauma ni kwamba hata David Moyes aliyeonekana ni ‘boga’, alianza mechi yake dhidi ya Chelsea kwa sare ya bila mabao. Vipi van Gaal, kocha wa ‘level’ ya Kombe la Dunia anafungwa na Swansea, tena ndani ya Old Trafford?

Katika mahojiano na runinga ya Sky ya Uingereza, van Gaal alizungumza kitu ambacho kama utatulia, utagundua Man United ina nafasi ya kurejea tena na kufanya vizuri ndani ya mechi mbili hadi tatu zijazo.

Ingawa kuna hofu kwamba kutokana na kuanza vibaya kwa van Gaal, basi Man United itaboronga zaidi ya msimu uliopita, lakini ukweli haitakuwa hivyo kama tayari kocha huyo ameliona hilo na majibu aliyoyatoa ni ushahidi tosha.


Alisema haya: “Kweli kipindi cha kwanza wachezaji walionekana kama waoga, wenye hofu na sielewi kwa nini. Tatizo jingine katika kipindi hicho, nilifanya uchaguzi kuwapa nafasi wachezaji ambao hawakuwa sahihi.


“Kipindi cha pili pamoja na kufanya mabadiliko, bado timu haikucheza kitimu kabisa. Hili nalichukua mimi kuwa ni tatizo langu, kwa kuwa ndiye ninayewajibika.”

Hii inaonyesha kweli van Gaal ni mkomavu, hakwepi majukumu, yuko tayari kujifunza na anaweza kuleta mabadiliko kama ataungwa mkono katika wakati huu mgumu badala ya kusakamwa.




Pre season:
Kipindi cha pre season ni kile cha kujiandaa na ligi, Man United ilifanya vema ikiwa ni pamoja na kufunga mabao hadi 7 katika mechi moja. Mashabiki wake wakachekelea sana huku wakiwa wamesahau ligi na mechi za kirafiki kuna tofauti kubwa.

Kipigo cha Swansea kinaweza kuwa somo kwa wale wanaoutabiri mpira kishabiki badala ya utalaamu, maana pre season ni kutengeneza timu na wala si mashindano.

Subira:
Kwisha kwa msimu wa 2013-14 huku Man United ikiwa imebaki katika nafasi ya saba na kukosa nafasi ya kushiriki Ligi ya Mabingwa Ulaya, iliwaumiza sana mashabiki wa Man United, wakaamini Moyes ndiye tatizo.

Asilimia 90 ya mashabiki wa Man United waliamini baada ya kuondoka kwa ‘tatizo’ Moyes, basi mambo yangekwenda vizuri na heshima ingerejea.

Hviyo mechi ya kwanza ya ligi ndiyo ilikuwa imejaa jibu la subira waliyoihifadhi tangu mwishoni mwa msimu uliopita.

Jibu limekuwa tofauti, ingawa hakuna kitu kibaya sana lakini imeonekana kuwaumiza na wengi wamezungumza kuwa bora Moyes, bila ya kujikumbusha kuwa walimzomea au kumshambulia sana msimu uliopita.

Mfumo:
Mfumo wa 3-5-2  alioutumia van Gaal, unaweza kuwa kweli una tatizo na hasa suala la kwenda taratibu kutokana na kasi ya Premier League.

Hata angekuwa nani angechanganyikiwa, ndani ya miezi 10, wachezaji wa Man United hasa wale wa zamani, wanakutana na mifumo ya makocha watatu tofauti, Alex Ferguson, Moyes na van Gaal. Si rahisi.

Bado ana uwezo wa kuendelea nao au kuacha, kila kitu bado ni chaguo lake. Lakini hana ujanja, lazima aongeze kasi ili kuendana na ule mfumo wa Man United.

 Beki wa kati:
Kwa mabeki wa kati waliocheza, Chris Smalling na Phil Jones, Man United haina ujanja. Lazima ihakikishe inapata beki mmoja wa kati kisiki na mzoefu kwa kuwa walivyocheza katika mechi hiyo, bora hata Rio Ferdinand ambaye alionekana umri umemtupa mkono na hafai kabisa!

Tatizo lilikuwa ni namna ya kujipanga, kukaba hadi kuwanyima raha washambuliaji, haikufanyika hivyo kuwafanya wacheze wanavyotaka kama lilivyopatikana bao la kwanza kwa kuwa mfungaji alikuwa peke yake hadi akaamua wapi pa kupiga na haipishani sana na bao la pili.

Lakini kiungo pia hawakuwa wakikaba vilivyo, hii ilionyesha kiasi gani Man United inahitaji kubadilika katika hilo kwa kuwa Swansea walipiga pasi 28 bila ya kuguswa hadi walipofunga bao la kwanza.

Kuinuka:
Nani anasema Manchester United haiwezi kuinuka baada ya kipigo katika mechi ya kwanza au ufunguzi wa Ligi Kuu England, tena ikiwa nyumbani?

Van Gaal alifundisha Barcelona akachukua makombe, hali kadhalika Bayern Munich. Anajua harufu ya La Liga na Bundesliga, sasa ameonja chumvi ya Premier League.

Kwa uzoefu wake ana uwezo wa kubadilisha mambo ingawa bado uongozi wa Man United una kazi ya kumuunga mkono kama alivyofanya mwenyekiti, Edward Martin aliyemuunga mkono Ferguson kuanzia mwaka 1986 hadi 1990 alipotwaa Kombe la FA kwa mara ya kwanza.

Kila mmoja kwenye uongozi hadi mashabiki waliokuwa wanaingia na mabango uwanjani, walitaka aondoke. Yeye akashikilia msimamo kwa kuwa aliamini ni kocha bora. Nani atakataa van Gaal si kocha bora? Basi wamlinde ili aweze kufanya mabadiliko na kutengeneza mfumo ili kazi iende anavyotaka.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic