August 1, 2014





Na Saleh Ally
KUMEKUWA na mambo mengi sana yanazungumzwa kuhusiana na kukatishwa kwa mkataba wa makocha Hans van der Pluijm na msaidizi wake, Charles Boniface Mkwasa.

Pluijm na Mkwasa kwa pamoja walikuwa wanainoa Yanga, lakini baadaye wakapata ‘pande’ la kuifundisha Shaolla FC ya Saudi Arabia, hivyo wakaamua kwenda kuanza maisha mapya katika nchi hiyo ya Mashariki ya Kati.


Mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly wakati wakiwa Yanga ndiyo ilimvutia wakala wa soka nchini Misri, kumfanyia mpango Pluijm raia wa Uholanzi ambaye baada ya kutua Saudi Arabia aliwashawishi mabosi wake wapya ‘wamvute’ Mkwasa, dili likakubalika.

Wakiwa huko walifanikiwa kuanza kazi vizuri na mwanzo ilionekana kama mipango ilikuwa inakwenda kama kila kitu kilivyopangwa, lakini wiki ya mwisho ikawa ngumu sana kwao.

Siku nne zilizopita, gazeti hili lilipata taarifa ya mkataba wao kusitishwa, juhudi zikaanza kufanyika kuwatafuta wao ili waweze kuelezea suala hilo na aliyekuwa wa kwanza ni Mkwasa ambaye alifafanua.

Baadaye gazeti hili pia lilifanikiwa kumpata Pluijm naye akafunguka lakini ombi likawa kama anaweza kuandika barua inayoelezea kuhusiana na kilichotokea, hakuwa mbishi, akaandika.

Zifuatazo ni barua za maelezo za Mkwasa na Pluijm kuhusiana na sakata hilo wakielezea A to Z ya mambo yalivyokuwa.


BARUA YA PLUIJM:

Hallow Saleh
Habari yako, kuhusu hapa katika klabu tunayofanya kazi, mambo si mazuri. Nitafafanua, kabla ya sisi kuanza kazi, klabu hii ilikuwa na wachezaji wengi nyota kutoka Mali na Morocco, lakini waliondoka na tulipouliza kwa nini, hatukuelezwa sababu.

Tulipoanza kazi, baadhi ya viongozi walitaka kutuletea wachezaji wa kiwango cha chini, wengine ni wa daraja la chini na wale ambao tuliona kwa tulichotaka, wasingekuwa na msaada kwa timu.

Tulikubaliana kuwapa nafasi, tukafanya nao mazoezi kwa siku 3 halafu tukaamua kuwaondoa, waende zao.

Wiki tatu ambazo tulifanya kazi na timu, zilikuwa nzuri na wachezaji walifurahia namna tulivyofanya nao kazi na muhimu zaidi, ilionekana kuna mabadiliko ya kiwango kuboreka. Wachezaji hao walionyesha hali ya kutuamini zaidi kitu ambacho kilikuwa kizuri kwetu.

Pamoja na hivyo, baadhi ya wachezaji hawakuwa wameanza mazoezi pamoja nasi na tulielezwa hawakuwa wamelipwa tokea msimu uliopita, baadaye tukagundua kulikuwa na matatizo mengi ya kifedha na kiuongozi!

Baada ya kuwa tumewakata wachezaji kama 10 hivi walioletwa kwa ajili ya kufanya majaribio, hapo ndiyo matatizo yalipoanzia.

Viongozi wakaja kwangu na Charles (Mkwasa) na kutueleza kuwa mkataba wetu umesitishwa, inashangaza sana, lakini ndivyo ilivyokuwa.

Sasa tuko kwenye maandalizi ya kila mmoja kutaka kurejea kwao.
Salamu kwenu
Kocha wa zamani wa Yanga
Hans.


BARUA YA MKWASA:
Salaam,
Nafikiri nyote hamjambo hapo nyumbani, hapa hali imebadilika ghafla baada ya kocha na uongozi kushindwa kuelewana kutokana na usajili wa wachezaji wapya kwa msimu ujao.

Viongozi waliwaleta wachezaji kwa majaribio ambao kwa muono wa kawaida hawakuwa na uwezo mzuri, kwa jumla tuliwakataa na pia walikuwa wanataka wachezaji kutoka madaraja ya chini pia walikataliwa, wao hawakupendezewa nalo, hivyo wakaamua kusitisha mikataba yetu kwa sababu kubwa wanasema hawana fedha.

Msimu uliopita timu hii ilishika nafasi ya 12 ambayo ni timu ya mwisho kubaki daraja hivyo Kocha Hans alitaka wasajili wachezaji wenye uwezo ili waweze kufanya uzuri, kama haitoshi wachezaji wachache wazuri wa Shoulla wa msimu uliopita nao walihama, hivyo timu ilikuwa inahitaji wachezaji wengine wa hali ya juu.

Habari ndiyo hiyo, likiharibika lawama kwa kocha, lakini usajili wanataka wachee. Taratibu za safari ya kurudi ma kwetu zinafanyika.

Asante sana kwa ushirikiano wako na Mungu akipenda tutaonana.
Wako.
Charles B. Mkwasa

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic