August 1, 2014

IKANGAA ENZI ZAKE.


WAZIRI wa mambo ya nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe ameonyesha kushangazwa kuhusiana na maandalizi waliyopata timu ya Tanzania katika michuano ya Jumuiya ya Madola na matokeo ya mwisho yaliyopatikana.


Wakati akizungumzia kuboronga kwa timu iliyokwenda Jumuiya ya Madola, Membe alizungumza vizuri kama mzazi ambaye anaonekana hataki kuharibu mambo, lakini maneno yake yalikuwa yanaashiria maswali mengi.
 
BAYI
Alisisitiza timu ikirejea, basi angependa kupata maelezo kuhusiana na kilichotokea lakini aliumia sana na timu hiyo kufanya vibaya.

Membe kwa niaba ya serikali, alifanya juhudi za kufanikisha kambi za wachezaji wengine walikwenda Ethiopia, China na kwingineko, hiyo ilikuwa ni sehemu tu ya maandalizi.

Wakati Membe anasubiri timu ikirudi ajue kipi kilikuwa tatizo, pumba zimeanza kuzagaa baada ya baadhi ya viongozi walioongozana na timu hiyo kuanza kutoa sababu ‘biskuti’, yaani zisizokuwa na msingi hata kidogo.

Meneja aliyeongozana na timu hiyo, Muharami Mchume alikaririwa na vyombo vya habari jana akisema, eti walishindwa kufanya vizuri kutokana na waamuzi kuwabania.

Haya ndiyo maneno ambayo tumekuwa tukielezwa tokea miaka ya 1990 wakati Tanzania ilipoanza kuboromoka kwa kasi kubwa kwenye mashindano ya kimataifa. Huenda viongozi wa sasa bado wanaishi enzi hizo, hawajui lolote.

Nasema hawajui lolote kwa kuwa sasa kila kitu kinaonekana, watu wameona kila kinachoendelea na sijui kama kweli kwenye riadha kunaweza kuwa na mwamuzi ambaye atakuonea. Pia kwenye ngumi, tuliona nahodha Selemani Kidunda akipigwa hadi kuchanika puani. Bado kocha akasema ameonewa, meneja naye ameungana naye, hawa watu wa aina gani?

Katika hali ya kawaida, tayari wameunda sera ambayo watarudi nayo nyumbani, kwamba wameonewa. Maana yake watakuja na mabegi ya nguo na viatu vya “mitumba” na “sale” walivyonunua, pamoja na mizigo rundo ya sababu za kijinga.

Membe anachosubiri, hatakipata. Hilo ninaweza nikamhakikishia kwa kuwa kufanya kwetu vibaya katika michezo ya kimataifa, pia huchangiwa na uongo na watu kutoamini kwamba kiwango chetu kiko chini. Kwanza tukubali, halafu tuanze kujiboresha ili kukipandisha, hivyo tutaweza.

Mimi naweza kuwa nina ushauri kwa Membe, nimueleze kwamba kwa hali ilivyo ya migogoro katika vyama vya ngumi na riadha, nadra kuwa mafanikio hata kama timu zitasafirishwa China, Marekani na kwingineko.

Kuna migogoro mingi, hata wale magwiji wa michezo hiyo hawana ushirikiano mzuri. Najua wataficha, wengine watakasirika kwa maandishi haya, lakini ukweli shujaa wa nchi hii kwenye riadha kama Juma Ikangaa na Filbert Bayi, hawako karibu na wanahitaji kukutanishwa.

Bayi ana sifa zake, atakuwa na mchango wake na huenda anafaidika na michezo hiyo kwa sasa kwa kuwa timu zikiweka kambi zinaweka kwenye shule yake, anasaidia kidogo na yeye anapata kidogo na mambo yanakwenda, shukrani.

Vipi kuhusu Ikangaa, shujaa wa Tanzania katika riadha, ikiwezekana mwanariadha mwenye medali nyingi kuliko mwingine katika historia ya nchi hii. Mbona hatumuoni, vipi hashirikishwi na maneno mengi na ninaweza kusema hapewi heshima yake. Kweli Ikangaa, Bayi wakiungana hatuwezi kuwa na mafanikio?

Siwezi kusema kuna hofu ya kufunikwa, mfano Ikangaa akionekana sana, wengine hawataonekana. Ninacholenga ni kuonyesha ushirikiano kuwa ni duni na sasa ndiyo wakati mwafaka mjue kuwa inapofikia timu ya Tanzania inakwenda Jumuiya ya Madola au Olimpiki, tambueni ni suala la utaifa.

Hivyo mashujaa wa taifa wapewe nafasi na viongozi wafanye kazi zao kwa kuangalia maslahi ya taifa letu na si nafsi na matumbo yao. Tumechoka kuabishwa, angalieni mlilia maandalizi hakuna 
sasa mmehamia kwa waamuzi. Oneni haya, mnatuumiza wajomba!
SOURCE: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic