August 11, 2014


FELLAINI


Na Saleh Ally
WAKATI mwingine inakuwa ni vigumu sana kukubali, lakini mambo yanapozidi kuwa magumu, kunakuwa hakuna mjadala tena.

Soka linakwenda na bahati au aina ya uchezaji katika timu fulani kutokana na kocha anataka nini, ndiyo maana mchezaji anaweza kung’ara hapa, akashindwa kule.


Kuna wale wanaoshindwa kule, lakini wakaenda sehemu fulani na kufanya vema kuliko ilivyotarajiwa.

Kwa misimu miwili, wachezaji wengi wameishindwa Manchester United ambayo wanaonekana hawana bahati nayo na si uwezo.

Wachezaji hao wamekuwa gumzo si England tu, hata Tanzania na duniani kote, kwamba ni mizigo, hivyo waondoke.

Kocha Louis van Gaal, mara tu baada ya kuchukua ‘job’, sasa ameruhusu wachezaji kadhaa waende zao.

Hawezi kusema ni mizigo, lakini ukweli ndiyo huo kwa kuwa wanaonekana hawana faida licha ya kuwa na uwezo wa juu na rekodi nzuri nyuma. Hivyo wanatakiwa waende zao, ili Man United iingize fedha na kujiongeza.

Marouane Fellaini
Alitua Man United msimu uliopita akitokea Everton baada ya Kocha David Moyes kumvuta kwa kuwa anajua ni ‘jembe’ lake.

Man United ilimwaga pauni milioni 27.5, lakini sasa iko tayari kumuuza kwa pauni milioni 20, ingawa inaonekana watapata si zaidi ya pauni milioni 15 tu.


Javier Hernandez 'Chicharito'

Idadi ya mabao na dakika alizocheza Man United zinamfanya kuwa mmoja wa wachezaji bora kabisa wa United. Lakini hapati nafasi ya kutosha ya kucheza mbele ya Wayne Rooney na Robin van Persie, hilo ndiyo tatizo lake na ajabu, Man United huwa haitaki kumpa nafasi kwa kuendelea kutafuta mastraika wengine.

Jiulize akiingia ‘sub’ anapiga mabao, vipi hapewi nafasi ya kutosha ili ajiamini zaidi na kuendelea kuwa hatari zaidi? Huenda hana bahati.

Man United inataka kumuuza kwa pauni milioni 12, lakini bila shaka itapata angalau pauni milioni 10 tu.

Jamaa ni mkali na tayari timu kibao kubwa kama Juventus na Inter Milan (Serie A), Atletico Madrid (La Liga), Tottenham na Southampton (Premier League), zinamhitaji.

Anderson
Ni kati ya wachezaji wenye uwezo mkubwa, lakini inaonekana majeraha kila mara limekuwa ni tatizo kwake.

Kocha Alex Ferguson hakukubali aondoke hadi mwisho alipokaribia kustaafu akamtoa kwa mkopo Fiorentina.

Lakini sasa mambo yanaonekana ni magumu na van Gaal amemuonyesha mlango aende zake.

Nani anaweza kusema Anderson si kiungo mzuri? Ana kila kitu, lakini Man United inaonekana si kwake.

Nani
Misimu miwili iliyopita amekuwa ndiye chachu ya aina ya mashambulizi ya Manchester United. Kasi kubwa, krosi za hatari na mashuti ya kushtukiza.

Lakini mambo yamebadilika, amekuwa kama ‘amerogwa’ na kila anapopewa nafasi, anaboronga.

Man United imeonyesha uvumilivu wa juu, lakini wapi na sasa bosi mpya ameamua kumpa nafasi akajaribu kwingine.

United iko tayari kumuachia kwa pauni milioni 15.

Shinji Kagawa
Mjapani ambaye Ferguson alimnunua kutoka Borussia Dortmund, lengo likiwa ni kuimarisha kiungo cha Mashetani Wekundu.

Kagawa kajitahidi kupiga gia ili ainuke, lakini wapi na ukweli huenda staili ya Man United imemshinda.

Ujio wa Juan Mata kutoka Chelsea ndiyo unazidi kutia mchanga kitumbua chake na sasa United iko tayari kumuuza kwa pauni milioni 10, ila zikipatikana 8 hamna noma, biashara inafanyika.

Kocha wake wa zamani, Jurgen Klopp anaonyesha bado anamkubali na huenda akarejea Dortmund lakini wabishi Atletico Madrid, wanaona anawafaa.

Wilfried Zaha
Akiwa Crystal Palace alionyesha uwezo mkubwa na wengi wakaamini ndiye Pele wa England, Ferguson akajipinda na kumuwahi kabla bei haijaenda juu.

Hakumtumia sana, alipoingia Moyes, kukawa na mgogoro kwamba dogo anakula raha na binti yake bosi ndiyo maana hapangwi.

Sasa van Gaal amesema acha dogo aende zake na United iko tayari kulamba pauni milioni 10 ili impige bei.

Timu kibao zinamkubali na zinaamini atafanya vizuri na West Ham, QPR, Crystal Palace na Newcastle, mojawapo inaweza kumpata.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic