August 6, 2014



Na Saleh Ally
KUPITIA runinga ya Msumbiji iliyoonyesha mechi ya Tanzania dhidi ya Msumbiji waliokuwa kwao, nilimuona beki Shomari Kapombe akiangua kilio mara baada ya mechi.


Sura ya Kapombe iliashiria uchungu au uzalendo kwa kuwa alitaka kushinda mechi hiyo na kuiona Tanzania inafuzu kwenye hatua ya makundi kuwania kucheza Kombe la Mataifa Afrika.

Mjadala umekuwa kuhusiana na kilio hicho cha Kapombe, kitu ambacho naona hakiwezi kuwa cha msingi katika mjadala huu wa kwa nini Tanzania imekuwa ni timu ya “ilibaki kidogo tu.”

Sidhani kama ni kipindi sahihi kujadili eti Kapombe alimwaga chozi, unaweza kuichukulia kama ni sababu binafsi ya uzalendo wake kwa taifa. Lakini bado Kapombe na wenzake ni sehemu inayohusiana na suala la kufeli kwa Stars.

Mchezaji gani wa Taifa Stars anaweza kujitoa kwenye timu na kusema mimi tu ndiyo nilifanya vizuri zaidi? Lakini kama maandalizi waliyopewa na TFF hayatoshi au hayakuwa sahihi, wanapaswa kusema pia.

Kwa hiyo wachezaji pia ni sehemu ya kufeli kwa timu yetu. Safari hii inabidi wawajibike kwamba wametufelisha na hakuna zaidi ya hilo. Hivyo acha Kapombe alie lakini ukweli ni hivi, wachezaji ni sehemu ya kufeli kwetu.

Mjadala mwingine ni kuhusiana na mwamuzi wa mechi hiyo, Dennis Bate kutoka Uganda pamoja na msaidizi wake kwamba ‘waliiuma’ Taifa Stars na ‘kuibeba’ Mambas ambayo iliibuka na ushindi wa mabao 2-1 na kusonga kwenye hatua ya makundi.

 Sababu nyingine ya Taifa Stars kutolewa imekuwa ikielezwa ni mwamuzi huyo Mganda kwamba aliiuma Stars kupita kiasi na kusababisha kutolewa. Tena mwamuzi wa pembeni ndiye amekuwa akituhumiwa zaidi.

Katika hali ya kawaida kuwalaumu waamuzi hao ni kupoteza muda, tena bila sababu za msingi. Waamuzi hao Waganda hawakuwepo wakati Taifa Stars chini Marcio Maximo ikishindwa kuifunga Msumbiji nyumbani Dar es Salaam na baadaye kwao Maputo.

Waamuzi hao hawakuwepo wakati Taifa Stars ya Kim Poulsen ilipong’olewa na Msumbiji baada ya sare Dar es Salaam na Maputo. Mikwaju ya penalti ikatumika, pamoja na Juma Kaseja kuokoa mara mbili, Stars ikang’olewa!

Mara zote mbili, waamuzi hao wa Uganda hawakuwepo. Hivyo kuwafanya wao ndiyo hoja ya Stars kufeli ni kupoteza muda. Ndiyo maana lile la machozi ya Kapombe, waamuzi hao naona si suala la msingi kujadili kwa sasa.

Mwisho wa Watanzania kusema “ilibaki kidogo tu” utakuwa ni lini? Hakika ni kitu kinachokera na huu ndiyo wakati wa kufanya maamuzi magumu. Nani anawajibika?

TFF ilifanya maandalizi kuanzia Tukuyu, Dar es Salaam, Afrika Kusini na mwisho ikapaa hadi Msumbiji. Kitaalamu kuna cha kujifunza, kwamba mazoezi hayo yalikuwa na tija au ndiyo yaliwachosha wachezaji!

Tuangalie mambo yaliyofanyika kisiasa zaidi kwa TFF kutaka kujivua gamba la aibu ya kufanya vibaya kama ikitokea timu ikatolewa. Kwamba inaonekana imefanya mazoezi sehemu nyingi lakini mwisho hayakuwa na msaada!

Je, kocha Mart Nooij anasemaje kuhusu wachezaji wetu, vipi kuhusu uwezo wake na huu ndiyo uwe mwisho wake au tuendelee naye? Wachezaji tulionao, wote wanastahili kuichezea Stars au ni kikosi kinachoitwa kwa kufuata mazoea?

Kama ni kikosi kinachoitwa kwa kufuata mazoea, vipi tunaoneana haya? Au kwa kuwa wachezaji ni rafiki na ndugu zetu tunaona haya kuwaambia ukweli? Haya ndiyo mambo ya kujadili sasa na si nani amelia au kujigaragaza uwanjani!

Kama ni mjadala uanze sasa na nini cha kufanyia kazi kwa kuwa visingizio pumba kama hivyo vya mwamuzi Mganda na mwenzake haviwezi kuwa msaada kwetu hata kidogo. Badala yake tutaendelea kujiangusha zaidi.

Nani tunamuweza, Tanzania inaweza kushinda au kufanya vizuri zaidi mbele ya nani kama Msumbiji wamekuwa wakifanya wanachotaka kila wanapokutana na sisi? Wakisikia wanakutana na Tanzania, wanajua kutakuwa na ugumu lakini kusonga mbele ni uhakika kwao!

Mjadala ndiyo umeanza sasa, lakini vizuri twende kwenye pointi za msingi na tuondoe ushabiki wa Yanga na Simba, upinzani wa nani anamtaka au hamtaki nani TFF. Badala yake tuangalie utaifa kwa kuwa sisi ni Watanzania, timu yetu inapoharibu, hatuwezi kubadili utaifa tukashangilie kwingine.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic