August 13, 2014



Na Saleh Ally
UMESIKIA taarifa za England kuhusiana na mauzo ya jezi? Mshambuliaji nyota wa Manchester United ndiye aliyemaliza msimu akiongoza kwa mauzo.
Jezi yake namba 20, ndiyo iliyouzwa zaidi kuliko nyingine ikiwa ni msimu mmoja tu baada ya kujiunga na Mashetani Wekundu akitokea Arsenal.
Mholanzi huyo amempiku mkongwe Steven Gerrard, nahodha wa Liverpool na kipenzi cha Waingereza wengi. Gerrard amepaa katika mauzo ya jezi kutokana na mwendo mzuri wa Liverpool katika msimu huo uliopita.
Baada ya Gerrard, fowadi Luis Suarez ameshika nafasi ya tatu akiwa na jezi namba 7 ya Liverpool, sasa ameiacha na kutua Barcelona.

Nafasi ya nne imekwenda kwa Eden Hazard wa Chelsea, halafu tano bora ikafungwa na Mesut Ozil aliyekuwa ametua Arsenal akitokea kwa vigogo, Real Madrid.
Wengine wanaofunga 10 bora ya jezi zinazouzwa zaidi katika Ligi Kuu England msimu uliopita ni Wayne Rooney (Manchester United), Sergio Aguero (Manchester City), Juan Mata (Manchester United), Shinji Kagawa (Manchester United) na Frank Lampard (Chelsea).
Hiyo ni 10 bora ya England, jiulize ya Tanzania Bara iko wapi, si rahisi kuwa na jibu wala kupata takwimu kwa kuwa klabu kubwa na zile maarufu za Tanzania wala hazijihusishi na biashara ya kuuza jezi.
Si kwamba haziamini hiyo ni biashara, lakini uvivu na kuridhika na viingilio vya milangoni na fedha kidogo za wadhamini, kwao inatosha.
Ukiangalia katika 10 bora ya England, utaona biashara imekuwa kubwa zaidi kwa wachezaji wanaosajiliwa kutoka klabu moja kwenda nyingine na wale wakongwe wanaokubalika sana kama Gerrard na Lampard, mauzo ya jezi zao yanaendelea kuwa juu.
Pia inategemea aina ya timu, kwani Fernando Torres alikaa kileleni kwa misimu mitatu mfululizo, wakati huo akiwa Liverpool, lakini baada ya kutua Chelsea, taratibu ameporomoka hadi kuondoka kabisa 10 bora.
Hapa nyumbani, Yanga na Simba ndiyo walikuwa na nafasi kubwa ya kufanya biashara kwa kutumia jezi za wachezaji fulani, halafu Mbeya City, Azam FC, Mtibwa Sugar na nyingine zingefuatia.
Angalia wakati wa usajili wa Emmanuel Okwi, Yanga wangeuza jezi kiasi gani na wangeingiza fedha kiasi kipi?
Hiyo haitoshi, usajili kwa ajili ya msimu ujao, Jaja, Coutinho, lazima wangeiingizia Yanga fedha nyingi kama ilivyo kwa Simba na Paul Kiongera, Pierre Kwizera, Amissi Tambwe na wengine.

Vipi sasa klabu hizo hazina hesabu ya kutengeneza fedha wakati kuna soko? Angalia Barcelona baada ya kukubaliana tu na Suarez, jezi zikaingia sokoni, mamilioni yakapatikana.
Klabu za Yanga, Simba na nyingine hazina wabunifu, watu hawaelewi au wavivu wa kazi. Basi wana kila sababu ya kujifunza, wakishindwa waombe ushauri.
10 YA JEZI ZINAZOUZA SANA ENGLAND:

1. Robin van Persie

2. Steven Gerrard

3. Luis Suarez

4. Eden Hazard

5. Mesut Ozil

6. Wayne Rooney

7. Sergio Aguero

8. Juan Mata

9. Shinji Kagawa

10. Frank Lampard





10 BORA BONGO KAMA WANGEKUWA MAKINI:

1.     Coutinho

2.     Paul Kiongera

3.     Jaja

4.     Amissi Tambwe

5.     Mrisho Ngassa

6.     Shabani Kisiga

7.     Mwagane Yeya

8.     Kipre Tchetche

9.     Pierre Kwizera

10.  John Bocco

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic