August 13, 2014



Na Saleh Ally
SIFA kubwa ya kocha Zdravko Logarusic ni uwezo wa kazi, kila sehemu utakayouliza, kila mmoja alisifia mipango na alivyotaka timu yake icheze.


Sifa hizo, kila ulipouliza au kuona ziliharibiwa na mwenendo mbaya, ukorofi, kukashifu wafanyakazi wenzake na dharau za waziwazi, lakini kuendekeza starehe kupita kiasi.

Simba wanajua, kwamba Loga alikuwa anaendekeza starehe lakini wao wakaamini kuficha maradhi ni kitu chema, mwisho wameumbuka na kifo. Usisahau, “mficha maradhi, kifo humuumbua”.

Tayari kuna tofauti au watu wanaona si sahihi, kwamba kwa nini Loga ameondolewa? Wengi wanahoji kwa nini ameachwa mara baada ya kufungwa mechi ya kirafiki dhidi ya Zesco? Wana haki ya kuhoji kwa kuwa hawajui lolote na hawana muda wa kuchunguza.

Ukweli ni kwamba Loga alikuwa na matatizo mengi na uchunguzi wa gazezi hili umebainisha hilo. Moja, ni kuendekeza starehe na kufikia kusahau hata kazi yake. Mfano wiki moja iliyopita, uongozi ulilazimika kumkalisha na kumsisitiza lazima afike mazoezini badala ya kubaki kwake huku akipikiwa ugali na mwanadada wa Bongo Muvi halafu kazi anamuachia msaidizi wake, Selemani Matola.

Kabla ya hapo, uongozi ulimuweka chini na kumuonya kuhusiana na suala la kutukana wachezaji na baadhi ya wafanyakazi wenzake. Usisahau hata wakati wa uongozi wa Ismail Aden Rage aliitwa na kuwekwa chini.

Kibongo, wapo watu ambao hawafanyi kazi vizuri bila hofu, huenda Loga alifanikiwa kuwasaidia baadhi ya wachezaji ndani ya Simba. Lakini wanadamu tunapishana, wapo wanaotaka kuaminiwa na waachiwe wafanye kazi si kuchungwa au kutukanwa kama watoto.

Loga amekwenda kwa amani, sasa anakuja nchini Patrick Phiri raia wa Zambia, kocha ambaye si mgeni hata kidogo kwa soka hapa nchini na kazi yake inajulikana.

Hakuna anayeweza kusema Loga alikuwa mtu mbaya, mchangamfu, mcheshi lakini mengi alikuwa anakosea anapokuwa kazini, hasa ujeuri, dharau na kutowajali wachezaji wake.

Sifa za Phiri ambaye ni mshambuliaji wa zamani wa Nkana na timu ya taifa ya Zambia ‘Chipolopolo’, ni tofauti na Loga, vigumu kumkosoa akiwa kazini au nje ya kazi. Mtulivu, msikivu, mng’amuzi wa mambo, mbunifu na asiyependa bugudha zisizokuwa na ulazima wowote.

Kabla, ukizungumzia sifa za mafanikio wala si suala la kuhoji kwa maana ya rekodi maana akiwa Tanzania, ametwaa ubingwa wa Tanzania Bara mara mbili (2004-05) na (2009-10), msimu mmoja bila ya kufungwa hata mechi moja. Amebeba ubingwa wa Tusker mwaka 2005. Akiwa na Zambia alibeba makombe ya Cosafa na Cecafa, pia kushiriki Kombe la Mataifa Afrika.

Hili ni deni kwa Rais wa Simba, Evans Aveva ambaye pia si mara yake ya kwanza kufanya kazi na Phiri ambaye hata ujio wake umechangiwa na heshima aliyonayo kwa rais huyo wa Simba.

Phiri aliyewahi kuipeleka timu ya taifa ya vijana ya Zambia katika Kombe la Dunia mwaka 1997 nchini Nigeria, anakuwa deni kwa Aveva kwa kuwa ni kocha mwenye msimamo na anayetaka mambo yaende kwa mpangilio na si kubabaisha.

Iwapo Simba itafanya mambo kwa kubahatisha, basi ijue itamkosa mara moja, maana yake Aveva na uongozi wake, wana deni la kuhakikisha mambo yake yanakwenda kwa mpangilio wa juu.

Kikubwa cha kukumbuka, Phiri naye ni bindamu, ana upungufu wake katika sehemu kadhaa na huenda linapaswa kukumbukwa.

Upole:
Kweli ni mkimya sana, ingawa ni maumbile, lakini amekuwa hapendi kusema au kufoka mambo yake yanapoharibiwa.
Ameifundisha Simba kwa vipindi vitatu tofauti, safari hii anarejea ni mara ya nne. Mara mbili aliondoka kimyakimya baada ya uongozi kumkorofisha.

Huenda angeweza kutatua tatizo kwa kusema kinachomkwaza, yeye hakufanya hivyo. Hilo ni tatizo na Simba wawe makini kabla hajaondoka tena kimyakimya, maana yake, hasubiri kufukuzwa.

Kurudi nyumbani:

Amewahi kusema kwao ni kama chifu, hivyo matatizo mengi ya familia yanamhusu. Ndiyo maana haishi kurudi nyumbani kwenda kuyatatua hata kama timu iko katika kipindi kigumu.

Akirejea nyumbani, kurudi kwake kazini pia kumekuwa mbinde. Kuna wakati Simba walimsubiri kwa mwezi mzima akiahidi kesho, keshokutwa, wiki ijayo lakini hakurejea.

Hilo pia ni vizuri akapewa taarifa kwamba halifai na sasa mambo yamebadilika, hivyo kwa kuwa kazi anaiweza na hakuna ubishi ni kocha wa kiwango cha juu, basi aipige bila ya konakona. Karibu tena Bongo ‘Fundi’ Patrick Phiri.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic