September 29, 2014


Na Saleh Ally
IKIWA ndiyo asilimia 15 ya msimu wa Ligi Kuu England imechezwa, tayari kuna mambo mengi sana yamejitokeza ambayo yanaonyesha utakuwa ni msimu wenye kila aina ya mapya yatakayojitokeza.


Tayari mechi 58 zimechezwa kati ya 380 ambazo zinatakiwa kuchezwa kwa msimu mzima wa Premier League kwa 2014-15.
Msimu unaonyesha mabao yaliyofungwa ni mengi, wafungaji waliofunga mabao mengi hadi sasa ni wapya na wachache sana waliofanya vizuri msimu uliopita.

Lakini idadi ya mabao yaliyofungwa na mchezaji mmojammoja pia iko juu, hali inayoashiria ushindani na utamu zaidi wa mabao kupachikwa kwa wingi kwenye msimu.

Mshambuliaji Diego Costa wa Chelsea ndiye anaonekana kuwa matata zaidi katika upachikaji mabao baada ya kufunga nane katika mechi sita za Premier League ambayo ilionekana ni ngumu kwake kwa kuwa anatokea La Liga.

Maana yake kwa asilimia, Costa amepanda juu ya 100% kiufungaji na suala hapa linaloangaliwa ni kama ataweza kuendelea na kasi hiyo au baadaye mabeki watamtuliza.

Wageni:
Baada ya mechi sita, chati ya wanaoongoza kwa kupachika mabao inashikiliwa na wageni zaidi ambao wanaongozwa na Costa mwenye mabao hayo nane.

Unaweza kusema wageni wameiteka ‘nchi’. Hadi sasa inaonekana wengi wao si wale waliofanya vizuri msimu uliopita au hawakuwepo England.

Jose Ulloa wa Leicester ana matano, Graziano Pelle wa Southampton ana manne sawa na Nacer Chadli wa Tottenham na Sergio Aguero (Man City).

Hii inaonyesha hadi sasa wageni ndiyo wanashika chati ya juu zaidi ya wafungaji bora huku wale wakali kama Wayne Rooney na Robin van Persie wakiwa wanachechemea lakini hawako mbali kwa kuwa mmoja ana mabao mawili na mwingine matatu.          

Wastani:
Tayari mabao 164 yalikuwa yamefungwa kabla ya mechi za jana Jumapili na leo. Hadi sasa wastani wa idadi ya mabao uko juu sana, kwani unaonyesha kuna asilimia 2.83. Kimahesabu ni hivi, katika kila mechi iliyochezwa, tayari wastani wake ni mabao matatu.

Kama ni mabao matatu kwa kila mechi na mechi kawaida hupigwa ni 380, kuna uwezekano wa kufungwa mabao 1,140, lakini kwa kawaida lazima yatapungua, kwa hali inavyokwenda, inaonekana hayatashuka chini ya 1000.

Penalti:
Inaonekana hadi mechi sita kwa kila timu zimechezwa na idadi ya penalti si nyingi sana kwani ni asilimia 4.3, idadi ambayo ni ya chini.

Idadi ndogo ya mabao ya penalti na idadi kubwa ya mabao ya kufunga inaonyesha kiasi gani uwezo wa kufunga mabao bila aina hiyo ya adhabu uko juu.


Mwisho:
Ukitaka kujua ligi bado ni ngumu, angalia namna mabao yanayofungwa katika dakika za mwisho. Kwamba kila upande unakuwa haukubali hadi hatua za mwisho.

Tangu kuanzishwa kwa ligi hiyo inaonekana kuna wastani mkubwa wa mabao yaliyofungwa baada ya dakika 80. Hadi sasa katika mechi hizo chache, inaonyesha kuna wastani wa mabao asilimia 16 yamefungwa dakika 10 za mwisho.

Nyumbani & ugenini:
Idadi ya mabao kuwa juu pia imeongeza ugumu katika mechi za nyumbani na ugenini. Inaonekana ushindi wa mechi za nyumbani wastani wake ni 31%, ushindi wa ugenini ni 33% na sare ni 36%.

Hii inakuonyesha ligi hiyo haina mwenyewe kwa kuwa ushindi wa ugenini unaonekana uko juu kuliko nyumbani. Maana yake timu zimepoteza mfululizo nyumbani na hii inathibitisha ugumu wa ligi hiyo.

Hata hivyo, unaweza kusema ni mapema kwa kuwa ligi inaweza kuwa na mabadiliko kutokana na makocha, makipa, mabeki, viungo na washambuliaji wanavyobadilika na kutokana na makosa wanayoyafanya.

Inawezekana washambuliaji wakafunga mabao mengi zaidi au mabeki wakawa imara na kupunguza idadi ya mabao yanayofungwa wakishirikiana na makipa na viungo wakabaji.

Raha ya ligi hiyo ni kuendelea kuangalia, lakini wiki hizo sita, tayari zimeonyesha kuwa kuna harufu ya ushindani wa juu zaidi kuliko misimu mingine iliyopita.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic