October 3, 2014



SIMBA imeanza Ligi Kuu kwa kutoka sare mechi zake zote mbili ilizocheza nyumbani kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Hali ambayo inaonekana kuwaudhi sana mashabiki na wanachama wa klabu hiyo.


Sare ya kwanza ya mabao 2-2 dhidi ya Wagosi wa Kaya, Coastal Union ambao walisawazisha mabao mawili wakati Simba ilitangulia kufunga mawili hadi mapumziko. Sare ya pili dhidi ya Polisi Moro.

Simba ilianza kufunga bao, ikaongoza hadi mapumziko lakini kipindi cha pili, Polisi Moro wakasawazisha kupitia Danny Mrwanda na kufanya matokeo ya mwisho kuwa bao 1-1.

Hizo ndiyo hasira za baadhi ya Wanasimba ambao wameonyesha wazi hasira zao kuhusiana na timu yao kushindwa kufanya vizuri. Kimahesabu hasi sasa Simba imepoteza pointi nne nyumbani.

Kila mechi imeacha pointi mbili zikipotelea hewani na sasa ina kazi nyingine ngumu mbele yake Jumamosi, itakapokuwa na kazi ngumu ya kupamabana na Stand United ambayo ilianza kwa kufungwa nyumbani, halafu ikashinda ugenini.

Sare mbili za Simba zimeanza kuonekana kama ni jambo kubwa sana, lakini sasa limeingia sehemu nyingine ambayo ninaweza kusema si sahihi.

Kwa kuwa kuna watu leo wanaamini eti kutofanya vizuri kwa kikosi hicho chini ya Patrick Phiri ni kutokana na kutokuwa na maelewano mazuri na mashabiki na wanachama wengine wanaojulikana kama Simba Ukawa.

Awali nilidhani ni jambo la utani wa kimpira, lakini kadiri siku zinavyosonga mbele limekuwa likizidi kuchukua nafasi na ikiwezekana kuanza kuwashawishi baadhi ya watu kwamba hao Simba Ukawa ndiyo wanaoifanya Simba isifanye vizuri.

Wako sasa wanaamini ambao nimewasikia wakizungumza hivyo huku nikiwatazama na wengine nikawasikia wakihojiwa kwenye redio. Baada ya hapo, kuna baadhi ya mashabiki wameanza kuushauri uongozi wa Simba kufanya suluhu na wanachama hao wa Simba Ukawa.

Suala la suluhu ni jambo jema kwa ajili ya kuongeza umoja ndani ya Simba maana umoja ni nguvu na hii ni kati ya misemo ya utambulisho wa Simba. Kushirikiana ni jambo jema na msaada mkubwa kwa kundi la watu linalotaka kufanya jambo moja kwa pamoja.

Lakini si kuweka hisia za kusema Simba ukawa ndiyo chanzo cha Simba kutofanya vizuri. Hii itakuwa ni sehemu ya kuonyesha kiasi gani bado watu wapo katika karne ya 21 wanaendelea kuishi na mawazo ya enzi za karne za mawe.

Mawazo potofu, mawazo yasiyo na mwendo, hisia zisizo sahihi, hisia pungufu zilizokuwa na mashiko na hazipaswi kupewa nafasi katika kipindi chetu hiki, la sivyo tutaruhusu kuwa na watu ‘old model’ kwenye maisha ya sasa!

Watu kama hao ni wale wanaoamini ushirikina ndiyo unaocheza ni kosa kubwa, kuwapa watu nafasi waamini wanachosema ni kweli ni kosa jingine kwa kuwa ni kuendelea kuidanganya jamii iishi na imani za zama za mawe.

Si sahihi hata kidogo kuamini soka leo linaendeshwa na ushirikina na kwamba timu haiwezi kufanya vizuri bila ya kuwa na mganga bora wa kienyeji. Hapa ndiyo tumekuwa tukikwama, najua ni mradi watu fulani, lakini vizuri kupima mnachofanya.

Msisitizo wangu, Simba inashindwa kufanya vizuri kiufundi uwanjani. Ninamaanisha kukosa mabao, mabeki wao kutokuwa makini, kiungo kupoteza ushirikiano katika kipindi cha pili ukilinganisha na wanavyoanza kipindi cha kwanza.

Kocha Mkuu Patrick Phiri amesema wanayafanyia kazi mambo hayo, wapeni nafasi na vizuri mambo hayo yashughulikiwe kwa kufuata utaratibu badala ya papara au kutaka kuonyeshana, mwisho mtajichanganya zaidi na kuanza kupokea vichapo na si sare tena.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic