November 8, 2014


Na Saleh Ally
LIGI KUU England huwezi ukaiamua kwa mechi moja hasa kama si mechi za mwisho za msimu. Utamu wake umegawanyika na hilo linathibitika kila mwisho wa wiki zinapochezwa mechi za Premier League.


Ndiyo ligi inayotazamwa na mashabiki wengi zaidi. Leo, kesho na keshokutwa utaona shughuli na namna mechi zitakavyokuwa na upinzani. Usitazame mechi ya Liverpool dhidi ya Chelsea pekee, kwa kuwa kuna mengi yatatokea.

Kila mechi ya Premier League inapochezwa, huacha gumzo kwa wiki au mwezi mzima kwa kuwa huwa hazikaukiwi vituko.

Katika mechi za wikiendi hii, kuna mambo mengi sana utayaona kutokana na kila timu inavyotaka kufanya lakini yote yanayokea, lengo likiwa ni kufanya vizuri.

Anfield yenye hofu:
Chelsea imesafiri hadi Anfield, Liverpool kucheza na wenyeji. Kumbuka haijafungwa hata mechi moja na ndiyo inaonekana ni ‘Top Team’ katika Premier League.

Tatizo moja Liverpool imekuwa na mwendo wa kusua, wanajua ilivyo kazi kuwazuia wakali kama Chelsea. Na kazi kubwa itakuwa ni kuwazuia wasifunge mapema ili kuendana na kauli ya msimu uliopita ya mshambuliaji wao wa zamani Luis Suarez aliyesema: “Raha ni kuitangulia Chelsea, ukiacha wakufunge kwanza, ujue umekwisha kwa kuwa kusawazisha dhidi yao ni karibu kabisa na kusema ni jambo lisilowezekana.”

Licha ya kuwa nyumbani, utawaona Liverpool wakijilinda sana na kufanya mashambulizi ya kushitukiza. Lakini inawezekana kabisa ukawaona watu usiowategemea kama Mario Balotelii na Didier Drogba waking’ara kwa kuwa wana uzoefu na mechi kubwa.

Arsenal na marekebisho:
Arsenal wapo ugenini dhidi ya Swansea, timu ambayo iliweka rekodi kwa misimu miwili sasa na kuchukua ile sifa ya Arsenal ya kumiliki mpira kuliko timu nyingine.

Safari hii Arsenal inakwenda ikiwa na timu nyingine ambayo ni tofauti na ile iliyokuwa ikiongozwa na Arsene Wenger, si yule aliyekuwa akipewa sifa ya ubahili.

Unaweza kusema Arsenal imekamilika kwa kuwa ina wachezaji wapya wazoefu na itaingia kuivaa Swansea ikiwa inataka kurekebisha makosa ya kutoka sare ya bao 3-3 katika mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Anderlecht ya Ubelgiji baada ya kuwa imetangulia kwa mabao 3-0, tena ikiwa nyumbani.

Licha ya kumuwekea ulinzi mkali Wilfried Bonny kutoka Ivory Coast, utakachokiona, pamoja na kikosi cha Arsenal kuonekana kiko imara, watafanya kazi ya ziada kuwazuia Swansea kumiliki mpira na watajaribu kuwafunga mapema ili kuwachanganya. Wakichelewa kupata bao la mapema, watakiona.

Ubabe wa Everton ugenini:
Everton haiko katika kiwango kizuri kama msimu uliopita ambao ulikuwa wa kwanza kwa kocha wake, Roberto Martínez ambaye alijiunga na timu hiyo akitokea Wigan Athletics ambayo iliteremka daraja.

Presha kwa kocha huyo iko juu licha ya kwamba hata kama atafanya vibaya katika mechi dhidi ya Sunderland, kesho ugenini, lakini ishu ni kupata nafasi za juu ili ashiriki tena michuano ya Ulaya.
Utaona mechi ya kasi iliyojaa ubabe kwa kuwa Sunderland wanajua Everton wana kasi lakini kocha wao, Gus Poyet lazima atakuwa amesisitiza Paka Weusi lazima waibuke na ushindi maana mwendo wao ni mbaya zaidi ya bibi kizee mwenye mkongojo.

Ngumu sana:
West Brom wakati wanawakaribisha nyumbani Newcastle, hii itakuwa kati ya mechi ngumu zaidi kwa wikiendi hii.

Kila timu ina pointi 13, Newcastle ndiyo wameamka lakini West Brom chini ya Alan Irvine aliyewahi kuwa msaidizi wa David Moyes kwa vipindi viwili tofauti, imekaa vizuri na utaona mtu kama Saido Berahino mwenye asili ya Burundi amekuwa moto.

Kila moja itataka kushinda na utaona mashambulizi mengi zaidi kwa maana ya takwimu na inawezekana kuwa na sare au kipigo kutoka upande wowote ule.

Hisia za uadui:
QPR inawakaribisha mabingwa Manchester City kwenye uwanja wa wake wa Loftus Road, ambao waliuachia majonzi katika msimu wa 2011/2012.

Sergio Aguero alifunga bao la dakika za nyongeza na City ikabeba ubingwa na kuwaacha Manchester United wakiwa wamezubaa.

QPR waligeuzwa ngazi ya ubingwa, mechi yao dhidi ya City itakuwa ngumu kwa kuwa watataka kuwaonyesha kuwa wao si wale wa kipindi kile, lakini usisahau kuwa hawana mwendo mzuri chini ya kocha wao mkongwe, Harry Redknapp.

Hivyo ni mechi ya kuonyeshana nani zaidi, pia ni mechi ya kila mmoja kutaka kurejea katika hali nzuri kwa kuwa hata Man City, wameingia kwenye kundi la wanaosuasua.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic