December 5, 2014


Kiungo mshambuliaji wa Yanga, Simon Msuva, ameendelea kuonyesha kuwa anaweza kuendelea kuwa hatari kwenye kikosi cha Yanga baada ya kuonyesha uwezo katika mazoezi ya timu hiyo.


Msuva ambaye amekuwa gumzo katika mechi za hivi karibuni, alikuwa nyota wa mechi ya mazoezini ya Yanga dhidi ya Abajalo FC, juzi Jumatano kwenye Uwanja wa Shule ya Sekondari Loyola jijini Dar.

Winga huyo alifunga mabao mawili na kuisawazishia timu yake ambayo ilikuwa nyuma kwa 2-0 dhidi ya wapinzani wao hao ambao wanashiriki michezo ya Ligi Daraja la Pili Taifa.

Katika mchezo huo uliochezwa huku kukiwa na manyunyu ya hapa na pale, Msuva alionyesha uwezo mkubwa wa ‘kulijua lango’ ambapo alifunga bao safi kwa kuwakusanya mabeki wa timu pinzani.

Kama hiyo haitoshi, baadaye Msuva alionyesha kuwa hakubahatisha kwa kufunga bao lingine kwa kichwa akiwa karibu na lango, akiitendea haki krosi iliyochongwa na mshambuliaji wa timu hiyo, Jerryson Tegete ambaye naye alifunga bao moja katika mchezo huo uliomalizika kwa sare ya mabao 3-3.

Hata hivyo, Abajalo ambayo haikupewa nafasi kubwa ya ‘kufurukuta’ kabla ya mchezo huo, ilionyesha soka safi hasa kipindi cha pili huku Yanga iliyokuwa chini ya nahodha wao, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ ikiwapa nafasi ‘madogo’ hao kucheza wanavyotaka.


Mabao ya timu hiyo yenye maskani yake Sinza jijini Dar, yaliwekwa wavuni na Bakari Mwinjuma aliyefunga mawili, huku Yusuph Kinamuhama akifunga moja.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic