December 6, 2014


Na Saleh Ally
MICHUANO ya Kombe la Mataifa Afrika (Afcon), inaanza kutimua vumbi Januari 17 hadi Februari 8, mwakani.


Gumzo lake lilipunguzwa kasi baada ya waliotakiwa kuwa wenyeji, Morocco kujitoa katika hatua za mwisho wakieleza kuhofia suala la ugonjwa hatari wa Ebola.

Sasa mzigo umesogezwa Equatorial Guinea ambayo mwaka 2012 kwa kushirikiana na jirani zao Gabon iliandaa michuano hiyo na wenyeji wote wakafanikiwa kutinga robo fainali.



Kuna makundi manne katika michuano hiyo, kila moja likiwa na timu nne. Kinachoumiza ni kwamba hakuna hata timu moja kutoka ukanda wa Afrika Mashariki!

Kusini wana Zambia na Afrika Kusini, Kati wana DR Congo na Congo BR. zilizobaki ni timu za Kaskazini na Magharibi ambazo unaweza kusema ni michuano yao.

Ugumu wa hatua ya makundi katika michuano hiyo, umefanya ule msisimko urudi tena, kwani timu kama Nigeria ambao walikuwa mabingwa watetezi, wametolewa kwenye hatua za kufuzu.

Maana yake, mwali hana mwenyewe na timu zote 16 zitakazoenda Equatorial Guinea zitakuwa sawa na hakuna cha kuangalia mkongwe au ubora kwa majina.

Lazima mpira upigwe, kama ingekuwa ukongwe, Nigeria ingefuzu. Lakini umeona timu kama Afrika Kusini ambayo hadi mwisho wa mechi za hatua ya kufuzu, haikupoteza hata moja na ndiyo iliyoibania Nigeria, haikusonga!

Cape Verde imerejea, Ivory Coast imerudishwa kundi moja tena na Cameroon ambao walikuwa kundi moja kuwania kufuzu. Maana yake Kundi D litawaka moto.

Lakini Kundi C ndilo hatari zaidi unapoziona Algeria, Senegal, Ghana na Afrika Kusini zikiwa pamoja. Zote zimewahi kushiriki Kombe la Dunia.

Lakini ubishi wa Afrika Kusini na Senegal, ubora wa Ghana na Algeria na zinatakiwa timu mbili tu, haitakuwa kazi ndogo.

Kwa kifupi itakuwa michuano migumu itakayovutia na vigumu sana kutabiri nani atakuwa bingwa licha ya kwamba kuna timu zenye uzoefu mkubwa kama Cameroon, Ivory Coast, Ghana, Algeria na Senegal.





KUNDI A: 
Equatorial Guinea, Gabon, Congo BR na Burkina Faso

KUNDI B:
Zambia, DR Congo, Cape Verde na Tunisia


KUNDI C:
Algeria, Senegal, Ghana na Afrika Kusini

KUNDI D:
Ivory Coast, Guinea, Cameroon na Mali



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic