December 15, 2014


Na Saleh Ally
ILE Simba ya Patrick Phiri unayoijua, inaonekana imekaribia kurejea na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Yanga unawaonyesha Simba kwamba wanastahili kuvuta subira.


Phiri amerejea Simba wakiwa wamepita zaidi ya makocha wanne baada ya kuondoka nchini na kuiacha timu hiyo.

Lakini kuna mabadiliko ya mambo mengi, ukiacha makocha, hata wachezaji na viongozi, wamepita wengi tofauti, hivyo mambo mengi yamebadilika.

Katika mechi ya kirafiki, juzi Simba ilishinda kikombe cha Mtani Jembe kwa kuichapa Yanga kwa mabao 2-0.
Phiri anaendelea kuwa na rekodi ya kuinyanyasa Yanga kwa kuwa amepoteza mara moja tu dhidi ya Yanga katika mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Aliyefunga bao pekee siku hiyo alikuwa Jerry Tegete, Yanga ikiwa chini ya kocha Kosta Papic iliutafuta mpira vibaya, lakini ikafanikiwa kuibuka na ushindi.

Ukiachana na ushindi huo, zaidi Phiri amekuwa akipata sare au ushindi lakini kikubwa alichoonyesha na kuthibitisha juzi ni kwamba yeye ni maestro tactician, yaani mwalimu hodari na hasa katika mechi kubwa zinazohusisha Simba dhidi ya Yanga. Kimahesabu, Phiri alimfunika kabisa Maximo.


Uchezaji:
Angalau sasa unaweza kusema Simba inakwenda kwenye uchezaji wa ‘Kiphiri’, pasi fupifupi lakini haraka.

Simba inaweza kubadili uwanja, mpira kutoka kushoto kwenda kulia hata mara nne ndani ya dakika moja. Kitaalamu wanasema “kuuondoa mpira kwenye matatizo.”
Lakini Simba ndiyo timu iliyocheza pasi nyingi za kupenyeza, mojawapo ilisababisha faulo baada ya Emmanuel Okwi kupenyezewa, akamtoka Juma Abdul aliyelazimika kumkwatua. Yanga ilionekana ni juhudi binafsi za wachezaji, si timu iliyounganishwa.

Katika kipindi cha kwanza, Simba walipiga zaidi ya pasi 12 za kupenyeza (penetration passes) na Jonas Mkude akionekana kuongoza kitengo hicho.

Angalia mabeki wote wawili wa pembeni, Nassor Said ‘Chollo’ na Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ walipata nafasi ya kupiga krosi kwa kuwa viungo walifinya ndani na kuwapa nafasi ya kupita. Wakati wachezaji wa Yanga, Oscar Joshua na Juma Abdul, walilazimika kubaki nyuma muda mwingi na hakukuwa na nafasi ya kusaidia mashambulizi.
Sub:
Mabadiliko yote aliyofanya Phiri, yalionyesha kuwa na msaada mkubwa ukilinganisha na yale ya Maximo.

Mwanzoni tu mwa kipindi cha pili, Phiri alimtoa Juku Musheed na kumuingiza Joseph Owino baada ya kuona kuwa Mliberia Kpah Sherman anawasumbua sana mabeki wake kwa kuwa alionekana kwenye uzoefu na nguvu nyingi.

Dakika ya 65, Simba ilimtoa Tshabalala baada ya kuumia akaingia Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, hii huwezi kusifia.

Wengine waliotoka ni Ramadhani Singano ‘Messi’ na kumuingiza Said Ndemla katika dakika ya 72, halafu Maguli akaenda nje dakika ya 84, akaingia Danny Sserunkuma.

Wakati mabadiliko hayo yanafanyika, tayari Phiri alibadili mfumo kutoka 4-4-2 aliyoitumia zaidi kipindi cha kwanza na kwenda 4-5-1. Hapa akawa analinda zaidi, hivyo Ndemla atasaidia katikati na Sserunkuma kubaki na mpira.

Wakati huo, Maximo ndiyo alikuwa anaamka na kumuingiza Hussein Javu na Mrisho Ngassa baada ya kuumia katika dakika ya 63. Usisahau alimuingiza Salum Telela katika dakika ya 56 kuchukua nafasi ya Mbrazil, Emerson Roque ambaye hakupaswa kurudi kipindi cha pili.
Phiri alimaliza mchezo kwa kumuingiza Shabani Kisiga katika dakika ya 86 akimtoa Simon Sserunkuma.

Maximo alichelewa kubadili mambo, hali inayoonyesha Phiri ni mwepesi kujua nini cha kufanya.

Amekutana na Maximo mara tatu, mara ya kwanza wakiwa na timu za taifa za Zambia na Tanzania, ikawa sare ya bila mabao kama sare ya pili katika mechi ya Ligi Kuu Bara msimu huu. Sasa amemmaliza.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic