December 17, 2014




Na Saleh Ally
MECHI ya kirafiki kati ya Yanga dhidi ya Simba, maarufu kama Nani Mtani Jembe, imepita lakini imeacha makovu lukuki.


Kama ilivyo kawaida, Yanga na Simba zinapokutana, anayepoteza basi habaki na amani. Utaona msimu uliopita, Yanga walifungwa 3-1, wakamfukuza Ernie Brandts.

Msimu huu wamefungwa tena mabao 2-0, Kocha Marcio Maximo, kiungo Emerson Roque safari imewakuta, wanarejea kwao Brazil.

Haya ni baadhi ya madhara ambayo timu zinakutana nayo kila zinapocheza mechi hiyo ya watani na safari hii inajulikana kama Nani Mtani Jembe.

Nani Mtani Jembe ni mechi inayoandaliwa na wadhamini wa klabu hizo mbili, Yanga na Simba. Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia kinywaji chake cha Kilimanjaro.

Kwangu naona wadhamini hao wamekuwa wakifaidika kupita kiasi na kuzinyonya klabu hizo kupitia timu zao zinapocheza mchezo wa Nani Mtani Jembe, nisisitize si sahihi, nitaeleza.

Katika mechi ya Jumamosi iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar, Simba walipata Sh milioni 15 za ushindi, Yanga waliopoteza wakapewa Sh milioni 5. Kabla ya mechi kila timu hupewa Sh milioni 30 za maandalizi.

Kulikuwa na fedha Sh milioni 100, hizi zinatokana na kura zinazopigwa na mashabiki. Simba wakashinda na kupata Sh 77, 590,000, Yanga wakashindwa na kupata Sh 2,410,000.

Ukichukua jumla, Simba ilipata Sh milioni 122.6 wakati Yanga iliambulia Sh milioni 37.4. Hapa ndiyo kwenye hoja yangu ya msingi, kwamba wanaofaidika zaidi ni wadhamini Kilimanjaro, kitu ambacho si sahihi, nafafanua.

Wadhamini hao wanafaidika zaidi ya maradufu kwa kuwa ndiyo wanaochukua mapato ya mechi, jiulize kwa nini iwe hivyo?

Umewahi kusikia wapi, eti Chevloret wa Manchester, Emirates wa Real Madrid, Arsenal au T Mobile wa Bayern Munich anakwenda kuchukua mapato ya mechi?

Jiulize, mapato ya mechi ile kama ni chini kabisa, basi itakuwa ni Sh milioni 500. Sasa Kilimanjaro walitoa Sh 190 kwa Yanga na Simba. Zote zinazobaki zinakwenda wapi?

Tena naweza kusema hivi, hata ile Sh milioni 100 waliogawana Yanga na Simba, hawakupewa na Kilimanjaro kwa kuwa ni fedha inayotokana na wanachama wa Yanga na Simba kwa kuwa walikuwa wakituma SMS kupitia namba maalum na wanakatwa kwenye fedha zao.

Hivyo kama utaitoa fedha hiyo ya upigaji kura kupitia SMS ambayo ni Sh milioni 100. Maana yake, Kilimanjaro ilitoa Sh milioni 80 pekee kwa klabu hizo kongwe, zenye jina kubwa lakini zinakubali kunyonywa fedha zao kirahisi na hakuna anayeamka.

Kwa mantiki hiyo ni hivi; ile Sh milioni 100 waliyogawana ilitolewa na mashabiki na wanachama wa klabu hizo kwa kukatwa kupitia SMS.

Sh milioni 20 ambayo waligawana, Simba Sh milioni 15 na Yanga Sh milioni 5 pamoja na Sh milioni 60 iliyogawanywa kwa ajili ya maandalizi, ndiyo fedha pekee walizotoa wadhamini hao.

Sasa jiulize kitu kimoja, wadhamini hao matangazo yao waliyojaza uwanjani, promosheni rundo na nguvu ya Simba kuwaletea watu zaidi ya 60,000 inalipwaje?

Utasema Simba wanadhaminiwa na Kilimanjaro, sawa. Si unajua vifua vya wachezaji Simba na Yanga ni ghali, ikiwezekana TBL wanaweza wakawa wanalipa kidogo.

Hilo linaweza lisiwe jambo la kuzifanya Yanga na Simba ziwe watumwa kwa kukubali kuchukua kiasi kidogo kabisa cha fedha kwa kuwa tu mdhamini ametaka au aliamua hivyo.

Wakati fulani, uongozi wa Yanga uliwahi kuhoji kitita cha Sh milioni 100 kilichokuwa kinatolewa na Azam TV kwamba ni kidogo. Kweli walikuwa na hoja, sasa huu ndiyo wakati wa kuhoji fedha kiduchu za TBL zinavyowatumikisha.

Inawezekana hamkuwa mmeamka, lakini kuna mengi ya kujiuliza, faida na hasara za Mtani Jembe na kama mnachopata ni sahihi.

Mimi nimeamka, hizi ni hoja chache. Nitarudi baada ya siku chache kuzijazia, ili tuchangie, ikiwezekana nitaanzisha mjadala wa wazi, mashabiki na wanachama wa klabu hizo wachangie, ili kuzisaidia kupata fedha zaidi kwa kuwa zinatumia fedha nyingi, ‘zinajiuza’ kama ulivyo msemo wa kibaya chajitembeza. Nitarudi.



2 COMMENTS:

  1. You are great Saleh. Viva forever. Umeongea jambo la msingi ambalo lina ukweli mtupu. Wapo watakochukoa coz utakua umeugusa mrija wao wanaoutumia kunyonya but it z better ulaumiwe lakini sauti ya UKOMBOZI IPAE NA KISIKIKA...Pamoja daima.

    Millanzi P.J

    ReplyDelete
  2. Wakukaya hapa umegusa kwenye mfupa, wengi hawatakuelewa lakini wachache wenye akili zinazochemka wataelewa nini unachomaanisha. TBL wanachokifanya hawakustahili kukifanya, wanaonesha hawana nia ya dhati kuzikomboa Simba na Yanga bali ni kujinufaisha matakwa yao kama wadhamini. Viongozi wa Simba na Yanga huu ndiyo wakati wa kustuka na kufumbua mambo kuona nyuma ya pazia ya mchezo huo kuna nini.

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic