February 16, 2015


Unapozungumzia kikosi cha El Merreikh, hakuna ubishi ni sehemu ya historia ya soka la Bara la Afrika.
El Merreikh ni moja ya klabu kubwa na kongwe katika Bara la Afrika, yenye uzoefu mkubwa na michuano ya kimataifa, tena inayoundwa na wachezaji wenye uzoefu mkubwa.


Makocha wanaoifundisha El Merreikh kama waliyekuja naye, pia ni wa kiwango cha juu kabisa kwa kuwa aliwahi kuipa TP Mazembe ubingwa wa Afrika.

Usisahau El Merreikh wamekuwa wakicheza katika hatua za makundi ya michuano ya Ligi ya Mabingwa, ikiwa na maana kwamba si kikosi cha kung’olewa mapema.

Lakini Azam FC wameonyesha kuna ambalo linawezekana licha ya kwamba wengi waliona haliwezekani. Wameifunga El Merreikh kwa mabao 2-0 katika mechi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa.

Azam FC wameweka rekodi nzuri sana, kwamba mechi yao ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika tena dhidi ya kigogo cha Afrika, wao wamefanikiwa kuibuka na ushindi, si kazi rahisi.

Ushindi wa Azam ni sehemu ya picha kwamba kuna mambo yanawezekana na kujipanga ndiyo jambo la msingi. Tunajua Azam FC wamekuwa wakijipanga kila siku zinavyosonga mbele.

Utakumbuka Azam FC walianza kushiriki michuano ya Kombe la Shirikisho, walifanya hivyo mara mbili kabla ya kutwaa ubingwa kwa mara ya kwanza na kufanikiwa kupata nafasi ya kushiriki Ligi ya Mabingwa kwa mara ya kwanza.

Wakati wanaingia katika Ligi ya Mabingwa Afrika, walikuwa wamejifunza mambo kadhaa kupitia katika Kombe la Shirikisho waliloshiriki mara mbili. Wameanza na rekodi nzuri kwa kushinda dhidi ya vigogo.

Azam FC wameshinda huku wakionyesha soka safi, wakishambulia zaidi na walionyesha ufundi mkubwa katika kujilinda dhidi ya timu hiyo ngumu ya El Merreikh.

Kitu ambacho wanapaswa Azam FC kukikubali kabla ya safari yao ya wiki mbili zijazo kwenda Sudan, bado hawajaimaliza El Merreikh na wanachotakiwa kuamini dakika 90 nyingine ndizo zenye uwezo wa kuwavusha mbele na kuing’oa  timu hiyo ngumu na kongwe  barani Afrika.

Ushindi wa mabao 2-0 uliopatikana Dar es Salaam Azam FC wakiwa wenyeji, unaweza kupatikana Sudan El Merreikh wakiwa wenyeji pia kwa kuwa ni timu yenye uwezo wa kufanya hivyo.

Tuliona uchezaji wao, kwamba licha ya Azam kufanya vizuri sana katika mechi ya jana, lakini kikosi hicho cha Wasudan kilionyesha soka safi linalothibitisha kwamba kweli wana kikosi kizuri.

Kawaida wanacheza taratibu, lakini wanaojiamini na wanaojua wanafanya nini. Watakapokuwa nyumbani kwao lazima kutakuwa na mabadiliko makubwa kiuchezaji.

Lakini uchezaji uwanjani hauwezi kutosha kuifanya Azam FC ipite katika michuano hiyo. Wewe utakataa, mimi nitakuambia kwamba michuano kama hiyo chini ya Caf ina mambo mengi pamoja na fitina nje ya uwanja.

Kamwe sisemi Azam FC wafanye ushirikina, lakini nawakumbusha umakini kabla hawajaingia uwanjani kwa kuwa Wasudan wana sifa ya kupulizia dawa ya kupunguza nguvu kwenye vyumba vya timu pinzani au kwenye lifti.

Taifa Stars wakati inafuzu kucheza kombe la Chan mwaka 2009, nguvu kubwa ya wadau na watu wa TFF ilitumika kuwazuia Wasudan hao kufanya fitina zao mbaya. Wachezaji hawakupanda lifti, wakatumia ngazi.

Safari hii Azam FC watajilipia hoteli kutokana na mabadiliko ya Caf. Lakini bado watakuwa ugenini, hivyo wanapaswa kuwa makini katika masuala ya chakula na wapi watalala.

Halafu baada ya hapo waingie uwanjani na kuhakikisha wanacheza soka kwa umakini mkubwa wakiamini bado wanaweza kufanya vizuri lakini nidhamu ya mchezo waliyoionyesha jana, basi wakiwa Sudan, iwe mara tatu yake. Kila la kheri.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic