Kikosi cha Mtibwa Sugar ya mkoani Morogoro, imecheza
kwa takribani dakika 720 mfululizo, sawa na michezo nane bila ya kuonja ladha
ya ushindi wa aina yoyote kwenye Ligi Kuu Bara msimu huu.
Mtibwa ambayo ilianza vizuri katika ligi hiyo na
kufanikiwa kukaa kileleni kwa muda mrefu, mambo yamebadilika kwani imeshaporomoka
hadi katikati ya msimamo.
Mara ya mwisho timu hiyo kupata ushindi ilikuwa
ni Oktoba 26, mwaka jana katika mchezo dhidi ya Mbeya City walipoifunga mabao
2-0 yaliyowekwa kimiani na Ame Ally na Vincent Barnabas.
Licha ya kutopata ushindi kwa muda mrefu,
Mtibwa pia itakumbuka vipigo vitatu mfululizo ilivyovipata kutoka kwa Ruvu
Shooting (mabao 2-1), Yanga (mabao 2-0) na kile kikubwa cha mabao 5-2 dhidi ya
Azam.
Matokeo ya michezo hiyo nane ilikuwa hivi;
Mtibwa 1-1 Simba, Mtibwa 1-1 Kagera Sugar, Mtibwa 1-1 Stand United, JKT Ruvu 1-1
Mtibwa, Ruvu Shooting 2-1 Mtibwa, Yanga 2-0 Mtibwa, Azam 5-2 Mtibwa na Ndanda
0-0 Mtibwa.
Kocha wa timu hiyo, Mecky Mexime, amesema
kikosi chake kina tatizo la kisaikolojia, ndiyo maana kimekuwa kikipata matokeo
mabaya kwa siku za hivi karibuni.
“Mazoezi tunafanya kama kawaida, tatizo ni
kwamba wachezaji wangu sasa wanasumbuliwa na mambo ya kisaikolojia tu.
Nitahakikisha nawaweka sawa haraka iwezekanavyo,” alisema Maxime.








0 COMMENTS:
Post a Comment