March 30, 2015



Na Saleh Ally
NILISHANGAZWA na taarifa ya mwandishi mmoja wa Kenya kutupia maneno kwenye mtandao akisema mshambuliaji wa Simba, Danny Sserunkuma aliamua kurejea kwao Uganda kwa kuwa viongozi wa Simba wamekuwa wakimlazimisha kutumia ushirikina.


Kauli ya mwandishi huyo ilinifanya niingie kufanya uchunguzi kwa mara nyingine tena kuhakikisha mambo mawili ambayo tayari niliwahi kuyafanyia utafiti wa kawaida kabisa.


Moja, kweli amekuwa akilazimishwa? Pili, Uganda au Kenya, hawafanyi mambo ya kishirikina katika mchezo wa soka kama ilivyo hapa nyumbani?

Mimi ninaweza kuthibitisha kokote kwa Yanga, Simba na klabu nyingine wamekuwa wakifanya mambo ya kishirikina. Hata klabu za daraja la kwanza, la pili, tatu na mechi za mchangani, ushirikina umekuwa ukifanyika.

Ushirikina katika soka ni miradi ya watu au nio kuridhisha imani za wanaoamini ushirikina unafanya kazi katika soka. Ukweli hakuna lolote lonaloweza kusaidiwa na ushirikina. Vipi wasiofanya wanafanikiwa na sisi ni ziro halafu tuamini ushirikina ndiyo uokozi?


Uchunguzi wangu unaonyesha kwanza Kenya na Uganda nao wamekuwa wakiamini mambo hayo ya ushirikina. Raha zaidi niliamua kufanya mahojiano na mmoja wa makocha wa zamani wa Gor Mahia ambayo alikuwa akichezea Sserunkuma, akanithibitishia ni jambo la kawaida kufanya ushirikina na mambo mengi ya kimira kwa kuwa ile ni timu ya kikabila!

Kamwe sitaunga mkono ushirikina, lakini tayari I mradi wa watu fulani wanaoutumia kupata fedha katika soka la Afrika ukizijumlisha Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi na kwingineko. Lakini ukweli, hausaidii lolote kwa mchezaji wala timu na wengine wamekuwa wakikubali kushiriki kama utaratibu tu wa kabla ya mechi, lakini hawaamini.


Baada ya hapo nikarudi kufanya mahojiano na viongozi wa Simba kupata usahihi wa kipi alichokifanya Sserunkuma na kama kweli alitishia kutorejea na kuhusisha ushirikina, licha ya kupigwa sana chenga, mwisho nikagundua ni kweli.

Sserunkuma alilalamika kwamba ameshindwa kuonyesha kiwango chake kwa kuwa anafanyiwa ushirikina. Mwisho akawaambia viongozi wa Simba anataka kuvunja mkataba, alifanya hivyo mara mbili kupitia kwake na kwa meneja wake.

Simba walishangazwa naye na kumtaka aachane na kuamini ushirikina. Mwisho yeye akasisitiza hatarejea na suala la kuvunja mkataba atalipa kipaumbele.

Baada ya Simba kukaa kimya, mwenye alituma tena ujumbe kupitia barua pepe akiomba radhi kwamba wakati anasema anataka kuvunja mkataba hakuwa katika hali nzuri. Siku iliyofuata meneja wake naye alituma narua pepe Simba na kusisitiza “wakati mwingine wachezaji ni kama watoto”, hivyo wamsamehe na atarejea kazini. Kweli alirejea na siku iliyofuata alionekana jukwaani wakati Simba ikishinda mabao 3-0 dhidi ya Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar!

Maswali mawili ya haraka. Moja, vipi mchezaji kama Sserunkuma anaanza kuamini utendaji wake umeshuka kutokana na kufanyiwa ushirikina? Pili, aliamua kuvunja mkataba, sasa vipi mbona ameamua kurudi?

Inawezekana majibu niliyoyapata yanaweza yasiwe sahihi, lakini lile la kuamini kuwa hata Sserunkuma naye ni tatizo linaweza kuwa sahihi zaidi.

Anaamini ushirikina unaweza kumfanya mchezaji fulani asicheze! Kweli unaweza kumroga Lionel Messi au Cristiano Ronaldo akashindwa kucheza? Kama anarogwa yeye ambaye hata bado hajakaa vizuri kwa kiwango, vipi hafanyiwi hivyo Emmanuel Okwi au Juuko Murishid ambao wote ni Waganda?

Ninaamini Sserunkuma ni kati ya wachezaji wenye uwezo. Amedhihirisha hayo akiwa Kenya, ameonyesha anaweza kwa kuitwa kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Uganda, The Cranes na inajulikana ina ushindani mkubwa.

Lakini hawezi kukataa kuwa ameingia kwenye mlango usio sahihi na kama ataendelea hivyo, basi hatainuka na ataendelea kuyumba hadi siku atakayoondoka Tanzania. Ukiuamini ushirikina, kweli unakushuka. Kama Mungu yupo, anayefanya ushirikina hawezi kuwa bora kuliko anayemuamini Mungu.

Kama Sserunkuma anaamini alikuwa staa Kenya, basi atafika hapa siku mbili na kuwa staa tena kajidanganya. Okwi hakung’ara siku ya kwanza au msimu wa kwanza, kapambana kweli.

Juuko, sasa ameanza kukubalika, anajituma na kazi anafanya. Sasa vipi yeye anataka alale au kutembelea nyota ya historia yake ya Kenya ambako aliishakubalika!

Kila himaya ina mfalme wake, kubadili mambo lazima uonyeshe kipya ulichonacho. Sserunkuma ndiyo ana uwezo na ana uwezo wa kufanya makubwa, lakini lazima ajipange, ajitume na kuwa mbunifu pia aache longolongo, acheze soka la sivyo, Bongo  kutamshinda na ataondoka watu wakiwa hawana lolote litakalofanya wamkumbuke.



2 COMMENTS:

  1. dah mkuu umeshuka nondo sana ila sioni kibofyo cha Like

    ReplyDelete
  2. dah mkuu umeshuka nondo sana ila sioni kibofyo cha Like

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic