March 2, 2015





Na Saleh Ally
JUMAPILI ijayo ndiyo siku ambayo makocha wawili wa Yanga na Simba wanaweza wakawa wanatamani isifike au ipite wakiwa wamelala.

Hans van Der Pluijm wa Yanga na Goran Kopunovic wa Simba, kila mmoja anajua ana kazi ngumu kupita zote kwa kuwa timu zao zinakutana.

Yanga inakutana na Simba ikiwa inataka ushindi kwa mambo mawili, kwanza kujiongezea heshima na kulipa kisasi kwa Simba ambao wamekuwa ‘wakiwadharau’ kila wanapokutana nao.

Simba wanajua, hali yao ni mbaya na pointi tatu ni muhimu kupita kiasi. Tena mechi inakuja baada ya ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya Prisons na kumalizika kwa mkutano mkuu uliokuwa na mikakati kibao.

Wanachama wa Yanga wanahitaji ushindi, mashabiki watafurahi kuona Mnyama kaanguka. Lakini pia Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji, angetaka kumaliza ‘kuonewa’ na Simba huku yule wa Simba, Evans Aveva angetaka kuonyesha kweli ni kiboko ya Yanga kama anavyoaminika alipokuwa kiongozi wa Friends of Simba (Fos).

Presha zote mwisho zinawaangukia makocha hao wawili ambao mapigo yao ya moyo yatakuwa yanazidi kupanda kwa wiki nzima ya maandalizi ya mechi hiyo.

Kuanzia jana, siku saba kamili, saa 168 ngumu kwa makocha hao, hakuna ubishi hawatakuwa na usingizi wa pono kwa kuwa mipango na presha ya ushindi itakimbiza usingizi wao.

Kila upande unataka ushindi, makocha wote wanalijua hilo. Hatari yake ushindi unatakiwa kuwa kwa timu moja, ikishindikana ni sare ambayo hakuna anayeitaka.

Kopunovic:
Atakuwa anafurahia ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya Prisons, lakini Jumapili ni siku ambayo hajawahi kuiona katika maisha yake akiwa kocha.

Amefundisha nchini Rwanda akiwa na Polisi, halafu Vietnam alipokuwa kocha wa Long Don Tam.

Jumapili atashuhudia umati wa mashabiki wengi zaidi. Lakini presha itakuwa juu kuliko zote ambazo amewahi kuwa nazo.

Huenda ile tabia yake ya midadi inaweza ikazidi kwa kuwa atatamani kuona timu yake inashinda na asipofanikiwa, basi ni kazi kwake.

Simba na Yanga wanapokutana ni presha kubwa, kocha anachotakiwa ni kushinda tu na hakuna mjadala mwingine.

Pointi 23 za Simba baada ya ushindi dhidi ya Prisons, iwapo watashinda dhidi ya Yanga watafikisha 26 na kuwa wanazidiwa tano tu na Yanga yenye 31.

Hiyo inaonyesha presha kubwa zaidi kwa Kopunovic na kikosi chake kwa kuwa wanajua iwapo watapoteza, pamoja na kupoteza furaha ya mashabiki, Yanga itafikisha 34 na kuwazidi kwa tofauti ya pointi 11, huku ikiwa na mchezo wa kiporo.



Pluijm:

Mholanzi Pluijm anaijua presha ya mechi hiyo, ingawa amefundisha nchini Ghana lakini aliona utofauti wa Yanga na Simba.

Pointi 31 ni nzuri kwake, zinaifanya Yanga kukaa kileleni lakini kuiruhusu ishinde dhidi yake ni kuiacha Simba isogee kwa tofauti ya pointi moja mgongoni mwao, si kitu sahihi.

Pia presha kubwa ni kwamba pamoja na Simba kuonekana haina kikosi imara, bado imekuwa ikiendelea kuinyanyasa Yanga inavyotaka.

Ushindi wa Yanga kwa Simba imekuwa ni sare. Kwa kikosi alichonacho, kushindwa kuifunga Simba, kibarua chake kitakuwa rehani.

Simba ina kikosi lakini si cha kudharau hata kidogo kwa kuwa kina wachezaji wanaoweza kubadili matokeo kwa uwezo wao binafsi.

Angalia Emmanuel Okwi, Danny Sserunkuma, Ibrahim Ajibu, Ramadhani Singano na wengine. Lakini Yanga bado ina wachezaji wengi wazoefu na wenye uwezo wa juu.

Hivyo presha ni kubwa zaidi kwa Pluijm ambaye analijua hilo na atapambana kuhakikisha anashinda.

Tatizo la Yanga, inatengeneza nafasi nyingi za kufunga lakini haizitumii. Kama itafanya hivyo mbele ya Simba, basi itajiponza.

Tena wachezaji kama watafanya hivyo, kuna uwezekano mkubwa wa kukutana na kashfa kwamba wamepewa ‘mlungula’ ili wasifunge wakati wamekuwa wana tatizo katika mechi kibao zilizopita na mfano mzuri ni zile mbili dhidi ya BDF XI jijini Dar es Salaam na kule Lobatse.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic