April 4, 2015




Na Saleh Ally
ZIMEBAKI mechi sita tu Simba kukamilisha msimu wa 2014-15 na sasa zaidi inapambana kupata nafasi ya pili angalau iondoe ugwadu wa kutoshiriki michuano ya kimataifa.


Wakati inapambana kwa kila namna, lazima kuwe na hesabu za usajili kwa ajili ya kuimarisha kikosi chake kwa kuwa kuna mambo mengi yamejitokeza.
 
TAMBWE...
Mfano, wachezaji wake wa kimataifa watano wote ni Waganda, lakini hadi sasa walioonyesha kiwango cha juu ni wawili tu, Emmanuel Okwi na Juuko Murishid. Joseph Owino, Simon na Dan Sserunkuma, hawakuwa sawa sana!


Kikosi kina vijana wengi, baadhi ya wakongwe walioachwa kama Amissi Tambwe sasa ni tegemeo Yanga.

SALEHJEMBE ilifanya mahojiano maalum na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe ambaye ni askari wa jeshi mstaafu ili aweze kuzungumzia mipango yao.

Zaidi kujua baada ya yaliyotokea, nini hasa wamepanga kufanya kuimarisha kikosi chao.

Mpango wa awali, mnataka kuimarisha kikosi kwa kusajili wachezaji katika nafasi ngapi?

Hans Poppe: Nafasi tatu ndiyo nina uhakika, beki wa kati, kiungo mmoja mchezeshaji pamoja na straika mmoja. Mengine, ni suala la kuangalia pia kusikiliza nyongeza  ya mapendekezo ya mwalimu.


 Dan Sserunkuma, ameonekana kushutumu kuhusiana na masuala ya kishirikina. Taarifa zinasema aliandika barua anataka kuondoka, halafu akabadili uamuzi. Unalizingumziaje hili?

Hans Poppe: Inawezekana kuna mambo yanatokea na sielewi lolote. Hilo la ushirikina yeye mwenyewe kakanusha, mimi nalielewa suala hilo tofauti. Sserunkuma aliomba ruhusa kwenda kumuuguza mkewe, akapewa siku tatu.

Alipofika akaambiwa anatakiwa kufanyiwa upasuaji, hivyo ilikuwa ni lazima akae zaidi. Akapiga simu kuomba ruhusa siku zaidi, akaruhusiwa.

Unafikiri akibaki anaweza kuisaidia Simba, au ni bora angeenda na kuwapisha Wazalendo katika nafasi yake?

Kama ni mawazo yangu nitasema ndiyo. Inawezekana bado aina yake ya uchezaji watu hawajaielewa, ana nguvu, mwepesi wa maamuzi na msumbufu sana kwa mabeki.

Watu lazima wajue kwamba Sserunkuma si lazima afunge, akitoa pasi au akiwapa wengine wakafunga bado atakuwa ni msaada kwa timu.

Nilimuona Kigali katika Kombe la Kagame, katika mechi mbili alifunga mabao matatu, tena alitokea benchi. Kwangu bado naamini ni mchezaji mzuri na atatusaidia.

Inaonekana kama unajitetea kuonyesha viongozi hamhusiki na ushirikina?

Hans Poppe: (Kicheko), Zungumza na kiongozi yoyote wa Simba atakueleza. Kwanza sijui kama wanafanya mambo hayo, hakuna anayeweza kufanya ushirikina mbele yangu.

Siwezi kuzungumza kuhusiana na ushirikina kwa kuwa siamini na siwezi kushiriki. Kila mtu Simba analijua hilo kuhusiana na mimi.
KIONGERA
Taarifa nyingine ni kwamba Patrick Kiongera anarejea Simba, nani sasa ataondoka katika wachezaji watano wa kigeni mlionao?

Hans Poppe: Tutakaa na kujadili, nani anaondoka na nini cha kufanya. Kiongera ni kweli tunamrudisha kwa kuwa hadi sasa ni mchezaji wetu na tunamlipa mshahara. Tulimpeleka Kenya kwa mkopo ili aendelee kucheza na wao wanajua atarudi Tanzania.

Wachezaji wengi hawapendi kutibiwa, baada ya Kiongera kuumia, bado aliendelea kulazimisha kucheza. Tukamuambia tuliyaona hayo wakati wa Owino ambaye alichelewa kwenda kutibiwa na hadi sasa amekuwa na matatizo ya majeruhi.

Pia Owino alitakiwa apumzike mwaka baada ya matibabu, sisi tukakubaliana na daktari alivyoagiza lakini Owino akaona kama anaonewa, akaamua kujiunga Azam. Siku chache kaumia, msimu mzima akakaa nje!

Hatukutaka kurudia makosa, ndiyo maana tulimsisitizia Kiongera lazima aende India, katibiwa na tumemsimamia hadi alipopona na sasa anacheza. Tuliona uwezo wake, hivyo atarudi kuja kusaidia safu ya ushambuliaji, hili halina shaka.


Wewe ndiye bosi wa kamati ya usajili, kamati yako imemuacha Tambwe! Sasa inaonekana kama ilichekesha, kweli mliona ni uamuzi sahihi na sasa kama mnaona haya mnatupia mzigo Kocha Patrick Phiri?

Hans Poppe: Nafikiri leo wakati mwafaka wa kuweka hili wazi, kwamba mimi ndiye nilisisitiza Tambwe aondolewe. Kweli Phiri hakutamka tumuondoe, lakini alisema vitu vinavyomaanisha kwamba hamhitaji.

Alipokuja alianza kumtumia Tambwe katika mechi za mwanzo, baadaye akaanza kumuweka benchi anaingia dakika za mwisho na baadaye ikawa anaingia kidogo. Nakumbuka mechi ya mwisho alimuingiza dakika tatu za mwisho.

Nikamuita kocha na kumuuliza vipi mfungaji bora wa msimu uliopita anaonekana kushindwa kucheza kwake. Phiri akaniambia kwa mfumo wake mchezaji wa box (anayesubiri kufunga) hawezi kufanya vizuri.

Kama hawezi kufanya vizuri, pia anamuingiza mwishoni au anakaa benchi kabisa. Sasa tunastahili kuwa na mchezaji anayekaa tu tena wa kimataifa?

Akifunga Yanga, haina maana ni kosa kumuacha. Alishindwa ku click (kufanya vema) katika mfumo wa Phiri. Angalia Yanga leo wana yule Mliberia (Kpah Sherman), ni mchezaji mzuri kabisa lakini sasa mambo hayaendi vizuri.

Hivi ni vitu vinavyotokea. Akiondoka leo Yanga anaweza kwenda kwingine akacheza vizuri na kufunga pia. Sasa ishu ya Tambwe isituumize sana vichwa.

Tena nisisitize, hata alipofika Yanga, bado Tambwe hakufanya vizuri hadi kocha wao (Hans van der Pluijm) alipobadili mfumo na kuanza kutumia viungo watatu kama Simba, angalau sasa unaona anaonekana.

Katika hili la Tambwe, nafikiri Simba tungepongezwa kumsaidia, sasa amepata timu imeendana na uchezaji wake. Angebaki huenda tungeua tu kipaji chake!

Sasa vipi viongozi wenzako walisema Phiri ndiye alisema Tambwe aachwe?

Hans Poppe: Kweli hilo silijui, ila nisisitize Phiri naye alikuwa tatizo. Alikuwa muoga wa lawama, aliwaamini wachezaji aliowajua zamani kama Shabani Kisiga na Amri Kiemba, unajua alidhani ndiyo walewale wa enzi zile, kumbe sivyo.

Kiemba aliboronga mechi na Prisons. Baada ya mechi tukamuuliza alimuonaje, yaani alivyocheza, akasema vizuri sana. Tulipomuonyesha mkanda wa video wa mechi, akasema ameshangazwa sana kuwa aliona amehujumiwa. Ikatushangaza sana, kwamba hakumuona pale uwanjani hadi aone tena kwenye mkanda?

Pia usisahau alikuwa hawaamini sana vijana. Angalia Said Ndemla na Abdi Banda, alisema wapelekwe kwa mkopo kwamba wanahitaji kukua kwanza, sikuwa nakubaliana naye.

Alipokuja Goran Kopunovic timu ilikuwa Zanzibar, tulimpeleka na kumuacha afanye kazi yake. Mwisho umeona leo Ndemla na Banda ni tegemeo na wanaisaidia Simba.


Kulikuwa na taarifa mmeamua kubadilisha kocha msaidizi, Selemani Matola alikuwa anaondoka, vipi imekuwa kimya?

Hans Poppe: Unaweza ulipita upepo mbaya, kipindi kile kila mmoja alionekana ni mchawi! Lawama kuna fulani tatizo mara vile.

Hakuna ambaye hakulaumiwa, hata mimi nilionekana ni tatizo kwa kutosajili vizuri. Sasa timu ni ileile na angalau inafanya vizuri. Kiongozi mmoja alionekana kumlaumu sana Matola, kuamini anaharibu. Lakini sasa mambo yametulia.


Je, bado mtaendelea na mkongwe Joseph Owino katika safu yenu ya ulinzi?

Kwangu naona Owino ameonyesha yuko tayari kustaafu. Maana aliondoka kwa madai alifarakana na kiongozi mmoja. Nikampigia simu na kumueleza haikuwa njia sahihi ya kuondoka, anapaswa kukumbuka ameishi vipi na watu, akarudi.

Lakini hiyo sehemu ya kuonyesha kwamba yu tayari kwenda. Ni mchezaji mzuri, lakini naona mwisho wake Simba umefika. Lakini naweza kusema ni suala la subira na kukaa pamoja ili tuone itakuwaje.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic