April 7, 2015

GARCIA AKIPIGA MAHOJIANO NA SALEH ALLY

Na Saleh Ally
LUIS Garcia Sanz ni kati ya wachezaji wenye kumbukumbu nyingi ndani ya klabu ya Liverpool ya England, pia Barcelona ya Hispania.


Luis Garcia tayari yuko nchini kwa ajili ya kujiandaa na mechi dhidi ya nyota wa Tanzania itakayochezwa Jumamosi wenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, yeye akiwa katika kikosi cha wakongwe wa Barcelona.
Wakongwe hao watacheza dhidi ya nyota wa Tanzania waliowahi kuwavaa wakongwe wa Real Madrid.
AKISHANGILIA NA RONALDINHO
SALEHJEMBE, imefanya mahojiano maalum na Garcia ambaye pamoja na kuahidi kuonyesha mambo ya uhakika hiyo Jumamosi, amejibu maswali lukuki ambayo wengi wangependa kujua.

Anajulikana kwa mafanikio makubwa wakati akiichezea Liverpool kuanzia mwaka 2004 hadi 2007 alipoamua kurejea Hispania na kujiunga tena na Atletico Madrid.

Garcia anasema mechi zake 121 akiwa na Liverpool aliyoifungia mabao 30, zinajenga mapenzi ya dhati na kamwe hatoacha kuipenda timu hiyo ya England hadi mwisho wa maisha yake.
AKISHANGILIA BAADA YA KUFUNGA BAO WAKATI AKIKIPIGA LIVERPOOL.
Katika miaka minne ya Liverpool, walibeba mataji matatu, moja la Ligi ya Mabingwa Ulaya. Tena katika miaka hiyo wakafika fainali ya Ligi ya Mabingwa mara mbili, si kitu kidogo.

Anasema mashabiki wa Liverpool wamekuwa wakiendelea kuimba na kumsifia hadi leo hata wanapokwenda kucheza mechi za Ligi Kuu England, jambo linalomfanya aamini Anfield ni nyumbani kwake milele.

Maisha yake ya soka linalotambulika yalianzia Barcelona B mwaka 1997, lakini ana mengi ya kuyakumbuka England likiwemo lile bao maarufu kama “Ghost Goal” alilofunga katika mechi dhidi ya Chelsea.
Kocha Jose Mourinho ndiye alilitoa jina la “Ghost Goal” akionyesha kupinga kwa kuwa mpira haukuvuka msitari. Lakini mwamuzi hakuona na kuonyesha kati, jambo lililomuudhi sana Kocha huyo Mreno huyo.
AKISHANGILIA BAADA YA KUWAFUNGA CHELSEA "GHOST GOAL"

“Mourinho alikasirika sana, lakini baada ya mchezo alikuja na kunipongeza kwa mchezo mzuri siku ile ila hakuzungumzia kabisa kuhusiana na bao hilo,” anasema Garcia katika mahojiano na gazeti hili jijini Dar, jana.
“Nimekutana na Mourinho mara kadhaa baada ya mechi ile, hakuwahi kukumbushia tena ingawa kwingine alilalamika sana.”
AKIFUNGA MBELE YA JOHN TERRY

Wimbo wake:
Kwake anaona ushindi au kufunga bao ilikuwa moja ya kazi yake kubwa kwa kikosi cha Liverpool.
Mashabiki wa Liverpool, wanaonyesha kuyakumbuka mazuri yake kwa kuendelea kuimba wimbo wake maalum wa “You’re my sunshine”.

“Nilifanya kazi nzuri, mashabiki hadi leo wanapoimba maana wana furaha na mimi. Marafiki na ndugu wamekuwa wakinieleza kuhusu wimbo huo na mashabiki wengine kupitia mitandao kama Twitter wamekuwa wakinieleza hilo. Ni Jambo la kujivunia, inanipa furaha sana.”
AKISHANGILIA NA XAVI...

Mashabiki wa Liverpool waliwahi kumpa nafasi ya 34 katika wachezaji 100 waliowahi kuichezea Liverpool.
Nafasi hiyo aliipata kutokana kura zilizopigwa na mashabiki hao wa Liverpool na hiyo ni sehemu ya kuonyesha kuwa ye ni kati ya vipenzi wa Liverpool.

Kipigo Arsenal:
Mechi yake ya mwisho Liverpool alikutana na kipigo cha mabao 6-3 dhidi ya Arsenal katika mechi ya Kombe la Ligi.

Garcia anasema ni kipigo ambacho hatakisahau kwa kuwa walikuwa nyumbani na Arsenal wakawaadhibu vibaya. Mbaya zaidi ilikuwa mechi yake ya mwisho.
Siku chache baadaye Liverpool wakatangaza aliumia na alitakiwa kukaa nje miezi sita. Ajabu, wakatangaza tena anakwenda Atletico Madrid ambako mwaka huohuo wa 2007 akaanza kucheza!

“Kidogo iliwashangaza mashabiki wa Liverpool, najua walipenda nibaki. Kweli niliumia, lakini mimi ndiye nilifikia uamuzi wa kurudi Hispania na kujiunga na Atletico Madrid ambayo niliondoka mwaka 2003 na kujiunga na Racing Santander. Ulikuwa ni uamuzi, kwamba narudi kucheza nyumbani Hispania:

Torres:
Kuondoka kwake kurejea Atletico Madrid, ilielezwa kuwa mwanzo wa uhusiano kwa klabu hiyo uliosaidia Liverpool kumpata Fernando Torres.

“Kweli ilisaidia, mazungumzo yalianza baada ya Rafa Benitez kwenda Liverpool. Lakini uhamisho wangu ulikuwa chanzo uhusiano mzuri kwa klabu hizo.
“Lakini kazi yangu nzuri pia ilichangia imani kwa Liverpool na wachezaji kutoka Hispania,” anasema Garcia.

Mshambuliaji huyo aliyekuwa akiujua mpira vema, aliamua kustaafu soka alipotangaza rasmi Januari 14, 2014.

“Kweli nilitangaza siku hiyo yenye namba 14 mara mbili. Hiyo ndiyo ilikuwa namba yangu ya jezi niliyokuwa ninaipenda sana.

“Ilikuwa ni siku mwafaka kwangu kutangaza kujiuzulu, lakini baadaye nimerudi na kucheza tena soka nchini India. Sasa nina miaka 36, katika klabu ya Atletico Kolkata ni mchezaji lakini zaidi ni kuhamaisha.
“Ninaweza kurudi tena India, wanajitahidi kukuza soka lao. Litafika mbali hivi karibuni,” anasema.
AKIPAMBANA NA FIGO...

Jumamosi Taifa:
“Wanakuja wachezaji wengi, mfano Mandieta, Deco, Sambrosa, Kulivert na wengine. Lakini tunalazimika kujiandaa kwa kuwa tulielezwa mechi Madrid ilikuwa ngumu.

“Tumeelezwa kuhusiana na kasi yao na pia nguvu. Tutajitahidi kucheza staili ya Barcelona na kushinda, lengo ni kushinda ingawa tunajua haitakuwa lahisi,” anasisitiza Garcia.

Garcia amecheza na wachezaji wengi wa kiwango cha juu, mfano Ronaldinho, Luis Enrique ambaye sasa ni kocha Barcelona. Pia Sergio Aguero akiwa Atletico Madrid, Steven Gerrard wakiwa Liverpool na wengine wengi.

“Wengi wanajua mpira, lakini Ronaldinho alikuwa kitu kingine. Kila aliyecheza naye atakueleza. Ni nyota hasa wa mpira ambaye anastahili.”




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic