April 17, 2015


KUNA jambo moja, linaweza lisiwe geni sana kwa wengine lakini mimi lilinivutia na kuona ni wakati mzuri sana ninaweza kulizungumzia, tukalijadili kwa pamoja.


Lengo langu ni kutaka muone namna gani tunavyoweza kuwa tofauti upande wa makosa, hasa linapofikia suala la utaifa.

Najua mashabiki wengi wa Yanga hawawezi kuishangilia Simba inapokuwa na majukumu ya kitaifa. Hali kadhalika, mashabiki wa Simba, hawawezi kufanya hivyo kwa Yanga.

Kila mmoja ana itikadi zake, mwingine anasema kuizomea Yanga ni raha yake, mwingine kuishangilia ni mwiko na mengine mengi lakini linapofikia suala la utaifa, kuna kila sababu ya kubadilika.

Etoile du Sahel wameamua kwa pamoja, kukodi ndege moja na kikosi kingine cha Esperance ili kwenda Sudan na kuja Tanzania kwa ajili ya mechi mbili zilizo chini ya Shirikisho la Soka Afrika (Caf).

Esperance wanashiriki Ligi ya Mabingwa Afrika, wanakwenda Sudan kupambana na El Merreikh walioitoa Azam FC na baadaye wakaing’oa Kabuscorp ya Angola, haitakuwa mechi rahisi.

Etoile wanakuja nchini kupambana na Yanga katika mechi yao ya kwanza ya Kombe la Shirikisho. Pia wameitoa Benfica ya Angola wakati Yanga iliitoa FC Platinum ya Zimbabwe.

Etoile waliitoa Yanga katika Ligi ya Mabingwa Afrika mwaka 2009 kwa kuichapa mabao 3-0 pale Tunis, nilikuwa uwanjani. Timu hiyo inatokea katika mji huo mkubwa na wapinzani wake wakubwa ni Club African.

Etoile inatokea katika mji mdogo wa Sousse, lakini zinapokutana kwenye Ligi Kuu ya Tunisia, maarufu kama League 1, kumekuwa na ushindani mkubwa baina ya timu hizo. Wakati mwingine zimekuwa zikitokea vurugu kubwa katika mechi zinazokutanisha Etoile na Esperance.

Lakini leo wamekwea ndege moja, kwa pamoja na umoja wakiwa marafiki wanaoweza kuzungumza lugha moja kwa kuwa wanakwenda kulitetea taifa lao la Tunisia.

Wanakwenda nje ya mipaka ya Tunisia kama wanajeshi wa nchi hiyo. Kama watashinda watarejea nyumbani wakiwa mashujaa wa taifa lao wakisubiri mechi za nyumbani kumaliza kazi.

Ndege inapita Sudan kuwashusha Esperance, inapaa tena hadi Dar es Salaam kuwasubiri Etoile. Baada ya mechi wanapitia Sudan kuwachukua ndugu zao, wanarejea nyumbani. Huu ndiyo ulikuwa mpango uliotangazwa na klabu zote mbili zikakubaliana.

Hata kama usingefanikiwa, nia yao ya kulitekeleza hili imenifanya niwe na maswali kama Yanga wanaweza kupanda ndege na Azam FC kwenda nchi fulani kupambana kwa ajili ya taifa!

Imenikumbusha jambo hili pia, kwamba je, wale mashabiki wa Simba wanaoizomea Yanga wanajua kwamba inapigana kwa ajili yao na nchi yetu? Hata wale ambao hawakuwahi kuishangilia Simba ilipofanya vizuri kimataifa, kweli leo hawakumbuki na kujuta? Kwamba hawakuwa wazalendo!

Mimi sijali ni Yanga au mimi ni Simba lakini kwangu naona siwezi kuwashangilia watu nisiowajua, wasio na faida kwangu ambao baada ya kuifunga timu ya Tanzania wanarejea kwenda kupokelewa kwao kwa shangwe.

Ninajua, hii hata kwako kuwa tuna marafiki, ndugu au wazazi wanaweza kuwa Yanga, sisi Simba. Au wewe Yanga, unaweza kuwa na ndugu na marafiki wakawa ni Simba. Sasa vipi uishangilie timu inayotokea usipopajua?

Huenda kelele za kishabiki, mfano usikie shabiki wa Yanga anasema hahitaji mchango wa Simba au sapoti, huyo anaweza akawa amezungumza kishabiki tu lakini ukweli lazima tukubali, lazima tubadilike na kuamini kulipenda taifa letu hakuwezi kuishia kwenye maneno tu.


Kwangu naona mtu ambaye anaona hataki kuishangilia Yanga ikipambana na wageni, si vibaya akabaki nyumbani ili baadaye ahadithiwe ilivyokuwa. Si sahihi kwenda uwanjani kuwavunja nguvu. Nasema hili leo kwa Yanga, kesho iwe kwa Simba au timu yoyote inayoliwakilisha taifa. Mimi ni mzalendo.

2 COMMENTS:

  1. BIG UP MWANDISHI.

    ReplyDelete
  2. lazima nikashangilie Etoile du Sahel hao yanga sipendi hata kuwatazama,..na huyo mwanahabari wao jeri muro...tutaukatana mwakani..TUSIDANGANYANE KWA HILI...WAO NDO WA KWANZA MWAKA 1993 KUIBA UZALENDO UMEWASHINDA WAKATUZOMEA PALE SHAMBA LA BIBI ...SO MUOSHA HUOSHWA

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic