April 27, 2015


SIKUFIKA uwanjani katika mechi ya Ligi Kuu Bara kati ya Ruvu Shooting dhidi ya Yanga ambayo iliisha kwa vijana wa Hans van Der Pluijm kushinda kwa mabao 5-0.


 Ushindi huo mnono wa Yanga umewaingiza katika dakika 90 tu wanazotakiwa kukamilisha kazi ya msimu, yaani kutwaa ubingwa.

Yanga wanashuka dimbani leo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kucheza na Polisi Morogoro na kama wakishinda, basi rasmi watatawazwa kuwa mabingwa wapya.

Nikiwa nashuhudia mechi hiyo kwenye runinga ya Azam TV, nilimshuhudia beki George Michael Osei akimpiga kiwiko Mrisho Ngassa wa Yanga.

Teknolojia mambo mengine bwana! Azam TV walirudia mara nyingine kuonyesha kwa uzuri kabisa beki huyo aliyepewa jina la beki katili akimtwanga kiwiko Ngassa akaanguka chini.

 Kitu kizuri kabisa kilichokuwa wazi, mwamuzi Isihaka Shirikisho wa Tanga alikiona kiwiko hicho na haraka akamuita beki huyo na kuingiza mkono katika mfuko wake wa kaptula ikiwa ni dalili angetoa kadi nyekundu.

Wachezaji wa Ruvu Shooting walimzonga Shirikisho kwa nguvu zote wakisisitiza kwamba Ngassa alidanganya na kujiangusha ili beki huyo apate adhabu kama ambavyo imekuwa ikielezwa kwamba anasingiziwa.

Shirikisho alikosa nguvu na mwisho akaamua kutoa kadi ya njano ambayo kwangu ilinishangaza. Mchezaji anampiga mwenzake kiwiko, tena hawagombei hata mpira unawezaje kusema ni bahati mbaya?

Ngassa alikuwa anapishana na Osei, akitokea upande mmoja kwenda mwingine na hakuna aliyekuwa akigombea mpira. Ilivyokuwa inafanana sana na ile ishu ya Emmanuel Okwi wa Simba dhidi ya Aggrey Morris wa Azam FC.

Kama unakumbuka Morris alifungiwa kwa kuwa Okwi alizimia. Lakini Osei pia alifungiwa baada ya picha yake akimkaba koo mshambuliaji Amissi Tambwe wa Yanga kunaswa na wapiga picha mahiri wa gazeti la Championi.

Ingawa ilizua mjadala, wapo waliosema anaonewa kwa kuwa walitanguliza ushabiki, mwisho alipewa adhabu ya kufungiwa mechi tatu. Shukrani kwa Championi kwa kazi nzuri kabisa.

Aliporejea, mechi dhidi ya Stand United, Osei akalambwa kadi nyekundu tena kutokana na kucheza rafu mbaya.

Msemaji wa Ruvu Shooting, Masau Bwire amekuwa akimtetea sana  Osei kwamba si mtu mkorofi badala yake wamekuwa wakimchokoza tu. Lakini ukiangalia marejeo ya yeye na Ngassa unagundua ni ukatili unaopita kiasi na mimi ninaamini hawezi kusonga mbele zaidi ya hapo.

Mchezaji anayeingia uwanjani kuwaumiza wenzake makusudi. Kwa kuwa anaamini mpira si kazi yake ana uhakika na ajira yake kwa kuwa ni askari.

Vipi unampiga mtu kiwiko bila sababu ya msingi, kwa makusudi, tena mkiwa hamna mpira! Mbaya zaidi siku chache zimepita tangu uboronge na mabosi wako wametumia nguvu nyingi kukusafisha.

Mimi naamini ukiwa askari nidhamu inakuwa juu zaidi. Vipi huyu Osei na ajabu bado viongozi kama Masau wanaweza kufungua mdomo na kumtetea tena kwa tukio hilo.
Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) litawashangaza wengi kama litamuadhibu rais wake, Jamal Malinzi, maana ndiye bosi. Lakini vipi suala la Osei kwa mara nyingine linatokea na hakuna lolote! Huyu beki ni maarufu sana? Akikosekana mambo yote ya Ruvu au soka la Tanzania yatakwama?

Ubaguzi unapigwa vita katika soka, watu wanabeba mabango, wachezaji wanavaa fulana na vinginevyo. 

Inawezekana ni wakati wa kumpinga Osei kwa mabango kwamba amezidi na anapaswa kujitambua, aache mambo ya kizamani, yasiyokuwa na msingi, mambo yanayofanywa na watu wasiojitambua na kama askari anapaswa kuwa mfano katika nidhamu.

Osei, acha longolongo, cheza soka. Pia litakuwa ni jambo sahihi TFF wakichukua hatua kwa mara nyingine kukomesha upuuzi kama huo katika Ligi Kuu Bara.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic