May 2, 2015



Na Saleh Ally
UNAPOKWENDA Ulaya, jezi inayoongoza kwa kuuzwa kuliko zote ni ya rangi nyeupe na ufito mweusi au rangi ya dhahabu.


Hiyo ni jezi ya mabingwa wa Ulaya, Real Madrid ambao tayari wameuza zaidi ya jezi milioni 1.5. Pamoja na kuboronga Ligi Kuu England, Manchester United inashika namba moja England na mbili Ulaya kwa kuuza jezi milioni 1.4.

Nafasi ya pili Hispania inakwenda kwa Barcelona ambayo inashika nafasi ya tatu Ulaya ambayo imeuza zaidi ya jezi milioni 1.2.

Chelsea wako nafasi ya pili England na nne Ulaya baada ya kuuza zaidi ya jezi 910,000 ikiwa ni mara ya kwanza kufanya vizuri zaidi na kuzipiku Arsenal na Liverpool.


Takwimu za Ulaya zinaonyesha ziko juu sana kama utalinganisha na za hapa nyumbani, lakini jezi yenye rangi za njano na kijani ndiyo imeonekana kuuzwa zaidi kwa msimu unaomalizika mwezi huu.

Kupitia tathmini kadhaa zilizofanywa na gazeti hili, inaonyesha jezi ya Yanga ndiyo iliyouzwa zaidi ya jezi nyingine yoyote.


Yanga imeuza jezi yake kwa kiasi kikubwa kupitia chache ambazo ni ‘orijino’ na nyingi zaidi ambazo ni feki.

Katika mahojiano na wauzaji na baadhi ya wanunuzi, inaonekana wengi wamekuwa wakinunua jezi za Yanga na kiwango cha manunuzi kilipanda kwa asilimia 68 kuanzia Januari, mwaka huu wakati Yanga ilipoanza kushiriki michuano ya kimataifa.

Asilimia 12 za mauzo kupanda ziliongezeka mwezi uliopita wakati Yanga ilipoanza kuonyesha ina asilimia kubwa zaidi ya kubeba ubingwa wa Tanzania Bara. Ilipofanikiwa kuubeba, mauzo yalizidi kuwa juu zaidi kwa jezi hizo za kijani na njano.

Wauzaji wakubwa wa jezi feki, wengi wanaamini huuza hadi jezi 1,000 kwa mwezi zikiwamo zinazokwenda mikoani. Maana yake kwa wauzaji hadi 10,000 zinaweza kufikia au zaidi ya jezi 100,000 ambazo zinanunuliwa kwa bei kuanzia Sh 8,000 hadi Sh 10,000.

Jezi za Simba pia huuzwa hadi bei kama hiyo ya Yanga ingawa kutokana na timu yao kutofanya vizuri, wanaouza jezi orijino wamekuwa wakilazimika kushusha hadi Sh 20,000 ili kuzisaidia kuuzika. Hii inaifanya jezi ya Yanga kubaki juu zaidi kwa bei na kuifanya kuwa ghali kwa msimu huu pia iliyouzika sana.


Jezi orijino, ambazo huuzwa kuanzia Sh 25,000 hadi 30,000 zinaonekana kuwa na mauzo ya chini kabisa kwa kuwa kwa mwaka mzima zimeuzwa 10,000 tu, tena pamoja na za Simba na hii tathmini ni kupitia kwa kampuni ya Romario ambao ni wasambazaji wa vifaa vya michezo vya Uhlsports ambavyo hutumiwa na Yanga, Simba na timu nyingine za Ligi Kuu Bara.

Kwa msimu mzima, inaonyesha Yanga imeuza jezi zipatazo 180,000 kwa feki ambazo ni nyingi zaidi pamoja na orijino.

“Unajua sisi tuna mkataba wa kusambaza jezi za Ligi Kuu Bara. Huwa zinabaki chache tu ambazo tunaweza kuziuza lakini si rasmi kwamba tunauza za mashabiki.

“Lakini Yanga na Simba kwa pamoja wanaweza kufikisha hadi jezi elfu kumi zinazonunuliwa. Ila wale wanaouza feki ndiyo wanauza zaidi,” kilieleza chanzo kutoka kampuni hiyo maarufu ya kusambaza vifaa vya michezo nchini ya Romario.


Wauzaji wengi wa mtaani, wanaonekana kupata faida kubwa kutokana na bei yao kuwa chini na jezi za Simba ndiyo zinazofuatia kimauzo.

Simba hawako nyuma sana, wana uwezo wa kuuza hadi jezi 125,000, wameporomoka kimauzo kutokana na timu yao kuyumba mfululizo kwa misimu mitatu sasa.

Wengi wamekuwa wakinunua jezi hizo kwa wingi kabla na baada ya mechi dhidi ya Yanga ambayo wana imani kubwa ya kufanya vizuri.

Timu ya tatu kwa mauzo imekuwa Mbeya City. Taarifa zinaeleza imeingia mkataba na Kampuni ya Romario ili watengenezewe jezi orijino wauze kwa mashabiki.

Wao wamefanikiwa angalau kudhibiti kidogo uuzwaji wa jezi feki lakini kwa Dar es Salaam bado zinauzika na kwa mwezi hadi jezi 2,000 huuzwa kwa mwezi. Wakati Nyanda za Juu, Kusini nako wana soko zuri.

Angalau kwa mwezi, Mbeya City wanaweza kuuza jezi 2,500 kulingana na wakati. Kwa msimu mzima, wameuza zaidi ya jezi 24,000 ukijumlisha feki na orijino. Msimu uliopita, ulikuwa mzuri zaidi, lakini msimu huu kuyumba kwa kikosi chao, kukayumbisha soko mtaani.

Azam FC imekuwa na mfumo mzuri wa usambazaji wa jezi zake. Hivyo kufanya iwe na soko angalau la jezi 11,000 kwa msimu.

Hata hivyo, inaonekana uchache wa mauzo unatokana na timu hiyo kuonekana si ya wananchi kama zilivyo Yanga, Simba na Mbeya City.

Hata hivyo, mpangilio mzuri wa uuzwaji wa jezi hizo unazifanya angalau kupatikana na sasa imezipiga bao hata timu za wananchi kama Coastal Union, Stand United na nyingine chache.


Mpangilio mzuri zaidi wa uuzwaji, upatikanaji na ubunifu unaweza kusaidia jezi za timu za Tanzania Bara kuuzwa zaidi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic