May 2, 2015


Na Saleh Ally
KAMA utazungumzia viongozi wa soka kwa sasa, basi Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Mahbub Manji ndiye gumzo zaidi kuliko mwingine yeyote.


Manji ambaye amekuwa kimya kwa muda mwingi, mgumu kusikika kwenye vyombo vya habari akizungumza lakini jina lake halitoki midomoni mwa mashabiki wapenda soka, wawe wa Yanga, Simba na timu nyingine.

Hali hiyo inatokana na mwenendo mzuri wa Yanga katika Ligi Kuu Bara hadi ilipofanikiwa kutwaa ubingwa ikiwa na michezo mkononi.

Lakini aina ya uongozi wake umeibadili Yanga na kuifanya sasa ni moja. Hakuna migogoro na kwa pamoja mashabiki wanachotaka ni mafanikio ya timu na klabu yao kwa jumla.

Katika mahojiano maalum na Championi Jumamosi, Manji anasema Yanga aliyoitaka ya umoja ndiyo iliyopo sasa kwa kuwa ni klabu ya watu wanaoshirikiana wenyewe, wanaoshirikiana na klabu nyingine, pia wanaoelewa kwamba michezo ni umoja na si uadui.


Tokea uongozi umeingia madarakani, kipi hasa unaweza kujivunia?

Manji: Najivunia kuwa na watu wenye umoja. Nikukumbushe, nguvu ya Yanga ni watu. Ndiyo maana nimekuwa nikisisitiza kuwa hii ni klabu ya watu, inamilikiwa na watu.

Zaidi ninajivunia umoja wao, kuwa na wanachama na mashabiki walio pamoja. Uongozi imara, kikosi imara na benchi bora la ufundi.

Hivi karibuni ilionekana kama uongozi wako umetikisika na viongozi kadhaa waliondolewa. Huoni ni tatizo?

Manji: Kuna wakati kiongozi inabidi uwe imara. Ilikuwa ni lazima kurekebisha matatizo yaliyojitokeza, ndiyo maana leo unaona Yanga imetulia.

Uongozi ni imara kwa kuwa waliopo ni watu sahihi. Tuna katibu ambaye ni daktari wa michezo, tuna viongozi wengi ambao ni vijana na wachapakazi. Tumebadili mambo, unaona vitu vinakwenda.


Kuna kitu ambacho kilikushinda mara baada ya kuwa umeingia madarakani na unatamani kukikamilisha kabla ya muda wako kwisha?

Manji: Ninaamini hakuna.

Vipi kuhusiana na kurejesha bao tano ambazo Yanga walifungwa na Simba misimu mitatu iliyopita?

Manji: Hapa watu wamekuwa wakichanganya, wakati naingia kugombea Yanga nilieleza kilichonifanya nigombee. Tulifungwa mabao tano bila na Simba na ikaonekana kama tumepoteana, tulisambaratika.

Niliamini kipindi hicho Yanga walihitaji mtu imara ambaye angeweza kusimama na kuwasahaulisha yaliyopita kwa ajili ya kupambana ili mambo yaendelee.

Niliahidi kurudisha umoja ambao sasa unauona.  Kuwafunga Simba tano ni jambo jingine kabisa na kama halijatokea wakati wa uongozi wangu, wengine watafanya.


Simba ni watani wenu, unacho cha kujivunia kama vile uliwahi kuwafanya washindwe kufanya jambo fulani?

Manji: Uongozi wa Simba uliopita na uliopo sasa unajua. Kwa misimu mitatu sasa Simba hawajashika nafasi ya pili wala kushiriki michuano ya kimataifa, ndiyo kipindi cha uongozi nimekuwa madarakani.

Kwa miaka mitatu nikiwa na uongozi wangu, tumeiwezesha Yanga kuchukua ubingwa mara mbili, nafasi ya pili mara moja. Ndiyo maana nasema kama Simba wakinyoosha vidole vitano, mimi nitanyoosha vitatu ambacho kimekuwa kipindi kigumu sana kwao katika ligi na michuano ya kimataifa.

Je, ulifanya lolote kusaidia kudumisha uhusiano wa kimichezo kati yako na Simba?

Manji: Nafikiri hujawahi kusikia nikiwasema Simba vibaya au kuwabeza hata mara moja. Simba si adui zetu, ni wapinzani na watani wetu. Utaona hata baada ya Rais mpya wa Simba, (Evans) Aveva kuingia madarakani, nilikuwa kiongozi wa kwanza kumpongeza.

Pia wakati tunataka kumsajili (Amissi) Tambwe nilimpigia Aveva na kumueleza kuwa pamoja na kwamba walimuacha, sisi tulihitaji kumchukua. Hii ilikuwa ni kuonyesha sisi ni watu ambao tunaweza kushirikiana.

Uongozi wa wakati wangu umezika mambo mengi ambayo yalifanyika nyuma na sasa soka ni sehemu ya kujenga, kufurahisha na kushirikiana pia.


Unafikiri nini kifanyike zaidi kudumisha yaliyopo ili kuepusha kupiga hatua mbili mbele na baadaye kurudi nyuma tatu?

Manji: Ushirikiano, viongozi kufanya kazi kwa maslahi kwa maendeleo ya klabu, pia upendo. Utaona leo kila mchezaji ikiwezekana kutoka kila timu anatamani kuichezea Yanga.

Hii inaonyesha tunaishi katika mwendo ulio sahihi na wengi wanatamani kufikia tulipo, hivyo lazima tudumishe.

Yanga imefanya vizuri nyumbani. Vipi kuhusiana na michuano ya kimataifa inaonekana bado mtihani?

Manji: Naungana na wewe, ni mtihani, lakini kwa sisi mnaotaka tuchukue ubingwa Afrika tukiwa hatuna hata uwanja wa mazoezi, nafikiri hamtutendei haki.

Nakumbuka uliahidi kujenga uwanja na sasa muda wako wa uongozi unakaribia kwisha, vipi sasa?

Manji: Nataka nikuhakikishie hiyo ilikuwa nia yangu mimi na viongozi wote wa wakati wetu, lakini umeona juhudi zetu za kuiomba na kuishawishi serikali kutupa eneo zilivyoshindikana.

Kweli ni ahadi, sasa uwanja tutajenga wapi. Wataalamu wameonyesha uwanja sahihi unavyopaswa kuwa na eneo ambalo serikali imetunyima. Kunaweza kuwa na sababu kwamba ni eneo la hifadhi, lakini kuna kituo cha mabasi kimewekwa pale.

Kwangu haikuwa changamoto kubwa, serikali imenikatisha tamaa. Nimeona wameshindwa kutupa eneo hilo kwa miaka mitatu sasa, wangeweza vipi kufanya hivyo ndani ya mwaka mmoja!

Uchaguzi unakuja. Je, una mpango wowote wa kugombea kwa mara nyingine?

Manji: (Tabasamu), nafikiri ni wakati mzuri wa kuwashawishi Wanayanga wengine wenye uwezo wagombee. Kwangu sioni changamoto nyingine mbele yangu. Kama ningekuwa nina eneo, ninatakiwa kujenga uwanja, angalau ningesema kuna la kufanya.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic