May 9, 2015


Na Saleh Ally
LOUIS van Gaal ni mmoja wa makocha bora duniani kama utazungumzia kwa kiwango cha klabu na hata timu za taifa.

Mafanikio yake akiwa na Ajax, Barcelona na Bayern Munich yanajulikana. Amekuwa bosi wa makocha wengi bora duniani akiwemo Pep Guardiola na Jose Mourinho.

Sasa amekuwa akihaha kuhakikisha Manchester United anayoinoa inasimama. Ana mipango mingi sana.

Hakuna anayeweza kumgeuza Van Gaal au kumfundisha kazi ila ushauri inawezekana. Kwa mujibu wa takwimu, inaonekana Man United ni timu ya nne kwa ubora hadi sasa England.

Si ubora kwa maana ya msimamo, takwimu za uchezaji mechi, ufungaji mabao zinaonyesha katika timu nne za juu Man United ndiyo dhaifu zaidi ya timu nyingine.

Udhaifu wake umegawanyika katika jambo kuu la ulinzi ambalo unaweza kuligawanya mara kadhaa.

Ingawa amemsajili Memphis Depay ambaye anaelezwa kuwa na uwezo zaidi ya Cristiano Ronaldo, lakini bado hilo linaonekana si tatizo la Man United kwa msimu huu ambao umebaki mechi tatu ufungwe na bingwa Chelsea tayari akiwa ameshajulikana.

Tatizo la Man United ni ulinzi, kwani unapochukua timu nne za juu kwenye msimamo, Man United ndiyo timu iliyofungwa mabao mengi zaidi.

Man United ndiyo timu iliyopoteza michezo mingi zaidi, sare nyingi zaidi. Hiyo inaonyesha ulinzi, unapaswa kuimarishwa zaidi kwa kuwa kikosi hicho bado kina wachezaji wengi sana wa ushambuliaji kama Wayne Rooney, Juan Mata, Angelo Di Maria, Radamel Falcao, Robin van Persie na wengine lundo.

Kufungwa:
Man United inaonekana kuwa na tatizo kubwa katika ulinzi. Kwani katika mechi zake 35 ilizocheza, imepoteza nane. Ndiyo nyingi zaidi katika timu zote nne za juu.

Chelsea ambao ni mabingwa wamepoteza mbili tu, Man City saba na Arsenal wamefungwa mara sita.

Kufungwa kumezidi kuiathiri Man United, utaona ilifungwa mechi tatu mfululizo na kuifanya iwe timu iliyoruhusu mabao na kupoteza michezo mingi mfululizo sawa na Wes Brom, Newcastle na Hull City.

Sare:
Katika timu hizo nne za juu Manchester United ni miongoni mwa zenye sare nyingi. Inazo nane, sawa na Chelsea, wakati Arsenal na Man City kila moja ina saba lakini kumbuka sare zinapoteza pointi mbili katika kila mchezo, hivyo si za kuzifanyia sherehe pia.

Ushindi:
Huenda hapo ndiyo Van Gaal ameanza kupafanyia kazi, kwani Man United ndiyo timu iliyofunga mabao machache zaidi katika timu nne za juu. Imefunga mara 59.

Mabingwa Chelsea wamefunga mabao 69, tofauti ya mabao 10 na Man United. Man City wamefunga 71 na Arsenal wana 66. Maana yake, Van Gaal kweli anatakiwa kuangalia nguvu ya ‘kucheka’ na nyavu na kuhakikisha inaimarika.

Ushindi ni muhimu kuliko jambo lolote kwa kuwa unatengeneza pointi tatu ambazo ni pointi nyingi zaidi katika soka kwenye mchezo mmoja.

Mourinho wa Chelsea amekuwa akijihakikishia ushindi bila ya kujali soka lake ni la kuvutia au la.

Si lazima Van Gaal acheze soka lisilo na mvuto lakini mvuto bila ya ushindi pia hauna faida kwa timu na hata shabiki.

Hakuna msimamo wa pasi au wa soka la kuvutia. Hivyo ingawa Van Gaal ameanza mpango wa kumsajili beki kisiki wa Borussia Dortmund, Matts Hummels lakini bado hakwepi kutakiwa kutwaa viungo bora wa ukabaji kuhakikisha Man United inafanya vizuri.

Kama itaendelea kuwa laini katika safu ya ulinzi, haiwezi pia kuwasaidia mafowadi wake kufanya vizuri mbele hata kama watakuwa na ubora wa juu sana. Maana watafunga na mabao yatarudi kirahisi. Mwisho, watakata tamaa.

Kwa maana ya ubora, maana yake, Man United kwa sasa haina ubora wa Arsenal, Man City na Chelsea na hicho ndicho kinachopaswa kuangaliwa na Van Gaal, sasa aonyeshe ubora wa ujuzi wake.

Man U katika msimamo wa Premier
                                 P       W      D       L       GF    GA    GD    Pts
4. Man United    35     19       8       8       59     35     24     65


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic